.

Welcome to Zanzinet Swahili Poems

Where Swahili matters!

KARAFUU MBOVU

 

Related links

KARAFUU MBOVU

        Huu ni utenzi kutoka kwa mzee wetu Sh. Khamis bin Nassor Al-Nabhany (Mola Amrahemu) wa Piki , Wete Pemba. Jina la utenzi ni KARAFUU MBOVU ambao ameutunga tarehe 28 Jamadul Akhir, 1381H (1961). Huu ni utenzi juu ya mambo ambayo yametokea na hata watu waliotajwa ni hakika wameishi na wengine wako hai na baadhi yao wengi humu munaweza kuwajua. Utenzi huu ni beti 325.

  1. Bisimillahi ni jina - Lake Mola Subhana,
    Ya Rabbilaalamina - Jalla wa alla taaa

  2. Ilahi Mola Wadudi - Yupweke Rabbi Wahidi
    Na mtume Muhammadi - Sayyidil anbiyaa

  3. Kwanza nastaghfiru - Kwa Mola wangu Ghafuru
    Naomba utunusuru - Na maovu ya duniya

  4. Dibaji naifupiza - Siwezi kuendeleza
    Nakhofu kuja teleza - Makosani haingiya

  5. Wala sitasema sana - Sifa za Mola Rabbana
    Kila mtu aziona - Jinsi zilivyoeneya

  6. Sasa hadithi naanza - Kiasi kuzungumza
    Na kidogo kueleza - Yaliyotupitikiya

  7. Naanza utenzi huu - Wa kisa cha karafuu
    Mazao yetu makuu - Yalivyotuozekeya

  8. Ingawa siyamalizi - Lakini siyanyamazi
    Kuvumiliya siwezi - Haddi yananikuliya

  9. Ni bora kuyaandika - Bukuni nikayaweka
    Yasijesahaulika - Yawe yakikumbukiwa

  10. Hivi kaeni tayari - Niwaeleze khabari
    Na mengi yaliyojiri - Yote tawahadithiya

  11. Tuanzie Mkoani - Mtambile na Kangani
    Kengeja na Matuleni - Tumalizie Ditiya

  12. Mote humo walichuma - Kwa sherehe na salama
    Hata siku za kuhama - Mengi wakaazimiya

  13. Wakaazimu moyoni- Wasirejee nyumbani
    Waendelee usoni - Kutafuta manufaa

  14. Kwao wasitake rudi - Wakenda walikokodi
    Hayo ndiyo makusudi - Waliyoyakusudiya

  15. Kwalizaliwa hakika - Makarafuu ya mwaka
    Kila utakapofika - Matunda yanin'giniya

  16. Nyoyo zikawatukuta - Kuuza walichopata
    Mashamba wakatafuta - Bei kubwa wakatiya

  17. Ikawa ni jitihadi - Shamba kubwa kuzikodi
    Kutwa husikiya hodi - Watu wakuhodishiya

  18. Kila atakaye kodi - Hufika kwa Masuudi
    Akaeleza muradi - Na alilokusudiya

  19. Na Masuudi husema - Ni bora kwenda tazama
    Mali muiyone vyema - Isije kuwahadaa

  20. Wahitaji hutamka - Shamba tunazunguuka
    Nasi tunafurahika - Ghilla tutainunuwa

  21. Shamba zote tumekwenda - Na mali tunaipenda
    Ela pa kujenga banda - Bado hatujapajuwa

  22. Masuudi huwajibu - Maneno yenu taibu
    Tutafanya taratibu - Mupate pa kutumiya

  23. Baada kuridhiyana - Mali wakakodishana
    Kila mtu humuona - Furaha zinamngiya

  24. Chake Chake na Msuka - Ni hayo yalitendeka
    Nami hapa nayaweka - Mengine tawatajiya

  25. Mengine nitayotaja - Ni jamaa wa Unguja
    Nao Pemba walikuja - Sababu walizoweya
  26. Pemba walipowasili - Wakenda kila pahali
    Wakasadiki ni kweli - Karafuu zimezaa

