|
|
Mtukufu Ramadhani
Date: 19 September, 2005
- Kwa jina lako Rahimu, naanza kusimuliya
Mola wetu Mkarimu, Ya Rabi nijaaliya
Nikadiri kukhitimu, haya nalokusudiya
Niusifu mwezi mwema, mtukufu Ramadhani
- Rabi peleka salamu, zende kwa wetu Nabiya
Mtume wetu Adhimu, Muhamadi Hashimiya
Na Swahaba Akiramu, na Isilamu jamiya
Niusifu mwezi mwema, mtukufu Ramadhani
- Ya Rabi tupe mwafaka, tufunge bila udhiya
Saumu yenye baraka, kwako twaitaradhiya
Tuifunge huno mwaka, na mwakani kwa afiya
Tuufunge mwezi mwema, mtukufu Ramadhani
- Karibu wetu mgeni, kwa hamu twakungojeya
Ulotukuka yakini, nuru ulivyo eneya
Mtukufu Ramadhani , karibu twakupokeya
Kongo mwezi wetu mwema, mtukufu Ramadhani
- Mtakatifu adhimu, sote twakukongoweya
Mwezi uliye muhimu, Mola met’utunukiya
Twafurahi Isilamu, kila pembe ya duniya
Kongo mwezi wetu mwema, mtukufu Ramadhani
- Mtukufu mwezi mwema , wa sisi kunyenyekeya
Mwenye kuyatenda mema , bila ya kufanya ri’ya
Tamswamehe Karima , madhambi kumfutiya
Kongo mwezi wetu mwema , mtukufu Ramadhani
- Mwezi wa nyingi faida , metukuzwa na Jaliya
Mwezi mwema wa Ibada , na imani kutungiya
Huondoka zote shida , nafusi zikatuliya
Kongo mwezi wetu mwema , mtukufu Ramadhani
- Mwezi huno wa maana , ameusifu Nabiya
Ni bora wajulikana , kwa kheri nyingi kungiya
Mwezi wa neema sana , baraka hutushukiya
Kongo mwezi wetu mwema , mtukufu Ramadhani
- Mwezi mwema wa swiyamu , wa mema kujichumiya
Milango ya Jahanamu , Rahimu huifungiya
Na ya Janatu Naimu , wazi hutufunguliya
Kongo mwezi wetu mwema , mtukufu Ramadhani
- Ni mwezi wa Quraani , mwanzo kuteremkiya
Alipokuja pangoni , Jibirili kwa Nabiya
Ilikiuwa Ramadhani , wah’ayi alipokeya
Kongo mwezi wetu mwema , mtukufu Ramadhani
- Mashetani makafiri , wawi wa kuharibiya
Hawawezi kuathiri , wasiwasi kututiya
Huwafungia Qahari , mbali wakatokomeya
Kongo mwezi wetu mwema , mtukufu Ramadhani
- Imo Lelatil Qad’ri , usiku huo kungiya
Bora sana mashuhuri , kuliko elifu moya
Miezi inayo jiri , ya taqwimu Hijiriya
Kongo mwezi wetu mwema , mtukufu Ramadhani
- Na hushuka Malaika , mbinguni wakatokeya
Kwa amri ya Rabuka , duniyani kufikiya
Amani hunawirika , hadi swabahi kungiya
Kongo mwezi wetu mwema , mtukufu Ramadhani
- Usiku mwema kipita , wakati huo kungiya
Na ukija kukukuta , Ibadani umengiya
Hakika utaipata , Rehema yake Jaliya
Kongo mwezi wetu mwema , mtukufu Ramadhani
- Haya basi Isilamu , mgeni ashaingiya
Natutimize saumu , tuifungeni kwa niya
Swala zote tuzikimu , za suna na faridhiya
Kongo mwezi wetu mwema , mtukufu Ramadhani
- Mashekhe na masharifu , wahimizeni jamiya
Hima tufungeni safu , Tarawehe kuqimiya
Tumlekee Raufu , kwa kuomba na kuliya
Kongo mwezi wetu mwema , mtukufu Ramadhani
- Darasani tuhimize , wenzetu kuhudhuriya
Kwa wakati tufulize , misikitini kungiya
Mawaidha tusikize , atatujazi Jaliya
Kongo mwezi wetu mwema, mtukufu Ramadhani
- Haya shime muombeni , Mola kumnyenyekeya
Quraani isomeni , kila siku juz’u moya
Mukiweza ongezeni , muzidi kukaririya
Kongo mwezi wetu mwema , mtukufu Ramadhani
- Na akhiri nimefika , beti nalokusudiya
Chache naloziandika , tosha kumi na tisiya
Namshukuru Rabuka, shairi limetimiya
La kuswifu mwezi mwema, mtukufu Ramadhani
- Amina Rabi Dayani , Dua yetu kubaliya
Ya Ilahi tuauni, tuepushe na udhiya
Tuifunge Ramadhani, kwa furaha na afiya
Twaomba yake neema, mtukufu Ramadhani
Shairi: Bw. Swaleh Suheil Abedi
Limeletwa na Sheikh Muhammad Faraj Salim
|