|
|
MZEE AMETUTOKA
Date: 03 March, 2005
Shairi la kumkumbuka mzee wetu aliyefariki baada ya miezi miwili na
nusu ya kusumbiliwa na stroke. Inna lillah wa inna illaihi rajiun.
Inshaallah Mola atamrehemu yeye na wote kabla yake
Shairi hili limetungwa na mwanawe.
- Bisimillahi naanza, Nakusalia nabiya
Mengi nitoyaeleza, Yafaa kuzingatiya
- Namshukuru karima, Nafasi kunijaaliya
Utenzi kuja kusoma, Wa wetu mtanguliya
- Baba Mwema katutoka, Akhera katanguliya
Machozi kwetu yatoka, Kikumbuka mazoweya
- Mlezi kaenda zake, Kamwe hutomsikiya
Kaondoka peke yake , Molatamu hurumiya
- Miyoyo yaingia fundo, Tangu alipojifiya
Kaondoka kwa kishindo, Mzee katukimbiya
- Ugonjwa ulomteka , Akaiwaga duniya
Tulombali twateseka , Japo kwake karidhiya
- Japokuwa kateseka, Maradhi kumpindua
Hikima yake rabuka, Mola hakumuonea
- Dhunubu kumfutia , Peponi apatengiya
Kwake na kwa sote umma, na waliyo tanguliya
- Ashura ni siku njema, Sabahi kakhitajiwa
Siku yake ya siyama, Raby kamra hisishiya
- Ami yetu alopema, Dua aki muombeya
Nduguye aliyomwema , Kibaki kujinamiya
- Maziko yalojazana, Rehema akiombewa
Kapelekwa kwa amana, Kituoni katuliya
- Dhiki zikitusakama , Nani tutamliliya
Msikizaji kahama, Khofu kwetu zabakiya
- Nguzo njema yavunjika , Mola tatusaidiya
Viumbe sote twapita , Hakuna atobakiya
- Ukweli usopingika, Kikumbuka waumiya
Mwema wetu katutoka, Mzee katangauliya
- Haki yaumiza sana, Raby tusahilishiya
Mrehemu yarabana, Na wote watanguliya
- Tuauni subuhana , Tusije tukapoteya
Twakwita kwa lako jina, Karima Tusaidiya
- Mema alotutendea, Vipi tutamlipiya
Mola alomjaliya, Kwake akijitoleya
- Kwa wana na wengi Umma, Sote katusaidiya
Nini tufanye la mama, Baba kumsaidiya
- Tukumbuke wake wema, Dua tukimuombeya
Kwake Jannatunaima , Mola tam ruzukiya
- Tusimsahau Mwema, Usiya alotwachiya
Fattima Kumtizama, Ili apate ridhiya
- Mlezi kutanguliya, Siyo kama kapoteya
Tatukutanisha naya, Mema tuki jitendeya
- Dua njema tupatapo, Na sadaka mtoleya
Tusalipo tuombapo, Mema tukimtakiya
- Mpe nguvu wetu Mama, Na wazazi jumuiya
Afya na umuri mwema, Walikatika duniya
- Yamani tukidhiya, Haja zetu kisikiya
Wote walotanguliya, Ghafuru Tawajaaliya
- Khusunul khatima njema, Tulobaki tujaliya
Qalima Tukiisema, Tuiwagapo duniya
- Tupate wakutuzika, Mema waki tuombeya
Mzee awe kafika, Peponi Kitungojeya
- Muweza wa yote piya, Dua tuta qabaliya
Kwa pekee msikiya, Kwako tuna tegemeya
- Twaitikia labeika, Waja kwako twatubiya
Situwache kuteseka, Na mwsiho tukapoteya
- Amina Raby Amina, Rasuli Twamsaliya
Kwa baraka zake Bwana, Maombi tu pokeleya
Imeletwa na Anonymous
|