.

Welcome to Zanzinet Swahili Poems

Where Swahili matters!

GARI!

 

 

 

 

 

 

Related links

GARI!

Date:  16 May, 2008

  1. Kwa jina lake Muumba, Mwenyezi Mungu mmoja,
    Ambaye ameviumba, mwili na roho pamoja,
    Leo tungo naipamba, inahusu gari moja,
    Abiria jihadhari, na usafiri mbovu.

  2. Kuna gari la mtumba, limezidisha vioja,
    Laendeshwa kwa kuyumba, kweli mwisho wake waja,
    Mijini na kule shamba, kwepeni gari likija,
    Abiria jihadhari, na usafiri mbovu.

  3. Gari hili linatamba, mbio mbio linakuja,
    Ubavuni lina namba, mwishoni nitaitaja,
    Kwa rangi wamelipamba, ziko mbili kwa pamoja,
    Abiria jihadhari, na usafiri mbovu.

  4. Gari moto linapamba, latafuta wateja,
    Kila kituo latamba, abiria kuwangoja,
    Heri likabebe pamba, tumechoshwa na viroja,
    Abiria jihadhari, na usafiri mbovu.

  5. Dereva katoka shamba, gari kaja kulifuja,
    Konda wake ombaomba, anatafuta natija,
    Wapiga debe ni pumba, wapo fedha kuzingoja,
    Abiria jihadhari, na usafiri mbovu.

  6. Wakianza kujigamba, kila jema hulitaja,
    Nyimbo nyingi wataimba, ili wakidhiwe haja,
    Nendeni nao sambamba, hadi waishiwe hoja,
    Abiria jihadhari, na usafiri mbovu.

  7. Gari hilo la kishamba, roho za watu lafuja,
    Kama sumu ni ya mamba, yaua kila mmoja,
    Heri nguo ya mtumba, yaweza pata mteja,
    Abiria jihadhari, na usafiri mbovu.

  8. Anzeni shimo kuchimba, mlitupe kwa pamoja,
    Mlikokote kwa kamba, mlizike mara moja,
    Gari lisishike namba, ili tupate faraja,
    Abiria jihadhari, na usafiri mbovu.

  9. Wananchi kila nyumba, kwepeni gari likija,
    Msije kuwa manamba, mkajuta siku moja,
    Wenzenu wanajigamba, waliita NAMBA MOJA,
    Abiria jihadhari, na usafiri mbovu.

Mohammed Amir,
Morogoro

  About Us | Zanzinet Home | Contact Us | ©2004 Zanzinet