.

Welcome to Zanzinet Swahili Poems

Where Swahili matters!

Wanichukia

 

 

 

 

 

 

Related links

Wanichukia

Date:  06 December, 2005

Nawasilisha hapa shairi lililoandikwa na ndugu yetu, Khatib Mohammed Khatib, ambaye baada ya uchaguzi wa mwaka huu hapa petu ni miongoni mwa wanaokumbwa na vitimbi vya chuki ya ubaguzi iliyomezeshwa kusudi vichwani mwa Wazanzibari.

Anaishi eneo la Fuoni, Wilaya ya Magharibi, na kuna bwana mmoja ambaye amekuwa akiingia katika himaya yake na kumfanyia uharibifu wa makusudi huku akijigamba: "Nyinyi ni wakuja tu hapa. Nani atakayenizuia mimi?"

Bahati mbaya, Khatib hajawa mwanachama wa ukumbi huu, lakini aliniomba ikiwa naweza kumpatia bega la kulilia huzuni zake popote pale pawapo. Nami nikaona katika ukumbi huu muna Wazanzibari wenzake ambao wanaweza kulia naye kilio.

  1. Unanichukia bure, sababu usuli wangu
    Waniombea nirure, yanishukie machungu
    Kwa lolote unikere, usonone moyo wangu
    Ni bure wanichukia
  2. Unanifanyia shere, wauviza utu wangu
    Wanipigia misere, hadi barazani kwangu
    Wasema hatuwi sare, wanifanyia mizungu
    Wanichukia bure
  3. Waniletea ukware, wanibughudhi kwa vyangu
    Nikijikuna upere, waungulika mwenzangu
    Kama kikuku kuchere, waniinga nendezangu
    Ni bure wanichukia
  4. Cheo cha mwanasesere, kwako ndiyo hadhi yangu
    Wanichomeka mishare, wakazia na marungu
    Nipige uniburure, mimi namwachia Mungu
    Wanichukia bure
  5. Nimeshakuwa bwerere, mbeleyako mlimwengu
    Wanipiga sasambure, wanivunjia na vyungu
    Illahi si “kamzore”, anayo yako mafingu
    Ni bure wanichukia
  6. Tunduni kama “tetere”, taabani haliyangu
    Ninahofu, tere - tere, sina hata “sungu sungu”
    Wavizia unipore, “yaailahi mola wangu”
    Wanichukia bure
  7. Ya Rabi hapa nikore, nalibana chozi langu
    Uwabane waniture, ya Rabi wababe wangu
    Migongoni uwachore, “WASALITI ULIMWENGU”
    Wanichukia bure
  8. Nyuso zao wazipare, ziwe weusi wa chungu
    Waongezewe upere, wajipare kwa uchungu
    Wakome kiherehere, sili sili ziwe pingu
    Wanichukia bure
  9. Kula yao wachekure, wangie kizungu zungu
    Nyonga zao waburure, kama kidege makungu
    Wajue waja si bure, dhuluma jazaye chungu
    Ni bure wanichukia

Limetungwa na Khatib Mohammed

Limeletwa na Mohammed Mohammed

Wanichukia

Date:  07 December, 2005

  1. Huyo akucheza shere, akuzongezonge pingu
    Kelele zisikukere, aso mtu ana Mungu
    Yamemshinda Mabere, aweje mramba vyungu,
    Ni bure akuonea.
  2. Utamsibu upere, ajikune rwangu rwangu
    Hata mbele ya wavyere, soni hana mpwa wangu
    Angie kiherehere, ishamshinda mizungu
    Lako shitakia Mungu.

Ahmed Rashid.

Wanichukia

Date:  07 December, 2005

  1. Napenyeza yangu pyere, ndani ya shairi langu
    Ukweli meona gere, gere la haki si jungu
    Shairi tamu ya ndere, kuletwa bila virungu
    Vumilia,
  2. Naomba ndugu wa "kureeee!!", uvumilie viwingu,
    Usipige "makerere", bora nyamaza kizungu
    Sheria kazipekure, pia muombe na Mungu
    Vumilia.

Mohammed Omar

Wanichukia

Date:  07 December, 2005

  1. Ndugu zangu sikizeni, haya ninayowambia
    Musiwe malimbukeni, watu kuwatumilia
    Mukaingia vitani, bila nyinyi kujijua
    Majuto ni mjukuu, Kilio huja mwishoni
  2. Vita hivi ni ya nani, ndugu mnatumiliwa
    Silaha zimkononi, Nyote mmedhamiria
    Tusichezee wattani, tutakuja jijutia
    Majuto ni mjukuu, kili huja mwishoni
  3. Kila mshika mpini, silaha kuichezea
    Aangalie ni nani, aliyemkusudia
    Ni ndugu wa ubabani, au wa mama mmoya
    Majuto ni mjukuu, Kilio huja mwishoni
  4. Tutakuwa simanzini, siku moja nawambia
    Tutajiuliza moyoni, kilio tutaomoa
    Hatuuoni wattani, sasa umetukimbia
    Majuto ni mjukuu, vilio huja mwishoni
  5. Wa kulaumiwa nani, ukweli utawadia
    Ni ndugu wa maduguni, au ni wa tumbo moja
    Au ni yule jirani, Ndie alotuchezea
    Majuto ni mjukuu , Vilio huja mwishoni
  6. Watoto wetu mashaka, ndio yatayowavaa
    Si mtoto wa Mashaka, Wala wa ndugu Vua
    Wote watapita shida, familia itasambaa
    Vilio vitawajaa, Majuto yatatovaa.
  7. Haraka imenizidi, mimi mwingi wafadhaa
    Wattani si ufaidi, ugeni umenijaa
    Kalamu naweka chini, ninakimbia udhia
    Majuto ni mjukuu, Vilio huja mwishoni

Anonymous-126

  About Us | Zanzinet Home | Contact Us | ©2004 Zanzinet