.

Welcome to Zanzinet Swahili Poems

Where Swahili matters!

Kiwera

 

 

 

 

 

Related links

 

Kiwera!

Date: Jan - Feb 19, 2003

Assalam aleykum

Wapenzi wa mashairi na wanaukumbi kwa jumla

Baada ya kukamilika shairi la Kiwera,leo ninafuraha kukuleteeni shairi kamili la beti 81 pamoja na utangulizi wa Professor Ibrahim Noor Shariff na majina ya watungaji wote wa shairi hili.

UTANGULIZI

Watunzi waliotunza tungo za watungaji wetu wa kale wameturithisha idadi nzuri ya tungo za zamani ambazo zinatupa taswira ya maana inayotuwezesha kuona ujuzi waliokuwa nao watungaji waliotutangulia. Kuna tungo za mvyele wetu aitwaye Fumo Liyongo ambaye, inasemekana aliishi zaidi ya miaka elfu iliyopita, na kuna tungo za wengi walioishi baada yake. Kuna tungo zenye maudhui mbalimbali - tungo za kidunia na za kidini, za kufanyiana mizaha na za kutiana vishindo vya kivita; kuna na za kusifu na za kuumbua; kwa ufupi, kuna tungo za maudhui mbalimbali zilizotungwa na Waswahili. Ninadhani kuwa hakuna watu wowote katika Afrika ya Kati, ya Mashariki na ya Kusini ambao wana utajiri wa aina hii katika fasihi yao.

Katika aina kwa aina za maudhui ya tungo zilizotungwa kwa bahari mbalimbali; bahari zisizopungua kumi na tatu - utenzi, wimbo, shairi, tumbuizo, wawe, kimai, Dura Mandhuma, Inkishafi na kadhalika - hakuna aina inayopendwa na Waswahili wengi kama tungo za kujibizana. Tungo za kujibizana si za bahari maalumu wala maudhui maalumu. Huweza kutungiwa kwa bahari ya wimbo, shairi, utenzi na kadhalika. Pemba, kwa mfano, kuna ngoma ya kibati (mdebe au cherewa) ambayo watu huimbana papo kawa papo bila ya matatizo. Ule uhodari wa kujibizana papo kwa papo na, aghlabu kwa maneno ya kutaniana, watu wakafurahi na kucheka, kumewapa wachezao ngoma hiyo sifa kubwa kwa wenye kupenda tungo za aina hiyo. Halikadhalika, katika mji wa Amu (Lamu) kwenye hafla za harusi upande wa wanawake, kulikuwa na tumbi ya mama zetu waliokuwa wakiimbana usiku kucha kwa nyimbo za kupigiwa mfano walizozitunga hapohapo ngomani, ndipo wakale wetu wakaturithisha msemo unenao: "wimbo hutoka ngomani."

Uswahilini kote kulikuwa na wazee wetu ambao walikuwa wakitungiana mashairi na kujibizana papo kwa papo, au kwa barua na katika miaka ya karibuni, katika magazeti pia; na hii leo mila na utamaduni huo unaendelezwa katika ZANZINET. Mola Karimu Rahimu awape kila la kheri na baraka waliouanzisha mtandao huu ambao lengo lake ni la kheri; lengo la kuwaunganisha Wazanzibari popote pale walipo.

Katika zanzinet kuna wajuzi wa fakhari katika kutunga na kujibizana kwa tungo zenye uzito wa thamani kubwa. Nilitaka kutoa mifano ya uhodari wa kutunga unaoonekana humu katika chombo hichi cha fakhari cha zanzinet, lakini nikaona kuwa watungaji ni wengi na tungo za fakhari ni nyingi na mwenye kusoma na kuelewa hahitajii kutolewa mifano ya udohoudoho. Mwenyewe huwa anasoma na kustaladha kila akutanapo na haluwa za lozi za aina hizo ambazo huandaliwa kila mara.

Leo tunakuleteeni, kwa ukamilifu, mashairi ya kujibizana yenye maudhui ya KIWERA ambayo yametungwa na idadi ya wanazanzineti. Tunatumai utastaladha na utamu uliomo katika tungo hizi.

