.

Welcome to Zanzinet Swahili Poems

Where Swahili matters!

Kimbia Ugwe!

 

 

 

 

 

 

Related links

Kimbia Ugwe!

KIMBIA UGWE, USIJAONA NG'OMBE ni shairi lililoanzishwa na Sheikh Saleh Barkey na kuchangiwa na watungaji waliotumia ufundi wao wa lugha yenye utajiri wa namna yake usiochosha kuusoma na kurudia mara kwa mara.

Maana ya neno "UGWE" ni kamba kama alivyotuelezea Sk.Kassim Abdulla, ambaye ni mjumbe mwenzetu mashuhuri katika zanzinet na mmojawapo walioshiriki katika ngonjera hii ya kimbia ugwe.Katufahamisha kuwa neno "ugwe" linalotumika katika msemo "kimbia ugwe, usijaona ng'ombe", lina maana ya "kamba" na hii ni hakika kabisa wala hakuna mushkeli wowote. Na maana ya jumla ya msemo ni kumtahadharisha mtu akimbie chanzo cha matata kabla matata yenyewe hayajamfika.Utaona dhahiri kwa maana ya neno "ugwe" iliyokusudiwa katika msemo huu ni "kamba". Maana nyengine ya hili neno "ugwe" abayo ni "uanguke" haioani wala haisadifu na usemi wenyewe kama ilivyofafanuliwa kwenye mjadala. Huwezi kumwambia mtu "kimbia uanguke" na wakati huo huo ukawa unamtahadharisha na pembe za ng'ombe!.

Haya yanatokana na kawaida za kikwetu na namna ya ufugaji, ambapo ng'ombe hufungwa kamba kichakani kwa malisho na inakuwa si rahisi kujuwa kajifichia wapi kwa kuona kamba yenyewe na ndio ukaja huu msemo kuwa uwe na hadhari kubwa kwa kuwa huwezi kufahamu atakutokea wapi, na dawa ya yote bora kimbia ugwe kabla hujaona ng'ombe.

