|
|
ASO CHAKE!
Date: 18 May, 2006
- Aso chake hana lake , wala hatambulikani
Na hata kwa walo wake , yeye hawi na thamani
Neno ni la mwenye chake , aso chake hunenani?
- Aso chake ni muinga , angawa mno mwerevu
Angawa fundi kupanga , hambiwa ni mpumbavu
Kwenye mambo humtenga , angaliya nazi mbovu
- Aso chake si mzuri , angawaa kama mwezi
Aso chake si hodari , angawa mno muyuzi
Aso chake ni jauri , angawa ni mtukuzi
- Aso chake ni fidhuli , na sawa yake ni jongo
Anganena yalo kweli , huwambiwa ni mrongo
Angawa huona mbali , huonekana ni tongo
- Aso chake ni mchafu , naangawa maridadi
Na aso chake ni dufu , angawa shekhe Biladi
Hapati umaarufu , angawa mwenyeji jadi
- Aso chake rai hana , angawa ni SAQARATI
Aso chake akinena , wa kusikiza hapati
Walo wake humkana , hata muda wa mauti
- Mwenye chake ndie bwana , mwerevu mwenye busara
Angawa hana maana , hupewa yeye bendera
Husoza nasi huwona , hini ni kuu hasara
- Na hini ndiyo sababu , ya mambo kuharibika
Zimetuzidi taabu , na kwetu kumefujika
Na tamaa ya karibu , hapana kutengezeka
- Ni sharuti tubadili , na fikira tugeuze
Wakisimama wawili , mwenye chake sishunduze
Tumpe mwenye akili , ili chombo achoweze
Limetunga na Ustadh Mahmoud Ahmed Abdul Kadir (MAU) kutoka Lamu - Kenya.
Limeletwa na Sheikh Saleh Barkey
|