Ili kuzidi kuonea raha yaliyozungumzwa, inataka uelewe maana ya "kiwera" ; na si maana ya "kiwera " tu, bali makusudio yaliyokusudiwa; kwani neno "kiwera" katika mashairi haya haina maana ya humbo au neema ya wingi wa dagaa au samaki. "Kiwera" ni "neema" ya aina nyengine kabisa iliyowafikia watu wa nchi ya jirani. Sasa nakuachilia msomaji unaposoma utose katika ubongo wako makusudio yaliyokusudiwa ili ustafidi na kuyaonea raha mashairi haya kama wanavyoingiwa na shauku wenye kupenda mafumbo na fani ya kujibizana kwa tungo. Soma ukishasha...

Ibrahim Noor

 

Kiwera!

  1. Twaanza Bismillahi, utungo kuucharaza
    Beti hizi ni nasahi, kwa kila mwenye kuwaza
    Kuna jambo tuliwahi, si jambo la kupuuza
    Kumeingiya kiwera, shime yapatilizeni
    (Saleh Barkey)
  2. Mvuvi kashuka pwani, kwenye usiku wa kiza
    Karabai mkononi, na nyavu kaning'iniza
    Samaki wingi wa shani, wezuka kwa kushangaza
    Kumeingiya kiwera, shime yapatilizeni
    (Saleh Barkey)
  3. Hakuweza kuamini, kadhani ni miujiza
    Samaki wa mkondoni, bandarini kutokeza
    Leo kumezidi nini, au apaazwa pweza
    Kumeingiya kiwera, shime yapatilizeni
    (Kassim)
  4. Katoa chombo nangani, akaanza kucheleza
    Nyavu zake za thamani, kataka zitandiliza
    Na mishipi kibindoni, ikibidi kurambaza
    Kumeingiya kiwera, shime yapatilizeni
    (Kassim)
  5. Samaki walioshuka, walishitushwa na kiza
    Ndipo walipoibuka, juu mwanga kufatiza
    Chini walihangaika, kiza kiliwapoteza
    Kumeingiya kiwera, shime yapatilizeni
    (Maher-Unique)
  6. Hata zilizotoboka, nyavuni waliingiya
    Walolala meamka, mikondoni mekimbiya
    Nyavu zikawa mkeka, kiziona walaliya
    Kumeingiya kiwera, shime yapatilizeni
    (Maher-Unique)
  7. Mishipi ikawa kamba, wakiona wapandiya
    Ndoana wakiziramba, bila chambo kuzitiya
    Madema yakawa nyumba, vururu wakiingiya
    Kumeingiya kiwera, shime yapatilizeni
    (Maher-Unique)
  8. Shime yapatilizeni, wakati umewadiya
    Juhudi tuongezeni, uzio na juya piya
    Leo ni leo jamani, mavuvi kumaliziya
    Kumeingiya kiwera, shime yapatilizeni
    (Mbarouk Mnyonge wa Nyali)
  9. Yapatilizeni shime, kiwera kimechagiza
    Inukeni mukachume, mukumbe mukijaliza
    Muwe wavuvi vidume, damu musije ilaza
    Kumeingiya kiwera, shime yapatilizeni
    (Saleh Barkey)
  10. Munamuona mwenzenu, wa heko kumpongeza
    Kuibaini fununu, hakunena ngoja kwanza
    Werevu na kila mbinu, mvuvi vyombo kajaza
    Kumeingiya kiwera, shime yapatilizeni
    (Saleh Barkey)
  11. Kiwera kilichongiya, hakitadumu milele
    Haitakuwa sawiya, jambo hilo mlijule
    Kesho tukiamkiya, kiwera si kilekile
    Kumeingiya kiwera, shime yapatilizeni
    (Mbarouk Mnyonge wa Nyali)
  12. Aweza vuma wa kusi, vyombo kuvitetemesha
    Ikawa ni wasi wasi, roho zetu kuzirusha
    Ikaingia nuhusi, wavuvi kuwazamisha