KIMBIYA UGWE USIJAONA NG'OMBE

  1. Yakueleya vizuri, fahali limechachama
    Hakuna cha ujabari, ukweli ukisimama
    Ukijitiya kiburi, pembe zitakuandama
    Akhuyi kimbiya ugwe, singoje kuona ng'ombe
    (Saleh Barkey)
  2. Nakuomba ya akhii, siri uifafanuwe
    Alokusudiwa hii, ya pembe simraruwe
    Leo miye sikwachii, hadi huyu nimjuwe
    Ataye kimbiya ugwe,asije kuona ng'ombe
    (Maher Fundi)
  3. Kimbiya ugwe n'nini, jamani musinikhini
    Nambiyeni hadharani, nami nione ya ndani
    Sina raha asilani, hivi nimo mashakani
    Ng'ombe huyo ni wanani, alokimbiya zizini
    (Juma Salim)
  4. Dudu unalolitaja, hakuna asolijua
    Kutwa limo kubwabwaja, na pia hujihashua
    Harufu chenza kangaja, apitapo lagwavua
    Natuufunge mkaja, ajuwe tumeamua
    (S.Hashil)
  5. Kimbiya ugwe kimbiya, yupo avuma kipole
    Mkinzi utaja liya, kusudi haina pole
    Akhuyi geuza njiya, sitende yale kwa yale
    Kushazuka ruhaniya, ganja na moja kidole
    (Saleh Barkey)
  6. Kimbiya sije jibana, ng'ombe hajuwi salama
    Kimbiya ugwe kijana, ng'ombe atakuandama
    Kimbiya leo si jana, tafuta mahala hama
    Kimbiya sije kuona, hakuwachi takuchoma
    (Salma Khamis)
  7. Jidhatiti barabara, ili usije teleza
    Pembe zake ni imara, tena sana zaumiza
    Uhitajilo tambara, ng'ombe kuweza mcheza
    Mjipange mduwara, mumtiye makengeza
    (Said Suleiman)
  8. Kheri bora kutuliya, nikachemsha akili
    Mti tauparamiya, kuiepuka ajali
    Nikigwa nitaumiya, kwa makwato ya fahali
    Inuka simama dede, upate mcheza ng'ombe
    (Said Suleiman)
  9. Dede tumeshasimama, fahali kuja mcheza
    Hata akija kwa wima, ngao tumeshatengeza
    Tumeshazijuwa njama, pembe tutazikwereza
    Katu haturudi nyuma, kidete tunamwangaza
    (miminae)
  10. Shemere tutamvika, pasi kuwa na khabari
    Na amri kuiitika, pasi na lake shauri
    Kiona tacho mfika, maisha yake takiri
    Pahala pake kafika, pakutolewa jeuri
    (Abdulla Al Harthy)
  11. Ukimpima kichwani, hana ukali pembeni
    Hawamuogopi nyani, wala watoto nyumbani
    Asomjuwa ni nani, ngombe wa aina gani
    Muache aje nyumbani, tumtiye mikononi
    (Abdulla Al Harthy)
  12. Dua ndugu iondowe, ng'ombe kumwita nyumbani
    Ng'ombe humjuwi wewe, ni ng'ombe wa majangwani
    Khuyi sijifaraguwe, huyo hachezewi ndani
    Hadhari uichukuwe, pembeze zina medani.
    (Walii Genderi)
  13. Kiburi si maungwana, tuliza yako akili
    Hodari ungajiona, dume usilikabili
    Ubingwa ja huo huna, wa kumcheza fahali
    Akhuyi kimbiya ugwe, singoje kuona ng'ombe
    (Kassim Abdullah)
  14. Usijifanye shupavu, ya akhi kimbia hima
    Utaanguka kibavu, ng'ombe akikuandama
    Kimbiya kama mwerevu, usisubiri nakama
    Akhuyi kimbiya ugwe, singoje kuona ng'ombe
    (Kassim Abdullah)
  15. Haya yangu usilumbe, kwa hakika nakwambiya
    Ukija kutogwa pembe, ndugu utajijutiya
    Neno hilo usiambe, ya kwamba tamchezeya
    Akhuyi kimbiya ugwe, singoje kuona ng'ombe
    (Kassim Abdullah)
  16. Nikwambiayo wafiki, yafikiri na kupima
    Usende kwenye hilaki, kipigo kitakuuma
    Maji ya goti huvuki, utawezaje ya pima?
    Akhuyi kimbiya ugwe, singoje kuona ng'ombe
    (Kassim Abdullah)
  17. Majuto ni mjukuu, daima huja mwishoni
    Nakupa wasia huu, usikilize akini
    Utaja vunjika guu, wakubwazo kikhaini
    Akhuyi kimbiya ugwe, singoje kuona ng'ombe
    (Kassim Abdullah)
  18. Yakhe usijipe tabu, hili sikio la kufa
    Si rahisi matibabu, ni mithili ya kifafa
    Mwache ujifanye bubu, usimpe maarifa
    Asitafute sababu, kashindwa kuziba ufa
    (Assad Abdullah)
  19. Haya huyo n'nani, anojitiya hodari
    Ng'ombe akamzaini, kumtiya mtegoni
    Kila siku hamkani, watu wako mafichoni
    Akhuyi aweze nini, mwenyewe yu taabani