  27. Tukashikana sambamba - Waunguja na Wapemba
    Kuoneshana mashamba - Kupita tukikaguwa

  28. Mambo yakawa ni hayo - Kila shamaba upitayo
    Uambiwe utakayo - Kattu huwezi chaguwa

  29. Hapo tukakodi mali - Rakhisi wala si ghali
    Lakini jambo thakili - Ni kule kudhaminiwa

  30. Iwapo mapesa huna - Sharti ulete dhamana
    Mengi hayana maana - Ni bure hutasikiwa

  31. Mashamba yakakodiwa - Wenye fedha wakatowa
    Wengine hawakupewa - Fedha hazikutimiya

  32. Ikawa banda kujenga - Karafuu zikechanga
    Lakini siku zasonga - Mali wazipapatuwa

  33. Mara zikawa tayari - Tena zeiva vizuri
    Hapo ikawa safari - Makambini kuhamiya

  34. Tukahajiri watani - Kuhamiya misituni
    Mtu kwake humuoni - Usije mkusudiya

  35. Tukaanza kuzichuma - Na jua linasimama
    Mara mande akavuma - Ule upepo wa mvuwa

  36. Mande alipovunjika - Shuwari ikaanguka
    Wingu likamiminika - Kubwa halina mithaa

  37. Mvua ikanya mchana - Kubwa mfano haina
    Kila mtu akaona - Leo tutaangamiya

  38. Yakawa mambo marefu - Sote tukangiya khofu
    Tukaomba takhafifu - Mvua inatuzuidiya

  39. Hakika yasikitisha - Na mengine yachekesha
    Kuyasema sitayesha - Tawakatiyakatiya

  40. Mambo hayo ni thakili - Wala hayana mithali
    Mazito kama jabali - Vigumu kuyachukuwa

  41. Hadithi ya karafuu - Mazao yetu ya juu
    Yanatuvunja miguu - Twafa tunanyon'gonyeya

  42. Tunangiwa na huzuni - Tajiri na masikini
    Hatujuu hatuchini - Kama kozi twaungiya

  43. Sote twapiga siyaha - Hapana mwenye furaha
    Nyoyo zina majaraha - Kwa huzuni kutungiya

  44. Huzuni ikarefuka - Kwa mali kuharibika
    Nyengine zapukutika - Kwa kuzidiwa na mvuwa

  45. Mvuwa ikatudamiza - Karafuu zikaoza
    Hata zikangiya funza - Ikawa kuzifukiya

  46. Kila utakapopita - Utaviona vikuta
    Zishageuka mpeta - Hizo zilizobakiya
  47. Basi hapo matajiri - Ziliwaruka nadhari
    Na wanyonge mafakiri - Wakazidi teketeya