    Kumeingiya kiwera, shime yapatilizeni
    (Mbarouk Mnyonge wa Nyali)
  13. Kake mnyonge wa Nyali, usemayo yaneleya
    Kiwera hiki kikali, mtu asije teleya
    Ingawa bado thakili, ya Kisumu kuja Mbeya
    Kumeingiya kiwera, shime yapatilizeni
    (Ahmed Rashid)
  14. Kimeingia chavuma, kiwera mbele na nyuma
    Kaskazi kisimama, kusi si hasha kuzima
    Ikawa kushika tama, leo mbona yamekoma?
    Kumeingiya kiwera, shime yapatilizeni
    (Ahmed Rashid)
  15. Wapo washatuambiya, mwaota mwajipumbaza
    Kiwera mwashangiriya, wala hamutakiweza
    Hachinjwi ng'ombe mkiya, mafumbo watufumbiza
    Kumeingiya kiwera, shime yapatilizeni
    (Saleh Barkey)
  16. Wasoona ya duniya, kwa kiyoo kuwacheza
    Wakawa wang'ang'aniya, kiwera hiki kubeza
    Wajuwe tushanuwiya, mambo yatawashangaza
    Kumeingiya kiwera, shime yapatilizeni
    (Saleh Barkey)
  17. Mambo yatawashangaza, wajue tushanuwiya
    Pamoja tutawekeza, jamii yote sawiya
    Tushauona mwangaza, nyuma mwiko kurudiya
    Kumeingiya kiwera, shime yapatilizeni
    (Mbarouk Mnyonge wa Nyali)
  18. Wenye tamaa kukata, kwa nini wajiumbuwa
    Kiwera kilichokita, ni haki kukinyakuwa
    Na wale wanaoteta, macho yao kufunguwa
    Kumeingiya kiwera, shime yapatilizeni
    (Mbarouk Mnyonge wa Nyali)
  19. Hata uvume upepo, wa kaskazi na kusi
    Ama kwa hapa tulipo, chombo chetu hatukisi
    Kiwera chetu kipapo, nasi twaongeza kasi
    Kumeingiya kiwera, shime yapatilizeni
    (Mbarouk Mnyonge wa Nyali)
  20. Watu walidhani ndoto, kiwera kilipozuka
    Walidhania ni moto, wakaratasi mewaka
    Kuripuka si kokoto, hata chuma meyayuka
    Kumeingiya kiwera, shime yapatilizeni
    (Maher-Unique)
  21. Na sasa hauzimiki, unawaka baharini
    Vilo juu vyaghariki, Jivu halipatikani
    Mkali haushikiki, unaelea majini
    Kumeingiya kiwera, shime yapatilizeni
    (Maher-Unique)
  22. Nauona waripuka, bahari yote yawaka
    Wavuvi mechangamka, wanavua wakitweka
    Maji chini yachemka, samaki wahangaika
    Kumeingiya kiwera, shime yapatilizeni
    (Mhhhhh-Miminae)
  23. Shime jamani shimeni, kiwera ki-uwanjani
    Shime tujikusanyeni, tuingieni chomboni
    Samaki tuwavueni, tufaidike jamani
    Kumeingiya kiwera, shime yapatilizeni
    (mhhhhh-miminae)
  24. Kwa kiwera kilomaki, hakitaki makelele
    Na aliyemo hatoki, asiye takaa kule
    Mwenye macho hapingiki, chomboni tajaa tele
    Kumeingiya kiwera, shime yapatilizeni
    (Mbarouk Mnyonge wa Nyali)
  25. Kama tumeshatongowa, ya muhimu kwa kiwera
    Ni kipi kukizongowa, cha mazonge udodora?
    Wasije kuzikongowa, nyavu mashua za mbura
    Kumeingiya kiwera, shime yapatilizeni
    (Ahmed Rashid)
  26. Wavuvi wafanye nini, nawauliza wahenga
    Na wavyele watendeni, nawadadisi wakunga
    Samaki wako jikoni, na shume limetuzonga
