|
|
BUNGE LOTE LASINZIA!
Date: 12 April, 2008
- Raia wa Tanzania, Bara visiwani pia,
Hivi kweli mnajua, kuwa bunge lasinzia,
Posho wanajichotea, na ‘mishangingi’ sawia,
Bunge lote lasinzia, ndoto ni posho na gari.
- Aibu inatokea, picha zinapotwaliwa,
Wabunge wa Tanzania, bungeni wanasinzia,
Wageni wanadhania, ni utani si sheria,
Bunge lote lasinzia, ndoto ni posho na gari.
- Spika kawaambia, ruksa kujilalia,
Ila amewausia, mkoromo kuto-toa,
Walale kwa kusinzia, na ute kujitolea,
Bunge lote lasinzia, ndoto ni posho na gari.
- Chaguzi imewajia, wa Tanzania raia,
Mbio watawajilia, kura mtawapigia,
Wabunge tawaambia, mema tutawatendea,
Bunge lote lasinzia, ndoto ni posho na gari.
- Muswada ukijilia, kwa kura kupitishia,
Kwa wingi wamezidia, wapinzani wanalia,
Vijembe tawapigia, na kedi tawafanyia,
Bunge lote lasinzia, ndoto ni posho na gari.
- Vema mkijiandaa, kura kuzikazania,
Kuchagua wanofaa, wenye na haki sawia,
Bunge - enda likafaa, miswada kujadilia,
Bunge lote lasinzia, ndoto ni posho na gari.
- Beti nane natulia, nazidi sisitizia,
Haki kuikazania, viongozi kuchagua,
Bungeni wende kukaa, macho-pasi kusinzia,
Bunge lote lasinzia, ndoto ni posho na gari.
Abdalla Sani
|