|
|
YUWAJA MGENI WETU
Date: 28 September, 2004
- Ya Allahu ya Karimu, Rahimu ya Rahmani
Ya Rabi Mola Adhimu, hamdu zako Manani
Amani kwa muadhamu, Rasuli wa tumaini
Yuwaja mgeni wetu, kipenzi chetu azizi.
- Naikumbusha qaumu, habibu yuko njiani
Ni johari mahashumu, waridi la busitani
Fakhari ya Isilamu, dhahabu tuitunzeni
Yuwaja mgeni wetu kipenzi chetu azizi.
- Wekuja musitaqimu, wajumbewe barazani
Kuitangaza saumu, Rajabu na Shaabani
Tukawaona ni sumu, ujinga metuzaini
Yuwaja mgeni wetu, kipenzi chetu azizi.
- Tujiandae muamu, kukaribisha mgeni
Tujongee kwa Rahimu, kwa tahajudi nyumbani
Tujipambe kwa saumu, na sala misikitini
Yuwaja mgeni wetu, kipenzi chetu azizi.
- Tusingoje baragumu, tukajajuta usoni
Qiyama siku ni ngumu, liqau kwa Rahmani
Anza sije jilaumu, kesho kesho hadi lini
Yuwaja mgeni wetu, kipenzi chetu azizi.
- Inawirishe kaumu, msifika Ramadhani
Twakusubiri kwa hamu, pingu atiwe shetani
Fika baki humu humu, siende twakutamani
Yuwaja mgeni wetu, kipenzi chetu azizi.
- Sabau kwa hii zamu, beti chache nabaini
Ramadhani tufahamu, tu wageni wa Manani
Vipi tumekosa hamu, hatufungi Shaabani?
Yuwaja mgeni wetu, kipenzi chetu azizi.
Ahmed Rashid.
|