    Kumeingiya kiwera, shime yapatilizeni
    (Ahmed Rashid)
  27. Wana wa kwetu imani, tuime tushikaneni
    Ya kiwera si mageni, yashatokea nyumbani
    Tushike sisi mpini, makali kwao usoni
    Kumeingiya kiwera, shime yapatilizeni
    (Maher-Unique)
  28. Yashatokea nyumbani, ya kiwera si mageni
    Ndio hasema watani, mavuvi yamalizeni
    Watumbatu na Kusini, Jadida na Mtemani
    Kumeingiya kiwera, shime yapatilizeni
    (Mbarouk Mnyonge wa Nyali)
  29. Kwani twasubiri nini, na kiwera kingalipo
    Vyombo tweunda zamani, vyetu sio vya mkopo
    Tuvishushe baharini, tuvitegeshe upepo
    Kumeingiya kiwera, shime yapatilizeni
    (Mbarouk Mnyonge wa Nyali)
  30. Ikiwa ni manahodha, wamejaa washupavu
    Tena wasio bughudha, wenye macho maangavu
    Wasafi hawana adha, sifa yao ni werevu
    Kumeingiya kiwera, Shime yapatilizeni
    (Mabrouk Mnyonge wa Nyali)
  31. Yaliyopita si ndwele, sasa tugange yajayo
    Wembe uwe ule ule, tusivunjikeni moyo
    Kiwera kilicho mbele, kisivuuke machweyo
    Kumeingiya kiwera, shime yapatilizeni
    (Kassim)
  32. Wavyele tuwasomeshe, wasijefanya zohali
    Wavuvi tuhamasishe, wa karibu na wa mbali
    Tusilale na tukeshe, kiwera tukikabili
    Kumeingiya kiwera, shime yapatilizeni
    (Kassim)
  33. Si moja linofumbika, hapalaliki nangani
    Mawimbi yateremka, mbao zinadata chini
    Mashariki zafyatuka, nasi tumumo chomboni
    Kumeingiya kiwera, shime yapatilizeni
    (Maher-Unique)
  34. Nahodha tuchangamke, tueleke bandarini
    Hapa tusiteremke, tutazama mkondoni
    Uwache utupeleke, hadi tufike gatini
    Kumeingiya kiwera, shime yapatilizeni
    (Maher-Unique)
  35. Kwa mwenye kutabaruku, matumaini haachi
    Mola ataturuzuku, tushinde kiwera hichi
    Takapokucha usiku, furaha mejaa nchi
    Kumeingiya kiwera, shime yapatilizeni
    (Kassim)
  36. Jahazi meshika kasi, na tanga lapeperuka
    Chombo hata hakikisi, mpingo waserembuka
    Kuvua jama rahisi, kazi kupata nafaka
    Kumeingiya kiwera, shime yapatilizeni
    (Ahmed Rashid)
  37. Kiwera meshika kasi, wavuvi wa Mgongele
    Wavuvi wavua ngisi, pweza,changu kwa makole
    Wavuvi sisi kwa sisi, ni wa Chaani na Kwale
    Kumeingiya kiwera, shime yapatilizeni
    (Ahmed Rashid)
  38. Kumeingia kiwera, yapatilizeni shime
    Tuiondoe sitara, tuyasafishe mahame
    Tusije kutekwa nyara, samaki wasituhame
    Kumeingiya kiwera, shime yapatilizeni
    (Ahmed Rashid)
  39. Kazi kupata nafaka, samaki tushawavuwa
    Eshiriki dada,kaka, chombo hawakuchaguwa
    Efanya nini Mahoka, jamii inatambuwa
    Kumeingiya kiwera, shime yapatilizeni
    (Ahmed Rashid)
  40. Kwa hapa tulipofika, ndio tumesharidhiya?
    Majahazi kuyatweka, kiwera kuyajaziya
    Kwa miye sijatosheka, bado hayajaningiya
    Kumeingiya kiwera, shime yapatilizeni
    (Mbarouk Mnyonge wa Nyali)
