.

Welcome to Zanzinet Swahili Poems

Where Swahili matters!

Kukimbia Nyuki

 

 

 

 

 

 

Related links

Kukimbia Nyuki

Date: 30 November, 2005

  1. Asadi etuhiliki, Kwenda tukumbusha leo
    Mbona wengine hataki, Afanya mapendeleo
    Au ni mtu wa chuki, Ataja watu kwa vyeo?
    Kweli Kukimbia Nyuki, Mashekhe Mbio ni Bora

  2. Pee na Mchina Tambi, Na huyu hukumtaja
    Makumba etoka Bambi,Alojifunga mkaja
    Ekuja siku za kambi, Kudondoa moja moja
    Kweli Kukimbia Nyuki, Mashekhe Mbio ni Bora

  3. Asadi usisahau, Au wajikurupusha?
    Na ikiwa ni dharau, Neepo nakukumbusha
    Hiyo siku ya pilau, Ndama tulipoangusha
    Kweli Kukimbia Nyuki, Mashekhe Mbio ni Bora

  4. Kama malenga njoo, Tena takupa na noti
    Mustafa Abdoo, Fundi dereva wa boti
    Echota wali kwa ndoo, Na Athumani makoti
    Kweli Kukimbia Nyuki, Mashekhe Mbio ni Bora

  5. Alokabidhiwa supu, Sulemani Mkojani
    Hawi mikono mitupu,, Eujaza pakachani
    Ana watoto gurupu, Wamngojea nyumbani
    Kweli Kukimbia Nyuki, Mashekhe Mbio ni Bora

  6. Ee Moh'd Khamisi, Mugheri washindwa kazi
    Wajidai udadisi, Kwenda wasema wazazi
    Wabakia mufilisi, Kutaja wote huwezi
    Kweli Kukimbia Nyuki, Mashekhe Mbio ni Bora

  7. Basi nitakutajia, Tena mmoja mmoja
    Wa mwanzo aloingia, Buda Baniani koja
    Na mbeba sufuria, Kijasho Kinamtoja
    Kweli Kukimbia Nyuki, Mashekhe Mbio ni Bora

  8. Akaja na babu yangu , Ati enda na wenziwe
    Alonambia mwanangu, Selemu leo ingiwe
    Tuache bodo na changu, Msi mwana lake jiwe
    Kweli Kukimbia Nyuki, Mashekhe Mbio ni Bora

  9. Wamjuwa Koti nje, Au hujamsikia
    Bwana akipenda punje, Nyali akifuatia
    Ni karibu azionje, Nyuki wakamrukia
    Kweli Kukimbia Nyuki, Mashekhe Mbio ni Bora

  10. Na kina mama kaumu, Wengi walihudhuria
    Kirongozi Bisaumu, Ama huyu twakambia
    Euna kama sumu, Wali akaukimbia
    Kweli Kukimbia Nyuki, Mashekhe Mbio ni Bora

  11. Na mwalimu wa sukuli, Alokuja na mwanawe
    Alimpiga chuchuli, Kamwambia usinawe
    Hawa si nyuki ni nduli, Wataka roho watwawe
    Kweli Kukimbia Nyuki, Mashekhe Mbio ni Bora

  12. Nikifika thinashara, Aghlabu siongezi
    Mana sina mshahara, Na wala hii si kazi
    Lakini leo tan'gara, Japo nikose mchuzi
    Kweli Kukimbia Nyuki, Mashekhe Mbio ni Bora

  13. Ni mambo ya mwaka huu, Na wala hayatajiki
    Nakumbuka Mabuluu, Ni mkali hafikiki
    Al-Bahri yu juu, Kipangani "Si riziki”
    Kweli Kukimbia Nyuki, Mashekhe Mbio ni Bora

  14. Kibwanga chesalimika, Si mtu wa kuokota
    Alikuwa yu Msuka, Ana gari akokota
    Naye angekaza shuka, Kwa tumbo kumsokota
    Kweli Kukimbia Nyuki, Mashekhe Mbio ni Bora

  15. Na Awadhi Mshihiri, Ee jamani ni mambo
    Afadhali kumsiri, Ndiye fundi wa mitambo
    Wanzake walikithiri, Walimfanya ni chambo
    Kweli Kukimbia Nyuki, Mashekhe Mbio ni Bora

  16. Huyu tulikwishajua, Kuwa yeye nuksani
    Ee auza halua, Anunue kitu gani
    Ni kuwa zimpungua, Wakutiwa gerezani
    Kweli Kukimbia Nyuki, Mashekhe Mbio ni Bora

  17. Ama Amuri wa Konde, Gando si kwao asili
    Aliyakata mabonde, Tena kwa dakika mbili
    Wacha matope aponde, Udhani hana akili
    Kweli Kukimbia Nyuki, Mashekhe Mbio ni Bora

  18. Mapicha asiye hoja, Mtu wa Majimbikani
    Ni bado kujikongoja, Ati yeye ni jirani
    Asema kwanza angoja, Pilau ije nyumbani
    Kweli Kukimbia Nyuki, Mashekhe Mbio ni Bora

  19. Kabwera bado mdogo, Na tena anachechea
    Kazi kuchoma muhogo, Na nguru kutoela
    Pahala palipo zogo, Asema hakuzoea
    Kweli Kukimbia Nyuki, Mashekhe Mbio ni Bora

  20. Latubi wake usugu, Ekataa kukimbia
    Mtu huyu hana ndugu , Pemba na Unguja pia
    Yeye ajifanya njugu, Alijivika gunia
    Kweli Kukimbia Nyuki, Mashekhe Mbio ni Bora

  21. Chumbuni na Pakashume, Hata Mdabi wa Bule
    Walijifanya vidume, Lazima wali waule
    Basi wache wangurume, Nyuki wapata tungule
    Kweli Kukimbia Nyuki, Mashekhe Mbio ni Bora

  22. Chani etoka Limbani, Na bakora mkononi
    Epita njia za ndani, Hakupitia sokoni
    Basi efika Pandani, Njia ya kwao haoni
    Kweli Kukimbia Nyuki, Mashekhe Mbio ni Bora

  23. Najuta kukulaumu, Mana ni wengi siweshi
    Kule kufanya ugumu, Ni bure hatuchokeshi
    Kumbe viumbe wagumu, Asonacho hakopeshi
    Kweli Kukimbia Nyuki, Mashekhe Mbio ni Bora

  24. Sasa nisifu karamu, Wali ulivyopikika
    Na nyama ilivyo tamu , Ukigusa yamezeka
    Kwa samli kemkemu, Yatoja ikianguka
    Kweli Kukimbia Nyuki, Mashekhe Mbio ni Bora

  25. Tonge bila ya mpango, Usitafune wameza
    Machaza na machinyango, Sio muengo wa pweza
    Kutwa uwazi mlango, Bwana Issa etuweza
    Kweli Kukimbia Nyuki, Mashekhe Mbio ni Bora

  26. Ela wawapi walaji , Wote washapiga mbio
    Baki kuponea maji, Hapakupikwa vijio
    Betri hazina chaji, Lala usage sikio
    Kweli Kukimbia Nyuki, Mashekhe Mbio ni Bora

Kutoka gazeti la Istiqama, mtungaji hajulikani
Limetwa na Suleiman Al Abdely

  About Us | Zanzinet Home | Contact Us | ©2004 Zanzinet