.

Welcome to Zanzinet Swahili Poems

Where Swahili matters!

Ameumbwa Malkiya

 

 

 

 

 

 

Related links

Ameumbwa Malkiya

Date:  25 July 2005

  1. Karibu ya yangu macho, mbele kanisimamiya
    Na kila alicho nacho, kamili kimetimiya
    Amira hana kificho, peke yake malkiya

  2. Dunia ameumbiwa, aiamuru ni yake
    Na taji alilopewa, halina mfano wake
    Kichwani katunukiwa, vito vyote pambo lake

  3. Vingi visivyo idadi, vinashindana kung'ara
    Almasi zumaridi, kama nyota zake sura
    Yakuti zabarijadi, zimeshikana imara

  4. Yake shingo menyo'oka, dede imemsimama
    Kifua kisicho shaka, kimemnyanyuka wima
    Kimwana ameumbika, huchoki kumtazama

  5. Uso umemkunjuka, amejawa na bashasha
    Anakenya mkicheka, jambo la kufurahisha
    Hasa panapo dhihaka, na meno hukuonesha

  6. Mungu kampa kipawa, hadhi yake kumuona
    Kwa uzuri alopewa, hamna wa kufanana
    Mrembo wa kushtuwa, mtoto bado kijana

Maher ( Unique )

  About Us | Zanzinet Home | Contact Us | ©2004-2006 Zanzinet