  41. Kiwera kimaridadi, kwa nguvu chashadidiya
    Chataka tujitahidi, mavuvi kumaliziya
    Na aliye mkaidi, si hasha haoni njiya
    Kumeingiya kiwera, shime yapatilizeni
    (Mbarouk Mnyonge wa Nyali)
  42. Yataka tujitahidi, mavuvi kumaliziya
    Tuvue kwa ustadi, isiwe kwa kutupiya
    Nnawapeni ahadi, nanga mwishowe tatiya
    Kumeingiya kiwera, shime yapatilizeni
    (Mbarouk Mnyonge wa Nyali)
  43. Patu na mabaragumu, zipigwe kwa kuchagiza
    Huko Mrima zihimu, zipukutike ajiza
    Wauke wenye naumu, kwa mavuvi kutangaza
    Kumeingiya kiwera, shime yapatilizeni
    (Saleh Barkey)
  44. Wajuwe utamu wake, wajute kujilemaza
    Kila mtu zana yake, mavuvi kufululiza
    Katu tusiweweseke, kazi tutaitimiza
    Kumeingiya kiwera, shime yapatilizeni
    (Saleh Barkey)
  45. Tumekutupa makwetu, tumewaacha wageni
    Kiwera sasa mtutu, tujenge wetu watani
    Tusirudi nyuma katu, tuelekee fukweni
    Kumeingiya kiwera, shime yapatilizeni
    (mhhhhh-miminae)
  46. Tusiruhusu wageni, kuingia kiwerani
    Wageni wana kunguni, walojaa tendeguni
    Siwaoni na huweni, kunyonya damu mwilini
    Kumeingiya kiwera, shime yapatilizeni
    (Ahmed Rashid)
  47. Wengi walichangamka, kiwera kilipongiya
    Haba walojipweteka, kuendekeza uviya
    Mavuvi kimalizika, sote tutafurahiya
    Kumeingiya kiwera, shime yapatilizeni
    (Mbarouk Mnyonge wa Nyali)
  48. Vyombo tukishavijaza, bandarini kuingiya
    Hata wachokoa pweza, nao watashangiriya
    Neema tasheheneza, ipate yote jamiya
    Kumeingiya kiwera, shime yapatilizeni
    (Mbarouk Mnyonge wa Nyali)
  49. Nyota njema ikitoka, mweye macho aiona
    Na yule asiyetaka, la kumfanya hakuna
    Kiwera kikamilika, naapa tutagawana
    Kumeingiya kiwera, shime yapatilizeni
    (Mbarouk Mnyonge wa Nyali)
  50. Pamoja tutagawana, kiwerani tulongiya
    Siyo kwa kubaguwana, ni nyeupe zetu niya
    Qasama bila sonona, tupate sote sawiya
    Kumeingiya kiwera, shime yapatilizeni
    (Mbarouk Mnyonge wa Nyali)
  51. Na tukivue kwa ari, nguvu moja insiya
    Hakuna la kusubiri, wakati watukimbiya
    Huu wetu utajiri, tusiache ukaviya
    Kumeingiya kiwera, shime yapatilizeni
    (Mbarouk Mnyonge wa Nyali)
  52. Walo juu ufukweni, kiwera kiangaliya
    Tukawahamasisheni, kwa makundi kuingiya
    Tusiwawache jamani, tuwaonyesheni njiya
    Kumeingiya kiwera, shime yapatilizeni
    (Mbarouk Mnyonge wa Nyali)
  53. Angenda juu kipungu, hafikilii mbinguni
    Ama kwa Mwenyezi Mungu, kubwa hakuna yakini
    Tutapata letu fungu, Inshallah kwa karibuni
    Kumeingiya kiwera, shime yapatilizeni
    (Mbarouk Mnyonge wa Nyali)
  54. Wale wanaotucheka, huku wakishangiriya
    Iko siku itafika, akili zitawangiya
    Kiwera tukikiweka, ndani ya zetu siniya
    Kumeingiya kiwera, shime yapatilizeni
    (Mbarouk Mnyonge wa Nyali)
  55. Wacheka nnawaomba, jambo moja kulijuwa