  48. Mvuwa ya mwezi mzima - Wengi yetutiya homa
    Ukatupata mughuma - Akili zikapoteya

  49. Mambo ni siku ya wiki - Mabovu hayakaliki
    Mapesa hayapatiki - Ya kulipwa vibaruwa

  50. Huona juwa latoka - Upesi tukaanika
    Mara mvuwa huanguka - Mbiyo tukenda anuwa

  51. Shani huko madukani - Ndiko kwenye mtihani
    Muhindi haonekani - Hayupo kashakimbiya

  52. Walokodi taslimu - Hao hawana fahamu
    Zinazidi darahimu - Pesa walizozitowa

  53. Walochuma mali zao - Wanakithiri kilio
    Bakhti kupata nguo - Na pesa ya kushonea

  54. Shekhe Salim Subeti - Ni tajiri madhubuti
    Alivichawanya vyeti - Watu wakavichukuwa

  55. Wengi aliwadhamini - Akitowa pesa ndani
    Alfu na alfeni - Mbali wa tisaa miya

  56. Wengine elfu sita - Watakao wakipata
    Hulifunguwa bueta - Watu kuwahisabiya

  57. Bin Subeti tajiri - Tena ni mtu dusuri
    Kwa Pemba ni mashuhuri - Kila mtu amjuwa

  58. Alizichawanya fedha - Kudhamini na karadha
    Na wala si kwa ghamidha - Alivyo akizitowa

  59. Akitowa nyingi mali - Kuwapa walokubali
    Kwa kiasi na dalili - Laki tano zatimiya

  60. Kwake ilikuwa soko - Kula saa watu wako
    Hapati kipumziko - Huyu toka huyu ngiya

  61. Bin Subeti kwa sasa - Mali yake kaikosa
    Kwa mvuwa kutupangusa - Hapana lilobakiya

  62. Mvuwa inatufilisi - Inatutiya nuhusi
    Unyonge bila kiyasi - Uliyotuelekeya

  63. Inaeneya khasara - Rabbi atupe nusura
    Isitufike idhara - Kuja tukafilisiwa

  64. Unatupata msiba - Alae hapati shiba
    Si mwana wala si baba - Msiba umeeneya

  65. Unaanza Mkoani - Wete hadi Mgogoni
    Basi Matangatuwani - Msiba wajipepeya

  66. Ama Shekhe Mselemu - Alizichuma kwa hamu
    Kwa siku sita timamu - Chungu zikamjaliya

  67. Majamvi akaongeza - Uwanja akaujaza
    Karafuu zikaoza - Moja hakuianuwa

  68. Hayo ni ya Mgogoni - Ilipoanza huzuni
    Basi Matangatuwani - Na huko yalitokeya

  69. L-azizi L-Kiyumi- Yeye ekuwa hasemi
    Kwa huzuni na mughumi - Akavunja kutembeya

  70. Temb eya ufike Konde - Huko ndiko kwenye ponde
    Ni kama tope za bonde - Ndivyo zinavyonukiya

  71. Kwa Rashidi bin Ali - Iliharibika mali
    Ikawa kucha halali - Kwa mawazo ya duniya

  72. L-Khaifi maarufu - Tena mtu wa sharafu
    Mvuwa ilimtilifu - Konde akaichukiya

  73. Hakika shekhe Rashidi - Mvuwa ilimfisidi
    Zake na alizokodi - Zote zikampoteya

  74. Msuka kwa mahabubu - Azizi bin Harubu
    Ilimfika adhabu - Kuhama na kuhamiya

  75. Alikuwa maghmumu - Hakai kichakapumu
    Ilimtoka fahamu - Akili ikapoteya

  76. Akili ikamtoka - Kwa mali kuharibika
    Akawa asikitika - Asema kinjiyanjiya

  77. Basi Msuka na Shumba - Humo watu wetirimba
    Ni mitaa ya ndaamba - Karafuu zeeneya

  78. Mvuwa yenyesha Makuwe - Ikawa kubwa Kinoe
    Watu wasijitambuwe - Bule na Maziwanjiya

  79. Bungala na Kwalegongo - Mvuwa yetiya kinyongo
    Ikaharibu mipango - Maksudi hayakuwa

  80. Tufike na Mgogoni - Ilikuwa tafrani
    Basi huyo CHEYAMENI - Alizidi kughumiwa

  81. Hamadi bin Abdalla - Mchana hataki kula
    Usiku hataki lala - Kwa huzuni kumngiya

  82. Alizichuma kwa inda - Zikajaa tele banda
    Mkutanoni akenda - Hawezi kukhutubiya

  83. Bwana mkubwa Sihaka - Yalimpata mashaka
    Kutwa akitaabika - Kuweka na kuondowa

  84. Akasema ndugu zangu - Naliya na mali yangu
    Na harusi ya mwanangu - Naona haitakuwa

  85. Kifundi hadi Kipange - Mvuwa yetiya unyonge
    Wajengao wasijenge - Jengo halikutimiya

  86. Basi kiumbe mzito - Kulikosekana pato
    Zilianikwa kwa moto - Na zote zikaunguwa

  87. Kwa upande wa Msuka - Ilikuwa pata shika
    Mvuwa ikimiminika - Nahari na lailiya

  88. Wete tusiisahau - Zilioza karafuu
    Zikapakiwa kwa dau - Baharini zikatiwa

  89. Shekhe Sultani Isa - Naye mvuwa yemtesa
    Ikamwishiya siasa - Asijuwe pa kendeya

  90. Maneno aliyosema - Sitaki tena kuchuma
    Unanipata mughuma - Fikira zinanishiya

  91. Basi kwa Abu Muniri - Mvuwa ilimuathiri
    Akamwita Hamiyari - Mwanawe akamwambiya

  92. Hima ingiya njiyani - Ukakodishe Kiwani
    Na shamba ka Makauni - Nalo piya walitiya

  93. Shamba hizo zikodishe - Moja usiibakishe
    Na nazi uziangushe - Tunachoka kununuwa

  94. Hamiyari katamka - Baba siwezi ondoka
    Mvuwa ikimiminika - Hapana wa kuondowa

  95. Mambo yekuwa Limbani - Kwa Jidde na Sefu Chani
    Pauro limkononi - Karafuu zafukiwa

  96. Jidde alichimba shimo - Ikawa zatiwa humo