    (miminae)
  20. Kimbiya wako uwovu, ng'ombe asijekubana
    Kwani huwi muwerevu, na mjinga uso mana
    Ukaondosha uvivu, kuwa naye mbali sana
    Ukanusurika shavu, ng'ombe akaja kuchana
    (miminae)
  21. Ukiambiwa makini, hadhari iwe kichwani
    Ng'ombe bado yu mwituni, hujuwi kichaka gani
    Kambaye iuwanjani, alama uhatarini
    Ujuwe wazi huponi, akikutiya mbaroni
    (miminae)
  22. Mbinu zenu zimeshindwa, fahali kumchezeya
    Sio yule wa kupandwa, sanamu lilo bandiya
    Ni mwingi aliyefundwa, ghafula hukutokeya
    Kikushika utapondwa, huna utapobakiya
    (miminae)
  23. Siyo kwamba ni hodari, mwenye nzito asili
    Bali nina ujasiri, wa shida kuikabili
    Kinachonitiya ari, na kule kutokubali
    Ni kupewa tahadhari, ya dudu liso akili
    (Said Suleiman)
  24. Kwangu ng'ombe atadunda, kwani mimi ni mchunga
    Pembe zake zitapinda, najiamini kwa chenga
    Mwishowe nitampanda, hali huku ninaringa
    Nitalifanyia inda, likome kutanga tanga
    (Said Suleiman)
  25. Hata angekuwa ndama, usingeweza mpanda
    Seuze ng'ombe mzima, mwenye nguvu za kuwanda
    Atakunyanyuwa wima, kikutupa uwe sanda
    Bila hata ya huruma, na mengi atakutenda
    (Maher Fundi)
  26. Pokea wangu wasiya, uepukane idhara
    Usikae kungojeya, dunia kukuburura
    Mambo umejioneya, mebadili yake sura
    Walopewa ruhaniya, tano na moya vitara
    (Maher Fundi)
  27. Gombe lifanyie shime, uchunga wake mpevu
    Hilo na tuliandame, hadi litoke mapovu
    Baadaye umpime, kama yeye ni mwerevu
    Halafu umtazame, kumbe si mkakamavu
    (S.Hashil)
  28. Mimi nimeligundua, kwamba halina halani
    Watu kimsujudia, ni hapo kale zamani
    Leo wanalizomea, na kulita punguwani
    Wallahi linaridhia, lajuwa li taabani
    (Said Suleiman)
  29. Macho yake kufumbua, ni nadra ubaini
    Pembe zake tazivua, bila hata ubishani
    Tambara kimtupia, yeye aona majani
    Sasa leo wanambia, tabishana kwa ruhani?
    (Said Suleiman)
  30. Usemayo si utani, limebaki hamkani
    Lajifanya kama nyani, lachupa kutwa mitini
    Haaminiki yakini, buluu kwake kijani
    Siruhani si shetani, ni joka kwenye majani
    (S.Hashil)
  31. Asemayo si muhimu, asijifiche chakani
    Aangaliwe kwa zamu, asitoweke kizani
    Sote tunamfahamu, kiumbe wa kizamani
    Apenda kumwaga sumu, jengine yeye haoni
    (S.Hashil)
  32. Alaa kumbe hukomi, wajifanya mjuaji
    Usijeleta magumi, na kutafuta majaji
    Na majeshi kukuhami, usipate kufa maji
    Ng'ombe aja hasimami, haraka kimbiya mji
    (Assad Abdullah)
  33. Simtetei akhui, uwazi mbele machoni
    Anadhani hatujui, mwana khaini nchini
    Kaona hatutambui,wake wizi lo'zaini
    sasa nakimbiye ugwe, asije kuona ng'ombe
    (miminae)
  34. Huyo tushambaini, hana lake la makini
    Twembeba mgongoni, akenda kutukhaini
    Leo yuwatutamani, ela kambini hafani
    Mungu keshambaini, sasa hayuko nyoyoni
    (Abdulla Al Harthy)
  35. Ya ng'ombe si fani yao, idhara waitafuta
    Ugwe ishingoni pao, kama kisu yakeketa
    Ng'ombe meirusha kwao, na sasa yawafuata
    Akhuyi utaja toka, mtini si ngao shuka
    (Salma Khamis)
  36. Inawatafuta mwao, mule walimojificha
    Wawe na nyundo na ngao, salama wakizificha
    Kitoa shauri yao, bora mapema ku'm'cha
    Akhuyi utaja toka, mtini si ngao shuka
    (Salma Khamis)
  37. Muwapi mlojikumba, kujiweka viamboni
    Kuwa mnakuja komba, vilivyo vyetu vya ndani
    Mkashindwa kuviwamba, mkabaki mabondeni
    Ng'ombe akawa ni simba, ugwe akakufungeni
    (Maher Fundi)
  38. Kwa vipazo mkitamba, bila watu viwanjani
    Matokeo tumesomba, ngome iko mikononi
    Sisemi tunajigamba, ukweli umebaini
    Ng'ombe alofungwa kamba, ndiye kakumalizeni
    (Maher Fundi)