    Kwa wetu Mola Muumba, hakuna lisilokuwa
    Takwenda nao sambamba, kwenye jua au mvuwa
    Kumeingiya kiwera, shime yapatilizeni
    (Mbarouk Mnyonge wa Nyali)
  56. Nimepata mnong'ono, nataka wasimuliya
    Ya wale samaki mbono, tunaowakimbiliya
    Ati akina Machano, wapanga kutuibiya
    Kumeingiya kiwera, shime yapatilizeni
    (Kassim)
  57. Wapanga kuzorotesha, kukifisidi kiwera
    Wameanza tisha tisha, kule upande wa bara
    Lazima kuwakomesha, wasitutie hasara
    Kumeingiya kiwera, shime yapatilizeni
    (Kassim)
  58. Samaki wengi wa shani, umma umejivuliya
    Kutoka mwambao pwani, maziwani nako piya
    Wenzangu tahadharini, wakioza tutaliya
    Kumeingiya kiwera, shime yapatilizeni
    (Ibrahim Noor)
  59. Kazi pevu i-jikoni, kwa jifya wanapikiya
    Jiwe moja hulioni, mawili yamesaliya
    Imani hima jamani, tuondoshe mabakiya
    Kumeingiya kiwera, shime yapatilizeni
    (Ibrahim Noor)
  60. Matoke hayapikiki, sima watuvurugiya
    Na mwiko hauzunguki, ziko kombo sufuriya
    Nazo kuni haziwaki, mbichi tukiangaliya
    Kumeingiya kiwera, shime yapatilizeni
    (Ibrahim Noor)
  61. Tengeni yalobakiya, tutumie seridani
    Na wapishi nao piya, hali zao taabani
    Umuri walofikiya, ni mkorogo mekoni
    Kumeingiya kiwera, Shime yapatilizeni
    (Ibrahim Noor)
  62. Korojo sufuriyani, mapishi yasiyolika
    Twaumiya matumboni, nyongo tunazitapika
    Takaudi tuwapeni, wapishi kupumzika
    Kumeingiya kiwera, shime yapatilizeni
    (Ibrahim Noor)
  63. Samaki wako jikoni, meko mawili mabovu
    Wachuuzi wa makini, wapishi wengi wachovu
    Sukuma wiki mezani, ugali u nyovunyovu
    Kumeingiya kiwera, shime yapatilizeni
    (Ahmed Rashid)
  64. Ugali u nyovunyovu, matoke ya hatarini
    Tutaondoa maovu, ja fahali Kisauni
    Nyangumi wabaki fuvu, wakapotee jaani
    Kumeingiya kiwera, shime yapatilizeni
    (Ahmed Rashid)
  65. Vyungu wameviunguza, hakuliki asilani
    Si moto kuteketeza, kwa moshi ulio ndani
    Harufu mehanikiza, havipiti mdomoni
    Kumeingiya kiwera, shime yapatilizeni
    (mhhhhh-miminae)
  66. Laiti kuwa vyalika, tungepakuwa tukala
    Kwa njaa zilotushika, tusingechagua kula
    Rojo limeharibika, hatuliwezi kulila
    Kumeingiya kiwera, shime yapatilizeni
    (mhhhhh-miminae)
  67. Roho zinafurahika, kizuri tunapokila
    Kupikwa kiloongoka, mapishi ya mwenye mila
    Na mafya yanapowekwa, kuenjekwa bila ila
    Kumeingiya kiwera, shime yapatilizeni
    (mhhhhh-miminae)
  68. Chungu chetu cha udongo, udongo wa mfinyanzi
    Chungu chetu si cha chongo, chongo mng'ong'wa na nzi
    Chungu chetu cha mzingo, mzingo ulo na enzi
    Kumeingiya kiwera, shime yapatilizeni
    (Ahmed Rashid)
  69. Yapatilizeni shime, wazee yatatupona
    Vijana mshike sime, chatu lisije waona
    Samaki jike na dume, chunguni kurundikana