    Na za Sefu humo humo - Na za bi Asha pamoya

  97. Na katika wanawake - Bi Asha tumkumbuke
    Ni kubwa taabu yake - Iliyomtokezeya

  98. Bibi Asha Muhamedi - Tabu kwake ilizidi
    Kwenda huku akirudi - Kutwa kiguu na njiya

  99. Kutulizana hapati - Wala kitako haketi
    Hata juu ya mabati - Yeye akianikiya

  100. Akizichuma bondeni - Akaja nazo nyumbani
    Na zilizo uwanjani - Nazo zajiri poteya

  101. Bibi Asha akisema - Shamba langu la Kingoma
    Linanitiya mughuma - Nikenda natekteya

  102. Mwisho esema Bi Asha - Kheri ningalikodisha
    Kama kujihangaisha - Na wahka kujitiya

  103. Chasasa kwa Kibeberu - Naye mvuwa yemdhuru
    Akasema nashukuru - Liwe litakalokuwa

  104. Kibeberu katamka - Mali inaharibika
    Azma inanitoka - Niliyoikusudiya

  105. Nalikuwa na dhamiri - Ya kwenda nunuwa gari
    Lakini nnaghairi - Fedha haikutimiya

  106. Akamwambiya nduguye - Kuchuma na tuzuwiye
    Vibaruwa tuwambiye - Kuchuma tunazuwiya

  107. Tuwambiye wende zao - Kila mtu ende kwao
    Na hayo mapesa yao - Tumo twawatafutiya

  108. Mara tukishazipata - Kwa baruwa tutaweta
    Sisi hatuna matata - Wala hatuna hadaa

  109. Na Uondwe hadi Nyali - Mvuwa yekuwa thakili
    Ikaharibika mali - Kele na Mpakanjiya

  110. Chekeya hadi Jambaji - Yalimiminika maji
    Khasara kwa wachumaji - Nao ikawashukiya

  111. Daya ilimiminika - Mvuwa kubwa kwa hakika
    Kila aliyeanika - Naapa hakuanuwa

  112. Kwenyesha mvuwa ya sifa - Isiyo na takhfifa
    Khalfani na Khalifa - Mughma ukawangiya

  113. Khalfani katamka - Kuchuma tapumzika
    Niendelee na duka - Hwenda nikafanikiwa

  114. Khalifa alizirai - Asiwezee kutalii
    Kutwa ashinda na njii - Chakula alisusiya

  115. Mkanjuni kulikondo - Kwa ndugu Hamadi Nondo
    Yeye alifanya bindo - Azowa akifukiya

  116. Hamadi Nondo esema - Kukodi nimeshakoma
    Ikiwa nataka chuma - Bora kwenda kibaruwa

  117. Mvuwa ya Makongeni - Ilihamisha wageni
    Na waliyo Tondooni - Nyuso ziliwachukiya

  118. Mvuwa haina kiasi - Tondooni ilighasi
    Shekhe Nasoro Khamisi - Ndevu asiweze nyowa

  119. Niwahadithiye Piki - Ilivyokuwa hilaki
    Mtu yundani hatoki - Kazi ni kuchunguliya

  120. Basi huyo shekhe wetu - Yeye hakisema kitu
    Ela Rabi Mola wetu - Tunusuru na Baliya

  121. Muhamedi bu Khamisi - Hakuwa na wasiwasi
    Lolote halimghasi - Hulimezeya kifuwa

  122. Akisali na kusoma - Na kuomba duwa njema
    Rabbi utupe salama - Ya akhera na duniya

  123. Hushinda msikitini - Kusali na kuadhini
    Na kumuomba Manani - Jalla wa Alla Taaa

  124. Tufike kwa Khalfani - Kutwa kucha humuoni
    Hatulizani dukani - Kero linamzidiya

  125. Khalfani bu Rashidi - Shamba nyingi alikodi
    Ikamwisha jitihadi - Zote zikamuozeya

  126. Vikuta vikajazana - Vyote vikaozeyana
    Apitaye akiona - Hahitaji kuambiwa

  127. Kadhalika na babaye - Ilimtoka suraye
    Japo echuma maliye - Huwezi muangaliya

  128. Huwezi kumtazama - Akaapo huinama
    Hanyamazi alalama - Kilemba keshakivuwa

  129. Hebu twende Kilimani - Karibu na darajani
    Karafuu zibondeni - Zote zinakokolewa

  130. Kambi ya shekhe Saidi - Mtu jusuri wa kodi
    Tena dalali anadi - Kina akikaribiya

  131. Lakini tunavyoona - Milele hakodi tena
    Kwa khasara kubwa sana - Iliyomfikiliya

  132. Kiliyo cha shekhe Isa - Aliyerudi Mambasa
    Hali yake hivi sasa - Si mzima asinziya

  133. Kanakonda kama uzi - Kula chakula hawezi
    Wala hana usingizi - Kucha ni kujinamiya

  134. Nami mtunga utenzi - Yalinipata majonzi
    Sikuwa na usingizi - Na wala sikusinziya

  135. Zangu nilizoanika - Nyengine zilikauka
    Dukani hazipeleka - Basi zilikataliwa

  136. Khasara ikanisonga - Kutwa kucha nikitanga
    Haja tembezewa kanga - Hashindwa kuzinunuwa

  137. Nyumba yangu ni nyeupe - Hataraji nizikope
    Muuzaji asinipe - Na tena akachukiwa

  138. Kanijibu kwa ukali - Kukopesha sikubali
    Neno hilo ni muhali - Sitaki kulisikia

  139. Jambo la kukopeshana - Linaondoka hapana
    Kama taslimu huna - Kanga zangu nachukuwa

  140. Kwa khabari ya kukopa - Khamisi siwezi kupa
    Najuwa hutanilipa - Ndiyo hakukataliya

  141. Miye nauza kwa haja - Sitaki ambiwa ngoja
    Kubaki shilingi moja - Siwezi kukuachiya

  142. Hamwambiya tafadhali - Niachiya kanga mbili
    Kijana hakukubali - Hayo niliyomwambiya

  143. Kanga mbili hazikosa - Sababu sina mapesa
