|
|
MATUNDA YA MAPINDUZI!
Date: 16 January, 2008
- Fumbo tena si fumbo, si siri bali dhahiri,
Kikao wenye matumbo, kiliketi Zanzibari,
Kwenye mambo na vijambo, kutangaza ubepari,
CCM ina wenyewe, wengine ni wapagazi.
- Ukitaka Uraisi, karatasi milioni,
Wa kwanza huo ukwasi, pesa zisizo na deni,
Kwa fukara si rahisi, japo uwe na tamani,
CCM ina wenyewe, wengine ni wapagazi.
- Na kisomo siyo shani, uchao wanabadili,
Bado kwenye kampeni, na mchujo wa batili,
Siasa za mumiani, wengine kuwa dhalili,
CCM ina wenyewe, wengine ni wapagazi.
- Ubunge ni laki moja, fomu sasa biashara,
Ni chama chenye vioja, sasa hivi ni mnyura,
Kizee chajikongoja, kimepoteza taswira,
CCM ina wenyewe, wengine ni wapagazi.
- Ni ruba sasa si chama, kimeacha maadili,
Pesa ndio zinasema, imetoweka asili,
Mfumo huu dhuluma, mimi nisingekubali,
CCM ina wenyewe, wengine ni wapagazi.
- Ningekulikuwa Mjumbe, kamwe nisingeafiki,
Chama kimekuwa wembe, kwa mnyonge akishiki,
Unyanyaso kwa viumbe, bila pesa hauvuki,
CCM ina wenyewe, wengine ni wapagazi.
- Japokuwa Udiwani, ulipe elfu kumi,
Wenye kipato cha chini, umeshakuwa unyimi,
Wewe uwekwe pembeni, ijapo uwe msomi,
CCM ina wenyewe, wengine ni wapagazi.
- Milango kwa upinzani, ndio kuliko bakia,
Tuibadili ramani, kikongwe kumfukia,
Tena hatumtamani, sasa kibaki mkia,
CCM ina wenyewe, wengine ni wapagazi.
Abdalla Sani
|