.

Welcome to Zanzinet Swahili Poems

Where Swahili matters!

Kukimbia Nyuki

 

 

 

 

 

 

Related links

Kukimbia Nyuki

Date: 02 December, 2005

  1. Hazikuwa tungo zangu, zangu hazina vihere
    Nalalama kwa uchungu, Salehe hewe taire
    usitutwange mizungu, ukanivisha shemere
    Kweli Kukimbia Nyuki, Mashekhe Mbio ni Bora

  2. Yalotokea Selemu, yalihanikiza Wete
    Nyuki walifata tamu, ilosongwa na Mapete
    Yeye ni watakarimu, wa akidi na wa fete
    Kweli Kukimbia Nyuki, Mashekhe Mbio ni Bora

  3. Mahiri kawa kidumu, asema asolijuwa
    Kasikia kwa mwalimu, Saidi wa Madaniwa
    Pariwala yu wa damu , kwa pilau utapowa
    Kweli Kukimbia Nyuki, Mashekhe Mbio ni Bora

  4. Wakafika wahudumu, kwa austini ya chani
    Wakazidi pata hamu, walotokea Limbani
    Likapigwa baragumu, bondeni na Kipangani
    Kweli Kukimbia Nyuki, Mashekhe Mbio ni Bora

  5. Bwana Juma wa Junguni, akaja kapanda punda
    Na mpwawe wa Shebani, na wakweze wa Kidunda
    Wamepania kwa kani , kusafi yaliyovunda
    Kweli Kukimbia Nyuki, Mashekhe Mbio ni Bora
  6. Likaingiya gurupu, warabu wa Mkanjuni
    Hawa wazijua supu, na lozi za maruhani
    Hatoki mtu patupu, pamefikwa shughulini
    Kweli Kukimbia Nyuki, Mashekhe Mbio ni Bora

  7. Bado viroja vimbali, kaja bwana Khalfani
    Mshenga wa serikali, na mwamba maarusini
    Katu ndoa si kabuli, usipompa saini
    Kweli Kukimbia Nyuki, Mashekhe Mbio ni Bora

  8. Joshi likahanikiza, kwa maudi na marashi
    Rubuni wakaekeza, kwa vazi la wanawashi
    Miwani-mdogo raza, ndie alieshawishi
    Kweli Kukimbia Nyuki, Mashekhe Mbio ni Bora

  9. Kanga za chapa kipanga, ndizo sare za arusi
    Palisadifu malenga, waloghani yasotusi
    Hakuna alojitenga, siku hiyo mahususi
    Kweli Kukimbia Nyuki, Mashekhe Mbio ni Bora

  10. Walipopanda sahari, wanafunzi wa sharifu
    Wanotawala membari, za maulidi na dufu
    Wazoefu wa viriri, kwa kasida usikhofu
    Kweli Kukimbia Nyuki, Mashekhe Mbio ni Bora

  11. Ndipo tulipokisia, kuwa ya kale nadhifu
    Kwani yaliashiria, kwenye safu ya machifu
    Maami walotulia, mashekhe waadilifu
    Kweli Kukimbia Nyuki, Mashekhe Mbio ni Bora

  12. Kina Sudi wa Mponda, na Abedi Daftari
    Shununi wa njia panda, na Yasini Daktari
    Hapo mambo yaliwanda, Pilau wakasubiri
    Kweli Kukimbia Nyuki, Mashekhe Mbio ni Bora

  13. Mara kiwingu chatanda, si cha maji ni cha shari
    Wadudu walipotanda , hawesubiri bukhuri
    Waliyawacha matunda, na utamu wa sukari
    Kweli Kukimbia Nyuki, Mashekhe Mbio ni Bora

  14. Vilivamiwa vilemba, kwenye safu mukhtari
    Mashekhe waliovimba, kwa elimu za akheri
    Nyuki waliwasirimba, kheri ikazaa shari
    Kweli Kukimbia Nyuki, Mashekhe Mbio ni Bora

  15. Tulistirika sisi, tulovaa suruali
    Wakatekwa waasisii, ukapotea muhali
    Hapakuwa na jinsi, mbio ni mustakabali
    Kweli Kukimbia Nyuki, Mashekhe Mbio ni Bora

  16. Mahiri kasimlia, bila hata ya kujali
    Mengi aloyasikia, hakufumba kwa mithali
    Wengine twayachukia, waungwana kawafeli
    Kweli Kukimbia Nyuki, Mashekhe Mbio ni Bora

Sultan Ahmed

  About Us | Zanzinet Home | Contact Us | ©2004 Zanzinet