    Nikabakiya kupwesa - Sina za kunuliya

  144. Kinyikani hadi Gasi - Kulizidi wasi wasi
    Shekhe Sefu bu Khamisi - Mvuwa yemuharibiya

  145. Alialika wajima - Nduguze wakenda chuma
    Vikuta avitazama - Hana pa kuanikiya

  146. Echumisha kwa mpanja - Akaujaza uwanja
    Akakataa kuwinja - Wenziwe wamngojeya

  147. Aliwambiya wenziwe - Mainji sasa yasiwe
    Siku hizi tupumuwe - Hakuinjiki kwa mvuwa

  148. Akawambiya jamani - Kwa sasa tupumuweni
    Hakwendeki msituni - Mainji hayatakuwa

  149. Mwenye yake akatende - Kuinja leo tusende
    Mwituni kuna umande - Nguo zetu zitarowa

  150. Siku hizi tusiwinje - Mainji na tuyavunje
    Tuwe nyumbani tukunje - Mvuwa ikitutokeya

  151. Basi Khamisi Kinenya - Mambo yalimkanganya
    Watu akiwadanganya - Waliomdondoleya

  152. Akiwambiya nendeni - Murudiye majumbani
    Nami hirudi dukani - Fedha nitawaleteya

  153. Nyote murudi makwenu - Mukafanye kazi zenu
    Na yote mapesa yenu - Takujawapelekeya

  154. Vibaruwa wakajibu - Kinenya watughilibu
    Leo twataka hisabu - Hatuna cha kutumiya

  155. Hatuwezi kuondoka - Tena tulipe haraka
    Pesa zetu twazitaka - Tumechoka kungojeya

  156. Kinenya twakukhubiri - Leo utupe shauri
    Hatuwezi kusubiri - Tunachoka khadaliwa

  157. Kama wataka matata - Tayari utayapata
    Maishayo utajuta - Kila ukikumbukiya

  158. Kinenya akenda mbiyo - Kwa babaye na kiliyo
    Maneno amwambiayo - Babaangu niombeya

  159. Baba nakuja unipe - Yule dumeo mweupe
    Hamuuze nikalipe - Vijana wataniuwa

  160. Akamjibu mwanangu - Dume mweupe si wangu
    Nami nna deni yangu - Kubwa nnayodaiwa

  161. Yule ni n'gombe wa watu - Kumuuza sithubutu
    Nami ndani sina kitu - Hakupa ukenda towa

  162. Wangu ni yule mtamba - Yule mweupe mwembamba
    Huyo siwezi mkumba - N'gombe wangu wa maziwa

  163. Sasa bora wende zako - Ukauze vitu vyako
    Ulipe madeni yako - Yaliyokushughuliya

  164. Baba kiume jikaze - Funga susu uchuuze
    Mwanagu usipuuze - Utakujashitakiwa

  165. Baba tafuta pesangwa - Hima ulipe malingwa
    Kinenya huwezi fungwa - Kifungo kina udhiya

  166. Ukifanyiza mchezo - Utapata matatizo
    Iwapo pesa hunazo - Basi utateketya

  167. Saidi Ali Mjaka - Yalimpata mashaka
    Ilikuwa aanika - Lakini hakuinuwa

  168. Hapo uwanjani pake - Akisema peke yake
    Ni kheri nipumzike - Saidi nitaumiya

  169. Najiona natilifu - Machumi yenda uchafu
    Siwezi kujikalifu - Afadhali tapumuwa

  170. Zote karafuu zangu - Zinapoteya kwa wingu
    Aidha na ndugu zangu - Wasema nawaibiya

  171. Nami naapa qasama - Shamba lao sikuchuma
    Aliyechuma ni mama - Ndiye aliyedondowa

  172. Kinyikani watu hao - Pamoja na wenzi wao
    Ni kubwa khasara yao - Iliyowafikiliya

  173. Basi Piki Mchangani - Palikuwa na mgeni
    Kwake ilikuwa shani - Namna ilivyokuwa

  174. Hadharmi wa Unguja - Naye Pemba alikuja
    Yalimfika maoja - Pemba akaichukiya

  175. Na maalim Hemedi - Mali nyingi alikodi
    Ikamshadidi hadi - Zote zikampoteya

  176. Taabu ikampata - Ya watu alioleta
    Mvuwa iliponyonyota - Wote walimkimbiya

  177. Wakabakiya wawili - Wenye ahadi ya kweli
    Wa tatu aitwa Ali - Muuzaji wa kahawa

  178. Kubwa lililomfika - Ekuwa asikitika
    Zote ziliharibika - Zile alizochumiwa

  179. Mgoli na Mavuika - Na fimbo hadi Kinyika
    Mvuwa ikimiminika - Wala haikinyamaa

  180. Makaani na Kinyuji - Yakimiminika maji
    Watu walivyotaraji - Hata moja halikuwa

  181. Mtanga mzee Khelefu - Hadithi yake ni refu
    Akenda kama kipofu - Macho hayaoni njiya

  182. Sababu alizochuma - Hepata moja nzima
    Basi alingiya homa - Akenda akiuguwa

  183. Khelefu kiliyo chake - Halilii mali yake
    Aliya kuhama kwake - Na muradi haukuwa

  184. Akarudi meli mbili - Taabani hana hali
    Yunifomu ya skuli - Selemani hekatiwa

  185. Selemani akasema - Yunifomu ni lazima
    Sikupata sendi soma - Na skuli takimbiya

  186. Khelefu akamjibu - Mwanangu utaharibu
    Kutoroka ni aibu - Nami nitalaumiwa

  187. Wakinikuta walimu - Sana watanilaumu
    Ikiwa ni yunifomu - Baba takununuliya

  188. Baba jikaze kiume - Wende shule ukasome
    Duniya uitizame - Huko tunakokwendeya

  189. Kodi ya bwana Khelefu - Ilikuwa ni dhaifu
    Na tena hakusadifu - Wala hakufanikiwa

  190. Na Shamisi Zaharani - Aliyeko Kisiwani
    Watu wekwenda muhani - Kama aliyefiliwa

  191. Na waliokuwa Finya - Karafuu zewavunya
