|
|
RABI TWEPUSHE NA NARI
Date: 04 November, 2004
- Hamdu za Maulana, Muumba janna na nari
Wokovu Ya Rabbana, maasi yamekithiri
Viumbe twatafunana, kimetuzidi kiburi.
Yatuaga Ramadhani, Rabbi twepushe na Nari.
- Kumi la mwisho mwungwana, jiweke mbali na shari
Ya shetani mwenye lana, asi wa Allah Qahari
Atujia kwa mapana, kuzishawishi suduri
Yatuaga Ramadhani, Rabbi twepushe na nari.
- Tutiye moyo dhamiri, tusijifanye hodari
Jahanamu kali nari, huwakumba majabari
Huchoma na kuadhiri, wakosefu makafiri
Yatuaga Ramadhani, Rabbi twepushe na nari.
- Saumu ituathiri,tutubu dhambi tukiri
Wanojitia ghururi, Haawiya yawasubiri
Watachomwa matajiri, wa inda wenye viburi
Yatuaga Ramadhani, Rabbi twepushe na nari.
- Nyoyo zikose sururi, kuasi si ufakhari
Pokea langu shauri, sijitie ujabari
Mja ngia tahayuri, hakuna jambo la siri
Yatuaga Ramadhani, Rabbi twepushe na nari.
- Mwenzangu ngia nadhari, utende lilo la kheri
Tambua Mola Qahari, yuko nawe huna siri
Alijua la dhahiri, na la batini vizuri
Yatuaga Ramadhani, Rabbi twepushe na nari.
- Jahanamu yavinjari, yawangoja majeuri
Na wale wasofikiri, wapenda umashuhuri
Wala hawangii ari, kurejea kwa Ghafuri
Yatuaga Ramadhani, Rabbi twepushe na nari.
- Wakiasi hawajali, wapenda sifa titiri
Nyoyo kama majabali, kamwe hazingii nuri
Hawasimami kusali, wamwasi Allah dhahiri
Yatuaga Ramadhani, Rabbi twepushe na nari.
- Nakhatimisha qauli, kiyama siku hatari
Funga ziwe maqubuli, hiyo siku ya hashiri
Twakuomba ya Jalali, Ya Alimu ya Jabbari
Yatuaga Ramadhani, Rabbi twepushe na nari.
Ahmed Rashid.
|