  39. Mkamiya hanywi mayi, funda moja hachubui
    Muache aliye ngoyi, Mshazume habagui
    Jecha Shumba hakugwiyi, sambe arambaye tui
    Hata ugwe agwegwenye, kuukata hatambui
    Ahmed Rashid)
  40. Kuukata hatambui, hata ugwe agwegwenye
    Kaja na kituitui, hata wajane anyonye
    Kumbe kipole hajui, yuko wima kinyekinye
    Hadaa kafanye huko, Ole wamekubaini
    (Ahmed Rashid)
  41. Ole wamekubaini, hadaa fanyeni huko
    Kimbiya ugwe fulani, kijiwe hiki si chako
    Ndugu wakiwa vitani, enenda kondeni kwako
    Halahala ncha hino, hoho tatoja matoni
    (Ahmed Rashid)
  42. Hoho tatoja matoni, halahala ncha hino
    Umeshindwa umetani, wagaagaa kipono
    Waropoka mitaani, kwa goli la kisigino
    Haja matao ngomani, ugenini jalalani
    (Ahmed Rashid)
  43. Mtenda mwenye ujuzi, hababaishwi na tao
    Ila awe mwanafunzi, wakujipachika cheo
    Akipita pande hizi, sikiza chake kilio
    Hawahi vuta pumzi, watu wajilia vyao
    (Said Suleiman)
  44. Sitishike asilani, kwa shani yake ya jana
    Muangaze kwa makini, pakukupiku hakuna
    Kesha tokeya zamani, sasa atumiya jina
    Hako wakumuauni, Aanza kwanga mchana
    (Said Suleiman)
  45. Sikiza wangu azizi, ujuwe hii hakika
    Shina meacha mizizi, na chini limeshang'oka
    Gogo latoa vibanzi, majani yanakauka
    Nzige mefanya kazi, mbuyu unaanguka
    (Maher Fundi)
  46. Safari ya kwenda mbali, mwanzowe hatua moja
    Waufahamu ukweli, sifasiri sina haja
    Tulipo hatuko mbali, yanjiani yanakuja
    Tumepaniya kikweli, twaisubiri faraja
    (Maher Fundi)
  47. Sitouka abadani, kwa kelele za mlango
    Nishaliona zamani, kama halina mpango
    Unamuogopa nini, ng'ombe alo na mapengo?
    Yake macho hayaoni, sikwambii hilo bongo
    (Said suleiman)
  48. Mapengo ni yake shani, hayo katu hatumii
    Zilokuwepo kitwani, akhui huzizuii
    Amepewa na Manani, hata humjuilii
    Ndugu ngiya safarini, mbinde hazisaidii
    (Walii Genderi)
  49. Mlango haukuwepo, usifanye ukaidi
    Ujuwe na Mungu yupo, akhuyi sinikejeli
    Kimbiya urudi papo, utizame yalofeli
    Bora wewe hukuwepo, ng'ombe alipo vinjari
    (Walii Genderi)
  50. Yaeleweka zamani, mpanda ngazi hushuka
    Ila hili hayawani, naona laporomoka
    Limechoka taabani, popote lajipweteka
    Limeishiwa na fani, kazi linababaika
    (Saidi Suleiman)
  51. Kwake kwenda malishoni, nako pia ni mashaka
    Mana macho hayaoni, nuru imeshamtoka
    Anategemeya nini, upupu au ukoka?
    Hao wakumuamini, kijasho kimewatoka
    (Said Suleiman)
  52. Ni mkubwa mtihani, yakupasa ubaini
    Nakuona taabani, wajikaza kisabuni
    Ya ng'ombe kubwaga zani,kutiya hofu mjini
    Kimbiya sio utani, asikutiye machoni
    (Assad Abdullah)
  53. Yaliwashinda malenga, tena malenga wa kweli
    Ikawa watangatanga, wahaha kila mahali
    Wakiitafuta kinga, ya vishindo vya fahali
    Ng'ombe kwake akitinga, nani wakumkabili
    (Assad Abdullah)
  54. Yalielezwa zamani, na wajuzi wa maana
    Kwamba haiwezekani, kuichezeya amana
    Si muhali asilani, ukipokonywa dhamana
    Katu ng'ombe si haini, wala hafanyi hiyana
    (Assad Abdullah)
  55. Mshari ni kama nani, kugombanisha wendani
    Wenziwe hawathamini, leo wamembaini
    Tutamchukuwa pwani, tukamchovye majini
    Tufanye yetu dhamiri, katu harudi nchini
    (Abdulla Al Harthy)
  56. Yasemwayo kumbe kweli, ng'ombe kang'olewa pembe
    Kaziye fanya ajali, mkali kuliko wembe
    Kadhoofu yake hali, na suraye ya uzembe
    Kuona kwake si mbali, hajiwezi hata chembe
    (S.Hashil)
  57. Sikwamba ni ushabiki, ng'ombe kumjaza sifa
    Mikubwa yake mikiki, kikupata ni maafa
    Na nguvu zake lukuki, mwenye mbio kama zefa
    Akhuyi nyuma sibaki, sipuuze utakufa
    (Assad Abdallah)
  58. Situone twakughasi, yote haya ni mahaba