    Wasijuwe la kufanya - Fikira zikawashiya

  192. Wa Pandani na Masipa - Walikuwa wakirapa
    Wa kule hafiki hapa - Maji yalivyoeneya

  193. Kadhalika wa Takao - Ilioza mali yao
    Mambo kwa jirani zao - Bwagamoyo na Bogowa

  194. Patini na Bahanasa - Humo mvuwa yepangusa
    Huoni mtu na pesa - Ambae aitumiya

  195. Waliyozidi Patini - Kwa Saidi Selemani
    Yeye hakitoka ndani - Kwa khofu ya kudaiwa

  196. Shekhe Saidi Riyami - Alikithiri naumi
    Kwa zile elfu kumi - Fedha alizozitowa

  197. Taabu ikampata - Eshindwa la kutafuta
    Pesa moja hakupata - Na deni yamngojeya

  198. Na shekhe Salim Sunda - Khasara ilimpanda
    Kama uzi akakonda - Kwa mali kumpoteya

  199. Maneno aliyosema - Bora nisingalichuma
    Afadhali ningelima - Roho ingelituliya

  200. Kuliko kutaabika - Kuanuwa hianika
    Na hata zikikauka - Sina wa kumuuziya

  201. Toba Ya Rabbi sitara - Imenipata khasara
    Mambo yote yanarura - Hapana lililokuwa

  202. Amma janibu za Gando - Kulikithiri kishindo
    Hakupitiki kwa vundo - Labda uzibe puwa

  203. Junguni hadi Mkote - Jumla ya watu wote
    Wekuwa kama viwete - Maguu yanyon'gonyeya

  204. Ali Hemedi wa Raha - Ilimtoka furaha
    Akipita na siyaha - Imkononi kofiya

  205. Kofiya haivaliki - Na Raha hakukaliki
    Gari haiendesheki - Mughuma unamngiya

  206. Ikawa apiga yowe - Akawambiya wanawe
    Leo bora mupumuwe - Sitaki kuanikiwa

  207. Japo mukazianika - Bure hazitakauka
    Wingu likimiminika - Itakuwa ni udhiya

  208. Akausiya wanawe - Leo Kheri mupumuwe
    Magari musiyatowe - Maji yanaziba njiya

  209. Ela bora niwatume - Mwende hima mukaseme
    Vibaruwa wasichume - Kishamba cha Madaniwa

  210. Basi skuli Ziwani - Sheke wetu Slemani
    Alikuwa taabani - Kwa alivyoozekewa

  211. Khasara walishikana - Njema ikawa hana
    Mabovu yakajazana - Asipate pa kukaa

  212. Mkasa wa Magogoni - Kwa Rashidi Sultani
    Amma ilikuwa shani - Siwezi wahadithiya

  213. Mali iliharibika - Kambini nzima yanuka
    Mwenyewe akaondoka - Mali akaikimbiya

  214. Maneno mengi aseme - Wanawake na waume
    Atakaye akachume - Zote natowa atiya

  215. Na Muhamedi Saidi - Khasara ilimzidi
    Ikamwisha jitihadi - Na mali yampoteya

  216. Akamwambiya mwanawe - Tufunge tusichumiwe
    Machumi yenda kwa gowe - Hwenda yakatuchachiya

  217. Ama shekhe Muhamedi - Mengi aliyaradidi
    Ikawa hapana budi - Kidimni kuhamiya

  218. Alipohamiya huko - Alizidi sikitiko
    Mradi kila endako - Hana faka ya kukaa

  219. Barawa hakukaliki - Kidimni hakwendeki
    Harubu kwenda hataki - Kwa huzuni kumwingiya

  220. Msiba umemfika - Aliya asikitika
    Zile alizoanika - Nazo zimemvimbiya

  221. Akamwambiya babaye - Baba kheri utuliye
    Kazi taifanya miye - Nikichoka tapumuwa

  222. Kutakao Hababuu - Aliumiya miguu
    Kwa kuoza karafuu - Hanyamaziki kuliya

  223. Aliyo akitamka - Mwaka huu ndiwo mwaka
    Khasara ilonifika - Nisiyoitegemeya

  224. Asema kiliyo changu - Yananizidi matungu
    Mali ya watu na yangu - Jamii imepoteya

  225. Sililii hizi zetu - Muhamedi sina kitu
    Naliya mali ya watu - Sina pa kuivumbuwa

  226. Azizi Saidi Komba - Nae mvuwa yemkumba
    Asilijuwe la kwamba - Kelele zikamwishiya

  227. Zikamwishiya kelele - Jamaa zake wa Ole
    Wakenda kumpa pole - Hawezi waitikiya

  228. Neno alilotamka - Naliya hisikitika
    Zote zinaharibika - Zile nilizochumiwa

  229. Inanifika hilaki - Kichemi hakukaliki
    Na Ziwani hakwendeki - Kwa kero la vibaruwa

  230. Saninga siwezi kwenda - Nikenda roho yadunda
    Maji yanajaa banda - Nikifika naghumiwa

  231. Barawa kwa masharifu - Kwa Alawi bin Yusufu
    Kulikuwa na uchafu - Ziligeuka makaa

  232. Zikawatiya kinyongo - Yakawashiya maringo
    Zilikuwa kama dongo - Tope za kukandikiya

  233. Hapo esema Alawi - Myaka yote sidaiwi
    Mwaka huu siyajuwi - Mambo yatavyokuwa

  234. Yusufu nakueleza - Mambo yamenishangaza
    Hidaiwa nitauza - Shamba la Tumbi wa kaa

  235. Yusufu akamjibu - Kwa maneno ya ghadhabu
    Neno hilo si muhibu - Kwa miye sitaridhiya

  236. Tumbi wa kaa kuuzwa - Alawi tutamalizwa
    Barawa tukifukuzwa - Wapi tutakimbiliya

  237. Utatupata mughuma - Tusiweze kusimama
    Nasi Shumba tushahama - Haijuzu kurudiya

  238. Tukiuza mali yetu - Hatutakuwa na kitu
    Tukipita kwa wenzetu - Si hasha kutuzomeya

  239. Kanambe hadi Makumbi - Maji yepiga msingi
