.

Welcome to Zanzinet Swahili Poems

Where Swahili matters!

Msalieni Nabiya (S. A. W.)!

 

 

 

 

 

 

Related links

Msalieni Nabiya (S. A. W.)!

Date:  19 April, 2006

  1. Mola amemswalia, Kipenzi chake Hashimu
    Kisha wakafuatia, Malaika wakarimu
    Na nyinyi umma jamia, Swalini mumsalimu
    Msalieni Nabiya, Na ali zake kiramu

  2. Na Swahaba zake pia, Ziwafikie salamu
    Wao walitangulia, Kunusuru Isilamu
    Yarabi Mola Jalia, Waja wako warehemu
    Msalieni Nabiya, Na ali zake kiramu

  3. Kifua kapanuliwa, Hana shaka wala dhana
    Utajo kanyanyuliwa, Kwa shahada na adhana
    Mizigo kaondolewa, Dini yake ikafana
    Msalieni Nabiya, Na ali zake kiramu
  4. Katuletea risala, Ujumbe kaueneza
    Kaamsha walolala, Wakauona mwangaza
    Mefika kila mahala, Nuru ameisambaza
    Msalieni Nabiya, Na ali zake kiramu

  5. Kakileta Jibrili, Mtume kakipokea
    Kitabu kilo kamili, Kiso shaka Katwambia
    Na vizimwe vibatari, Mwanga ushatufikia
    Msalieni Nabiya, Na ali zake kiramu

  6. Kandili zote zimeni, Tunacho cha kuonea
    Maneno Yake Manani, Risala ilotimia
    Uwongofu Qur-ani, Kwa amchae Jalia
    Msalieni Nabiya, Na ali zake kiramu

  7. Kote zimeshaenea, Baraka za Subuhana
    Nuru katufikishia, Muhamadi kwa amana
    Nasi tumeipokea, Jamii muuminina
    Msalieni Nabiya, Na ali zake kiramu

  8. Kitabu hiki adhimu, Mola ameweka wazi
    Kupitiwa na kalamu, Za viumbe hakiwezi
    Jinni wala binadamu, Kakihifadhi Mwenyezi
    Msalieni Nabiya, Na ali zake kiramu

  9. Sunnah ilotahirika, Kufuata ni lazima
    Mafunzo yenye hakika, Ilimu na tarjima
    Ni kauli ziso shaka, Maneno aliyosema
    Msalieni Nabiya, Na ali zake kiramu

  10. Awe ruwaza njema, Annabiyul khatimu
    Tusiwe tu twasema, Tufuate kwa timamu
    Kufuata ndiko kwema, Uzushi hautodumu
    Msalieni NabiyaNa ali zake kiramu
  11. Ya Rabbi Mola Adhimu, Tunakuomba atiya
    Ya Rabbi utukirimu, Utuweke na Nabiya
    Na Sahaba wakarimu, Walofuata yake njia
    Msalieni Nabiya, Na ali zake kiramu

 

Muhammad Faraj Salem Al Saiy

  About Us | Zanzinet Home | Contact Us | ©2004-2006 Zanzinet