    Mana wewe kwetu sisi, unapendeka si haba
    Wala baya usihisi, sisi nduguzo kwa baba
    Kwa hiyo ukituasi, mateso utayabeba
    (Assad Abdallah)
  59. Woga umekuzidiya, Shuruti unatetema
    Amini ninokwambiya, kweli alikuwa chuma
    Zama zimempitiya, hawezi tena kuchoma
    Madhali ana bidaya, na nihaya ni lazima
    (Said Suleiman)
  60. Walojifanya vidume, wangapi wameshaenda
    Wakajifanya mitume, watakalo wakatenda
    Akina Mkamandume, pia na Jabu Mponda
    Basi na lilo likome, lishapata ndugu donda
    (Said Suleiman)
  61. Khuyi huu ni usiya, upate yako salama
    Kama hutaki sikiya, ungali wajitutuma
    Atakuja kuvamiya, ushindwe na la kusema
    Akhuyi kimbiya ugwe, singoje kuona ng'ombe
    (Saleh Barkey)
  62. Usijitiye umbeya, ujionee huruma
    Khatari kuichezeya, huo si mchezo mwema
    Vipi utajiteteya, dume likija kufuma
    Akhuyi kimbiya ugwe, singoje kuona ng'ombe
    (Saleh Barkey)
  63. Tafuta umtakaye, umchukuwe pembeni
    Huyu niachiye miye, nikamfunge mtini
    Usiwe na kazi naye, humuwezi ni wa nini?
    Asishughulishe kamwe, ng'ombe huyu wa utani
    (Abdulla Al Harthy)
  64. Amtaka ulonaye, amtiye mikononi
    Mikononi awe naye, amdhibiti ugweni
    Ugweni chini akaye, amjuwe yeye nani
    Nani yeye ajuaye, asiye penda undani
    (S.Hashil)
  65. Huyu sitampa mtu, Mtashindwa ishi naye
    Ana wake utukutu, nao naujuwa miye
    Alinikhasimu kwetu, kuwa sisemi na yeye
    Ng'ombe huyu wa mzimu, ni wangu si wenu nyiye
    (Abdulla Al Harthy)
  66. Akhuyi sifanye manza, kuzidi kumkebehi
    Ng'ombe alifungwa kwanza, ndio mbio ukawahi
    Ugwe wake umetanza, nakuwapia Wallahi
    Lau angekusabahi, ungeangukia Mwanza
    (Walii Genderi)
  67. Sauti mnazotoa, ng'ombe hamjamfika
    Ya bure mnatongoa, au woga mewashika
    Parakacha akitoa, mbona mnatawanyika?
    Akhuyi huyo si nyoka, sifanye kumchokoa
    (Walii Genderi)
  68. Zama ulipoambiwa, kiona ugwe kimbiya
    Akhuyi hukutakiwa, hoja kutuhubiriya
    Shauri kila kipewa, waja na jawabu miya
    Lipi utaja twambiya, ng'ombe akikuraruwa
    (Walii Genderi)
  69. Nyingi hamrere zako, bado hujaona ng'ombe
    Majigambo ndiyo yako, huku waogopa pembe
    Umewafata wenzako, kumpiga kwa vijembe
    Ugwe maneno ni hako, je kiona mwepembe
    (Walii Genderi)
  70. Takupa kisa cha kweli, Pemba kilichotukiya
    Cha yule aliyesali, karibu sana na njiya
    Akatishwa kweli kweli, sala kamtengukiya
    Basi nawe zingatia, tumia yako akili
    (Dr.Hassan)
  71. Kaambiwa anosali, hasemi anasikiya
    Kipole ng'ombe mkali, keshakata atujiya
    Endelea na kusali, ela miye nakimbiya
    Khushui ikapotea, kwa bwana mwenye kusali
    (Dr.Hassan)
  72. Kimbia mwana kimbia, kimbia sirudi nyuma
    Kimbia mbali kimbia, kimbia sione nyuma
    Kimbia kule kimbia, kivumbi uwache nyuma
    Nyuma huko ndio nyuma, siyatafute kimbia
    (Walii Genderi)
  73. Habari ulisikia, za bwana mwenye kusali
    Yaache kuyarukia, ya ng'ombe yana kejeli
    Wengi alowazukia, wamekufa chalichali
    Huyo kweli ni mkali, dume lilopindukia
    (Walii Genderi)
  74. Watupie wenye ngeli, wanotamani mauti
    Wamcheze kwelikweli, japo kafungwa na mti
    Wakiiona batili, weshakuwa mahututi
    Shujaa wa atiati, imedumbwa yake hali
    (Walii Genderi)
  75. Mja unayo khiyari, kwambwa ukaambilika
    Au kudhani hodari, ukakumbwa na mashaka
    Kushapewa indhari, geuza njia haraka
    Akhuyi kimbiya ugwe, singoje kuona ng'ombe
    (Dr.Hassan)
  76. Tamati natamatiza, sina tena niendako
    Yangu usijeyabeza, nakuasa ndugu yako
    Ugwe ukiuangaza, usijipeleke huko
    Akhuyi kimbiya ugwe, singoje kuona ng'ombe
    (Dr.Hassan)
  About Us | Zanzinet Home | Contact Us | ©2004 Zanzinet