|
|
Nguvu za Mola
Date: 20 August, 2005
- Nguvu zao na za Mola, Ni zipi zilo shadidi
Kula,kunywa na kulala, Mola ndiye mfanidi
Mwenye hekima na hila, Pia na nguvu shadidi
Nguvu zao na za Mola, Ni zipi zilo shadidi
- Sitaikata tamaa, Kufanikiwa muradi
Nangojea yangu saa, Saa ya Sada na Sudi
Dini yetu ndio taa, Yamurika mahasidi
Nguvu zao na za Mola, Ni zipi zilo shadidi
- Ukilea mwana mwema, Mola atampa sudi
Nazo tumwa za rehema, Za Mtume Muhammadi
Zitakutunza makama, Siku isiyo baidi
Nguvu zao na za Mola, Ni zipi zilo shadidi
- Ama wanotakaburi, Mashetani wa Biladi
Kuna siku ya khatari, Anokwenda hatarudi
Njia yetu ni kaburi, Njia ilo maridadi
Nguvu zao na za Mola, Ni zipi zilo shadidi
- Amali ulizotenda, Ndizo zinokupa kadi
Roho itakapokwenda, Mbele ya Mola wadudi
Utaoneshwa sana, Na hilo halina budi
Nguvu zao na za Mola, Ni zipi zilo shadidi
- Waliasi makafiri, Na kujitia taadi
Wakijiona hodari, Kumtesa Muhammadi
Roho zao zikiguri, Usiyahi utanadi
Nguvu zao na za Mola, Ni zipi zilo shadidi
Shairi : Maalim Abbas M. Mdungi
Limeletwa na Salma Said katika Makala ya Nabwa
|