    Watu wakavunja kambi - Wengine wakakimbiya

  240. Wakavunja kambi zao - Wakarejeya makwao
    Sababu mabanda yao - Mengi yewavunjikiya

  241. Bakari Abdrahmani - Ilimtoka imani
    Akasahau hisani - Kubwa aliyofanyiwa

  242. Alikodi akachuma - Kwa sherehe na salama
    Mali akiitazama - Nyingi kajikusanyiya

  243. Lakini mvuwa yenyesha - Bakari hajakausha
    Kazi ajishughulisha - Fikira zinamwishiya

  244. Akawa mtapitapi - Hana khofu haogopi
    Vibaruwa hawalipi - Kaziye awahadaa

  245. Ubaya akawafanya - Vibaruwa kuwabinya
    Mwisho aliwanyan'ganya - Pesa moja hakutowa

  246. Basi wachumaji hao - Hakuwapa pesa zao
    Na yeye hana kituo - Deni inamzidiya

  247. Vibaruwa wakasema - Bakari si mtu mwema
    Kazi yake ni dhuluma - Ndiyo aliyozoweya

  248. Na Omari Athumani - Kwa kodi hawezekani
    Ni jasiri kwa yakini - Sifaye mtu hupewa

  249. Shamba nyingi alikodi - Kwa shime na jitihadi
    Alfu nane lukudi - Fedha alizozitowa

  250. Akaweka watu wake - Kuchumiwa mali yake
    Waume na wanawake - Wote wakaimchumiya

  251. Zikachumwa kwa haraka - Mali ikakusanyika
    Wingu likamiminika - Nahari na lailiya

  252. Hapo alipoziweka - Ekwenda akazishika
    Zinavimba zatumbuka - Akazifanya mboleya

  253. Akawambiya wanawe - Nendeni mukazizowe
    Zote mukazikokowe - Sitaki zishuhudiya

  254. Muzizowe kwa mabamba - Zote muzirovye shamba
    Mashimoni mwa migomba - Mupite mukizitiya

  255. Athumani kaondoka - Machozi yapukutika
    Na Musa asikitika - Kwa yale yalotokeya

  256. Watoto wakalizana - Kina wakiambiana
    Baba yetu pesa hana - Za kodi na vibaruwa

  257. Kikaanguka kiliyo - Na maneno yasemwayo
    Baba mapesa hanayo - Hwenda akashitakiwa

  258. Shekhe Omari kasema - Deni linaniandama
    Unaningiya mughuma - Fikira zinanishiya

  259. Hii ni bakhti yangu - Kunipiga ulimwengu
    Mali ya watu na yangu - Yote yananipoteya

  260. Wanangu musiogope - Roho naziwe nyeupe
    Tauza mali nilipe - Deni nnayodaiwa

  261. Kwanza nitauza nyumba - Na kikataa cha shamba
    Na n'gombe wangu mtamba - Tamuuza atakiwa

  262. Azizi shekhe Salimu - Ekodi mali kwa hamu
    Akawaita hirimu - Ili kuja mchumiya

  263. Akachuma zikaoza - Iikawa zamshangaza
    Hata siku ya kuuza - Mali haikutakiwa

  264. Vibaruwa wamdai - Wataka pesa za chai
    Salimu awalaghai - Kina akiwazuzuwa

  265. Vibaruwa wakajibu - Salimu watughilibu
    Hima fanya taratibu - Hatutaki zuzuliwa

  266. Salimu sibu shauri - Hima usitaakhari
    Na tena twakukhubiri - Khadaa zitakwishiya

  267. Salimu yake maqali - Sina kitu sina hali
    Bora mustahamili - Nami nawatafutiya

  268. Vibaruwa wasemayo - Itakwisha khadaayo
    Pesa zetu hii leo - Tupe bila kupunguwa

  269. Twazitaka pesa zetu - Haraka turudi kwetu
    Jawabu ya sina kitu - Hatutaki kuambiwa

  270. Hapo Salimu Nasoro - Kikamjiya kihoro
    Akajifanya mtoro - Atoroka vibaruwa

  271. Jamaa wa Kibochano - Na wale wa Meli tano
    Wote wakishika vyano - Karafuu zafukiwa

  272. Birikau na Mavungwa - Mabanda yameshajengwa
    Wachumaji wakapangwa - Siku ya kwenda hamiya

  273. Siku ya uhamiaji - Yakamiminika maji
    Yote waliyotaraji - Wasipate hayakuwa

  274. Shangafu Hindi na Jojo - Khasara kubwa na fujo
    Wakakata mikongojo - Fimbo za kuchechemeya

  275. Kokole na Pondeyani - Na N'gambwa na Miburani
    Zilioza majamvini - Zilishinda kuanuwa

  276. Muradi kila wendako - Ukifika mvuwa iko
    Mkanjuni ndiko huko - Watu walikoumiya

  277. Nasoro bin Majidi - Na L-baqashi Asedi
    Shilingi arba ziadi - Ndiyo aliyochukuwa

  278. Walikodi shamba hiyo - Watu wakaliya choyo
    Pato lao ni kiliyo - Kina wakiomboleya

  279. Waliya wakiongeza - Kwa mali yao kuoza
    Na hizo zilizosaza - Ni bahati kutakiwa

  280. Basi tukenda usoni - Kuna kijana Amani
    Alikodi Kuungani - Pamoja na Tundauwa

  281. Bwana huyo wa kimanga - Khasara ilimsonga
    Kutwa kucha akitanga - Kwenda kiguu na njiya

  282. Waliyopata maoja - Siweshi nikiwataja
    Pemba hapana mmoja - Ambaye alibakiya

  283. Ikatufika dharuba - Pasiwe mwenye akiba
    Hata nusu ya kibaba - Sikwambii kwa guniya

  284. Na hizo zilizosaza - Hapana pa kuziuza
    Wahindi watufukuza - Nao zinawajaliya

  285. SI-JI-EE ukiifika - Ni vivyo kutaabika
    Ukipewa pa kueka - Kupima utangojeya

  286. (SI-JI-EE = C.G.A. = Cloves Growers Association)

