.

Welcome to Zanzinet Swahili Poems

Where Swahili matters!

Kuna Siku Yatakwisha

 

 

 

 

 

 

Related links

Kuna Siku Yatakwisha

Date:  11 December, 2005

  1. Mungu atupe subira, na nyingi stahmala
    Itushukie nusura, wahizike zao hila
    Iwangie khofu mara, iwatoke kwa ghafula
            Kama ndoto walo lala
  2. Yana tutia uchungu, kila mara tukiona
    Kupigwa watu virungu, hata sababu hapana
    Wanatugawa mafungu, kwa chuki zisizo mana
            Kwa hili hamtapona
  3. Huku kutu dhalilisha, nako kuna mwisho wake
    Kuna siku yatakwisha, yaondoke yende zake
    Hawatodumu maisha, Mungu ana siri yake
            Tusubiri tusichoke
  4. Wangapi wameondoka, wameiaga dunia
    Walio wakidhihaka, majumba kutuvunjia
    Wakapita wakicheka, mabaya kufurahia
            Hawapo wamejifia
  5. Hapa palipo bakia, padogo simbali tena
    Muhimu kuvumilia, machungu tunayoona
    Tuwe shujaa wa nia! , pamoja kushikamana
            Tuangaze mbele sana

Maher ( Unique )

Kuna Siku Yatakwisha

Date:  12 December, 2005

  1. Usemayo nawafiki, yatakwisha masahibu
    Masahibu na mikiki, kuteswa bila sababu
    Sababu kudai haki, kudai bila harubu
            Harubu si mwendo wetu
  2. Yatakwisha ya dhuluma, na watu kuadhibiwa
    Kuadhibiwa kwa chama, wengi walokichaguwa
    Walokichaguwa vyema, sio kulazimishiwa
            Kulazimishiwa na wasio wetu
  3. Watu sasa wamechoka, na matumizi ya dola
    Dola ilojipachika, kwa mabavu kutawala
    Kutawala kwa shabuka, na majeshi wasolala
           Wasolala kwa hofu ya umoja wetu
  4. Matumizi ya mabavu, ndio kubwa yao ngao
    Ngao yetu utulivu, hatujali nguvu zao
    Zao nguvu za uovu, hazilindi roho zao
            Roho zao, mjuzi ni Mola wetu
  5. Kubwa wanaloliweza, ni kuchelewesha siku
    Siku ya Mola muweza, alopanga tuwapiku
    Tuwapiku kuongoza, hakuna mtafaruku
           Mtafaruku wa nani kiongozi wetu

Kassim O. Ali

  About Us | Zanzinet Home | Contact Us | ©2004 Zanzinet