    Kumeingiya kiwera, shime yapatilizeni
    (Ahmed Rashid)
  70. Ewe baba ewe mama, umoja mshikamano
    Mabarobaro simama, kukilinda chungu hino
    Kesho kesho wanosema, katu si mfungamano
    Kumeingiya kiwera, shime yapatilizeni
    (Ahmed Rashid)
  71. Kiwera kilichozuka, ni kiwera cha wavuvi
    Tena walio Msuka, sio hawa wa Michamvi
    Watu wanalalamika, bado wanakula duvi
    Kumeingiya kiwera, shime yapatilizeni
    (Hassan)
  72. Mate Yanawadondoka, wanangoja wachuuzi
    Ajabu hawajafika, kunako shehia hizi
    Kitoweo wakitaka, washazichoka mbaazi
    Kumeingiya kiwera, shime kipatilizeni
    (Hassan)
  73. Wachuuzi wa Vinyenga, ninawapa indhari
    Bei wasijeipanga, kama ile ya jodari
    Yawaje vivyo la panga, kuuzwa kama johari
    Kumeingiya kiwera, shime yapatilizeni
    (Hassan)
  74. Basi panapo kiwera, wasizuke matapeli
    Navioze wenye ghera, ya kuuza bei ghali
    Yafaa tuwe imara, tuwadhibiti kikweli
    Kumeingiya kiwera, shime yapatilizeni
    (Hassan)
  75. Kiwera tuwe imara, tukishike kweli kweli
    Isitupate hasara, bahati si mara mbili
    Inshaallah iwe tijara, Mola twaomba kubuli
    Kumeingiya kiwera, shime yapatilizeni
    (Hassan)
  76. Na sasa ndiyo tamati, mengi tushayaeleza
    Twamaliza hizi beti, kiwera kukitangaza
    Kwa ari tujizatiti, hima tusije teleza
    Kumeingiya kiwera, shime yapatilizeni
    (Saleh Barkey)
  77. Ndugu zangu na wendani, tamati tumeifika
    Tumuombe Rahmani, Mola aso mshirika
    Tumswaliye Amini, Mtume asiye shaka
    InshaAllah muwafaka, iwe kun fayakuni
    (Ibrahim Noor)
  78. Humbo jingi limefura, karibu nasi si mbali
    Na kwetu hiki kiwera, Rabbi twaomba kabuli
    Mola tupe 'stimrara, neema zako Jalali
    Mpunguti ya Adili, kheri yawe midrara
    (Ibrahim Noor)
  79. Mtukufu mwenye sifa, wa haki Mola Manani
    Twondolee makhawifa, i-Kwako enzi na shani
    Utupe kila la sifa, nyoyo ziwe furahani
    Kafu isiunge nuni, ndiwe Adhimu Razaqi
    (Ibrahim Noor)
  80. Rabbi Mola taturidhi, atupe kila la jaha
    Ajaaliye hifadhi, na iqibali swahiha
    Haja zetu azikidhi, zizidi kwetu furaha
    Twakuombawe Ilaha, Jalla waAlaa Jalilu
    (Ibrahim Noor)
  81. Mola wetu tukirimu, utujazi kila mema
    Tuyatakayo yatimu, izidi kwetu neema
    Inshalla Mola Rahimu, tatuhifadhi daima
    Ya Rabbi tupe salama, Duniyani na Akhera
    (Ibrahim Noor)

Watunzi

Yafuatayo ni majina ya watunzi wa shairi la Kiwera kwa
ukamilifu:
1)Sk.Saleh Muhammed Barkey (Saleh Barkey)
2)Prof.Ibrahim Noor Shariff (Ibrahim Noor)
3)Dr.Kassim Omar Ali (Kassim)
4)Dr.Mbarouk Hamad Shariff (Mbarouk Mnyonge wa Nyali)
5)Dr.Hassan Omar Ali (Hassan)
6)Maher Moh'd Ahmed (Maher-Unique)
7)Sk.Ahmed Rashed Ahmed (Ahmed Rashid)
8)Bi.M.A.Masoud (mhhhhh-miminae)

 

 

 

  About Us | Zanzinet Home | Contact Us | ©2004 Zanzinet