|
|
Akanidanganya
Date: July 1 - 2004
- Akanidanganya, akanambia takuja, hafikwa n'tabu, na mashaka na mauja
Kaniparaganya, nami meishiwa hoja, yaliyonisibu, meona bora kuyaroja
Nataka waonya, haya yangu si kioja, na wewe sahibu, upime na kuyachuja
Yaliyompata Mtoja, yemfika na ..... mmoja. (Kassim Ali)
- Akanighilibu, kumbe yeye ni laghai, na hana ahadi, ni vyema kumuepuka
Mtu wa ajabu, mbaya, tena hafai, na pia fisadi, ni mbovu zake hulka
Aweza jaribu, kuja kukurai rai, akipiga hodi, kwako mlango shindika
Yaliyompata Mtoja, yemfika na ..... mmoja. (Kassim Ali)
- Amenifisidi, nyingi sana zangu mali, sio mtu mwema, tapeli, mdanganyifu
Aliniahidi, kwa hila za kifedhuli, kumbe anichuma, jangili mla nyamafu
Nalizikaidi, nasaha zake ahali, mauja me'kwama, jahili la takilifu
Yalompata Mtoja,yamemfika na? mmoja. (Ahmed Rashid)
- Akanipumbaza, kwa tabasamu na cheko, tegoni hangia, nduyenu hapumbazika
Sasa kajibanza, vimondo tele mbeleko, mwenzenu nalia, mashaka yamenifika
Mepondwa cha pweza, mejaa masikitiko, mwenza angalia, usije kuhadaika
Yalompata Mtoja, yamemfika na? mmoja. (Ahmed Rashid)
- Ya nini mayowe, kuteleza ni kusoma, kakushinda tonge, mshinde kwa matoezi
Hila zitambuwe, usibaki kulalama, usiwe mnyonge, inuka wacha ajizi
Yawahi mwenyewe, sipembejee huruma, hata awe nge, nguruma aone kazi
Yaliyompata Mtoja, yemfika na ......mmoja (Saleh Barkey)
- Yataka vilinge, hila na ujanja mwingi, ndio umshinde, ukipate utakacho
Kaweka mazonge, na vingi sana vigingi, wengi maafande, mezagaa kama kocho
Mefanya vigenge, kampeni na mitingi, ni nini nitende, nimzibe yake macho?
Yaliyompata Mtoja, yemfika na ......mmoja (Kassim Ali)
- Ngoma ivumayo, mwishowe ni kupasuka, miko ni imani, na mipango kuisuka
Kama huna moyo, lijalo wababaika, atakubaini, akuzidishe mashaka
Ni mengi yajayo, sikuye nae tafika, uwe furahani, kiteweji kimteka
Yaliyompata Mtoja, yemfika na ........mmoja (Saleh Barkey)
|