|
|
Yaliyomkuta Sahib yangu!
Date: 01 June, 2006
- Nnasahibu mpenzi,umri wake makamo
Amejitia kitanzi,moyoni ndimo kiwamo
Kampata mwanagenzi,mwari na chake kisomo
Utadhani mbaa'mwezi,mashaalla ana kimo
- Alikuja nishauri,kuwa anakwenda posa
Nikamwambia subiri,ndoa inataka pesa
Na kanzu ilonzuri,na naali za kisasa
Hakupinga akakiri,kingoja yangu ruhusa
- Nyuma akanizunguka,akenda kwa baba'ake
Asimkute katoka,mama yupo peke yake
Maneno yalomtoka,kuwa anataka mke
Mama roho menutsuka,akamwambia atoke
- Machozi yanamtoka,kaja kwangu analia
Huku akinung'unika,hajui lakunambia
Mambo yameshamfika,asiyo yatarajia
Kahisi keshamtoka,hakuna nyengine njia
- Tukaifunga safari,kumtafuta babaye
Ilikuwa laasiri,tulipo onana naye
Tukampa yetu siri,twamtaka bintiye
Ni muungwana jasiri,kajibu tukaribiye
- Baba katoa shuruti,kwa mwanawe kumtowa
Anazitaka yakuti,kilo bila kupunguwa
Apewa nyumba binti,na khati kuandikiwa
Ndipo atapodhibiti,bintiye kuolewa
- Tukapewa wiki mbili,tulete yetu jawabu
Katuvuruga akili,tukabakia mabubu
Kuzipata hizo mali,yataka nyingi sulubu
Hata miaka miwili,sirahisi kwa sahibu
- Nikamwambia mwenzangu,kila jambo linakheri
Limeandikwa na Mungu,Kukuepusha na shari
Hili sio lako fungu,jikaze onesha ari
Najuwa unauchungu,sahau nakushauri
- Tukakifunga kitabu,kwa nyuzi kukishonea
Yalo sibu yamesibu,kule hatukurejea
Ikawa ndio jawabu,baba kumpelekea
Tulihisi ni aibu,kwake tena kumwendea
Barkoa007
|