|
|
HEKO DA SALMA!
Date: 15 April, 2008
- Kadhia hii ni nzito, yenza aibu na ufinyu
Wala si sera ya mpito, ni ya itikadi na mbinu
Wajib kuipangua vito, kwa kuhifadhi chetu kinu!
- Na kuhifadhi chetu kinu, ni kujitwangia maana
Tusiige ya wenye ZANU, yao Zimbabwe kuichana
Hata tufikapo ONU, kwa viongozi kusutana!
- Na viongozi kusutana, ndio kheri ya kwetu sote
Kusimamisha mahakama, pa hayo kuyasema yote
Waungwana hawato zama, kwa kuto ogopa chochote!
- Kwa kuto ogopa chochote, na kufunuwa kwa makini
Uwongo ufichuke kote, majabari wanapo khini
Na ukweli usi kokote, pale wakatapo maini!
- Pale wakatapo maini, ni pa kuvunja wetu moyo
Tusionee masikini, kuvumilia wenye choyo
Tusijitose baharini, kwa kuridhisha Bagamoyo!
- Kwa kuridhisha Bagamoyo, Wapemba waona mazito
Hawatokwenda kamwe Tokyo, na katafuta ya mpito
Kwani wao si mabogoyo, wa kutafuna hivyo vito!
- Salam Bi Salma salamu,
ama kweli wanikosha
Kwa wako mshiko kalamu,
maelezo kuyaanyosha
Na lugha lako timamu,
wajinga kuwapotosha!
- Wajinga kuwapotosha,
ni kutunuwa matende
Twende zetu Kigomasha,
nduzetu tuwapende
Kwa fahari na tamasha,
na sio kwa peremende!
- Na sio kwa peremende,
kwani wao si mikizi
Wa kusuma twende,
ni wa kuzamia mbizi
Kwenye milima na mabonde,
na kuandama mabwizi!
- Na kuandama mabwizi,
ni kusafisha wetu moyo
Kwa vituko vya siku hizi,
kutawalisha wenye choyo
Wa zuwao ukimbizi,
kutuhamisha Bagamoyo!
- Kutuhamisha Bagamoyo,
ni kutufukuza makwetu
Kutufanya watu ovyo,
na kupora mali zetu
Katu tusikubali hayo,
shime vijana wetu!
Salim Himidi
HEKO DA SALMA!
Date: 17 April, 2008
- Shekh Salim mtunzi, nishani ninakutunza
Mwenzetu unaujuzi, hakuna anokuweza
Kijiweni kuna kazi, tutumie mbinu pweza.
Hashil Seif
HEKO DA SALMA!
Date: 17 April, 2008
- Maalim umetamani,
hii nishani kunitunza
Mi si mtu wa thamani,
kwa yote ulonifunza
Elimu ya Makuhani,
ya Janab kukujaza!
- Na Janab kukujuza,
hajajua haya yote
Ndo wivu wa Mke Mwenza,
kuangamiza mila zote
Wazanzibari kutomeza,
haluli ya nduli zote!
- Haluli ya nduli zote,
imetia bawasili
Kuvunja kunga zote,
kwa kupoteza akili
Na watwani si cho chote,
duniani leo hii!
- Duniani leo hii,
kutambua mtu kwao
Adhabu ya Wahshii,
asojua lake jambo
Si wa Dola si wa Ntii,
huko Ndani hata Ngambo!
- Huko Ndani hata Ngambo,
hutambui kipi chetu
Hiyo Mbiu Ya Mgambo,
na hizo haki zetu
Hazina tena majambo,
yako wewe na Sepetu!
Salim Himidi
|