  287. Aibu ya SI-JI-EE - Ukenda sharti ukae
    Karani akuringie - Uwe wampembejeya

  288. Karani huyo taringa - Kina akikusimanga
    Aseme zina mchanga - Ni lazima kutolewa

  289. Ni mbichi zikakaushwe - Zina taka zisafishwe
    Nzima tuzipasishe - Karani atakwambiya

  290. Moyo takupiga fundo - Akufanyiye kishindo
    Sharti utaje magendo - Ndipo utakubaliwa

  291. Kama magendo hutowi - Ujuwe hupasishiwi
    Karafuu hupimiwi - Wallahi nakuapiya

  292. Ukifanya ukaidi - Utakwenda ukirudi
    Mwisho uwe huna budi - Maliyo kuichukuwa

  293. Magendo ukikubali - Zitapasi hazifeli
    Tena kwa muda qalili - Fedha utahisabiwa

  294. Tena pana wachukuzi - Wanakaa domo wazi
    Iwapo huwakonyezi - Hawaligusi guniya

  295. Hilo sharti ulijuwe - Wote wataka wapewe
    Ulichonacho mugawe - Pekeyo hutaachiwa

  296. Sasa twende kwa Wagunya - Tujuwe walivyofanya
    Nguo walizochawanya - Watu wakazichukuwa

  297. Wakiwakopesha watu - Vitambaa na viyatu
    Khasara wageni wetu - Nao ikawashukiya

  298. Hiyo siku ya kudai - Huondolewa kwa rai
    Na kupigwa ulaghai - Na nguo zishavaliwa

  299. Yamini naweza apa - Jamii waliokopa
    Hapana aliyelipa - Na mwisho walikimbiya

  300. Amma yewafika mambo - Watembezaji urembo
    Shida kuu na vikumbo - Kutwa kiguu na njiya

  301. Hutanga na mabahasha - Kupita wakikopesha
    Bure kujihangaisha - Na fedha zikapoteya

  302. Waliondoka Mambasa - Kuja tafuta mapesa
    Wasipate wakakosa - Nauli ya kurudiya

  303. Na mafundi charahani - Wakishinda barazani
    Sabaha hadi jioni - Hawana cha kutumiya

  304. Hushinda kutwa mchana - Huoni fundi kushona
    Wengine huambiana - Tushoneni sidiriya

  305. Tutashona tukiuza - Watu wengi wauliza
    Nyengine tutatembeza - Mwenye pesa tanunuwa

  306. Na hao wenye magari - Ziliwesha tazbiri
    Dereva na matajiri - Wasijuwe pa kwendeya

  307. Huona gari zapita - Hawana walichopata
    Hata pesa za mafuta - Ilitabu kutimiya

  308. Garini watu hujaa - Wasipate pa kukaa
    Ashukae hushangaa - Hana pesa za kutowa

  309. Na wapikaji miseto - Kutwa huchezeya moto
    Jioni hawana pato - Uji hewenunuliya

  310. Hatokei mnunuzi - Apitae haulizi
    Huwapata bumbuwazi - Mseto unachelewa

  311. Na wachinjao magombe - Hawana faida chembe
    Wakiuza hata pembe - Mikamo wakifukiya

  312. Na wakifanya hisabu - Pato lao ni taabu
    Pesa zao zinaghibu - Nyingi zinawapoteya

  313. Apatae sigireti - Akikosa kibiriti
    Mawili yote hupati - Usijeyatumaniya

  314. Kila mwenye biashara - Ilmpata khasara
    Mambo yote yalirura - Hapana lililokuwa

  315. Kasoro iliyopita - Wengi iliyowapata
    Kila unayemkuta - Ana kiliyo aliya

  316. Yaliyopita ni hayo - Na zaidi mengineyo
    Hayo ndiyo matokeyo - Pemba yaliyotokeya

  317. Na sasa nakhitimisha - Mwisho hapa nafikisha
    Mengi nnayabakisha - Siwezi kuendeleya

  318. Haya niliyoandika - Hata nusu sikufika
    Naona yakirefuka - Hwenda nikaja poteya

  319. Ndiyo nikatiya tamma - Kuandika hasimama
    Fahamu sinayo vyema - Na kutunga sijajuwa

  320. Ni kazi kubwa kutunga - Na maneno kuyapanga
    Nami bado ni mjinga - Moyo haujatuliya

  321. Moyo sijatulizana - Nikabaguwa maana
    Ela nawambiya jina - Mupate kulitambuwa

  322. Niwambiye jina langu - Na jina la baba yangu
    Jina la mtaa wangu - Nalo nitawatajiya

  323. Jina langu ni Khamisi - Mtu fakiri mchesi
    Lolote halinighasi - Hulimezeya kifuwa

  324. Nasoro ni baba yangu - Mpenzi wa moyo wangu
    Piki ni mtaa wangu - Ndipo nilipozaliwa

  325. Ni mzalendo wa Pemba - Na mimi nakaa shamba
    Kazi yangu ni migomba - Kupanda nikilimiya

  326. Kadi tamati utenzi - Nimechoka sijiwezi
    Kwa yote siyamalizi - Mengi sikuyatambuwa
  327. TAMMA

    Sk. Khamis bin Nassor Al Nabhani [28 Jamadul Akhir, 1381H (1961)].

    Limeletwa na Saleh Barkey

     

  About Us | Zanzinet Home | Contact Us | ©2004 Zanzinet