KARAFUU MBOVU (Sehemu ya pili)
Sh. Khamis Bin Nassor (Mola Amrahemu), baada ya kukamilisha utenzi kuhusu
karafuu zilizoharibika kutokana na mvua kali iliyonyesha
mwaka 1961, aliandika tena juu ya mada hiyo katika mwaka 1962
lakini ameelezea khasara iliyowakuta watu wa Mkoani tuu
- Yaliyopita Msuka - Ya mali kuharibka
Mwaka ulipopinduka - Na Bopwe yalitokeya
- Yalizaliwa kwa kweli - Makarafuu ya vuli
Kwa wingi kila pahali - Kazole zikaeneya
- Bopwe kwa kila wendako - Karafuu nyingi ziko
Mkoani ndiko huko - Khasa zilikohamiya
- Kipapo na Kichunjuu - Huwezi tizama juu
Kwa wingi wa karafuu - Uzazi unatimiya
- Zilizaa nyingi sana - Za watu kuonyeshana
Bopwe nzima hapana - Ambapo panabakiya
- Washitiri wakafika - Wa Wete na wa Msuka
Ikawa ni pata shika - Kupita wakikaguwa
- Kila shamba upitalo - Ni zuri lipendezalo
Nalo ndilo litakwalo - Washitiri wawaniya
- Washitiri watamka - Mali hii twaitaka
Na bei tuliyofika - Yafaa kubarikiwa
- Akasema mwenye mali - Iwapo mushakubali
Tumngoje shekhe Ali - Sasa hivi tatokeya
- Shekhe Ali akafika - Hata hajapumzika
Washitiri kwa haraka - Nao wakamtokeya
- Bwana Ali kashakuja - Wala yeye hana hoja
Ela liko neno moja - Alisema hasikiya
- Neno alilodhukuri - Kuwambiya washitiri
Katazameni vizuri - Nipate wabarikiya
- Pana jengine muhimu - Na hilo mulifahamu
Sharti fedha taslimu - Moja isije punguwa
- Akasema shekhe Ali - Taslimu fil hali
Kukopesha sikubali - Na wala sitaridhiya
- Wengine wakakodishwa - Wengi wakahangaishwa
Wengine wakakopeshwa - Ambao waaminiwa
- Mashamba yakakodiwa - Wenye fedha wakatowa
Wengine wedhaminiwa - Kodo ikategemeya
- Basi hapo washitiri - Wakakaa kusubiri
Zilipokuwa tayari - Kambini wakahamiya
- Waliyo na mali yao - Zinatuwa roho zao
Wawangoja watu wao - Wapate kuwachumiya
- Hata siku za kuchuma - Ikaanguka zahama
Mvuwa ikatuandama - Kubwa haina mithaa
- Ilianza Mkoani - Kichunju na Kangagani
Khususa Mkanyageni - Kivumbi Mtu haliwa
- Ukipita Mtambile - Watu wote ni wawele
Yafaa kupewa pole - Maradhi yanawangiya
- Wambaa hata Kengeja - Ilikuwa tafrija
Mvuwa ya moja kwa moja - Nahari na layliya
- Basi Gae la mtungi - Mvuwa ilikuwa nyingi
Haikutosha msingi - Karafuu zepoteya
- Chonga Mkungu Kipapo - Humo mvuwa yekuwapo
Mtu hatoki alipo - Kwa maji kuwazidiya
- Ama upande wa Jonza - Ilikuwa miujiza
Namna zilivyooza - Siwezi wahadithiya
- Mvuwa iliyokuwako - Sehemu za Kunguziko
Yoyote hana endako - Matope yanaeneya
- Mtu hatoki kwa tope - Havai nguo nyeupe
Na upande wa Kigope - Ukipita wateleya
- Mgagadu na Kuyuni - Kulikithiri huzuni
Watu wote taabani - Kwa kuzidiwa na mvuwa
- Mangurumo na umeme - Yalikuwa Jambangome
Wanawake kwa waume - Nyuso zikawafiziya
- Upande wa Mgelema - Mvuwa nyingi ikavuma
Muda wa wiki nzima - Halionekani juwa
- Ukipita Mizingani - Wanunuzi kituoni
Hawaigusi mizani - Hawana cha kununuwa
- Ngwani hadi Chemi - Kulikithiri huzuni
Watu wote hawasemi - Kazi yao ni kuliya
- Waliya hawanyamazi - Kwa huzuni na majonzi
Hawapati usingizi - Huwaoni kusinziya
- Waliya kiomboleza - Hawana la kufanyiza
Macho yanagiya kiza - Kutwa ni kujinamiya
- Ama Sipesi na Kendwa - Mitaa hiyo yekwendwa
Lakini wote weshindwa - Kodi ikawachachiya
- Ikawachachiya kodi - Ikawesha jitihadi
Ikawa hapana budi - Wengine kufilisiwa
- Vizuke hadi Nanguji - Yalimiminika maji
Yote waliyotaraji - Wasipate hayakuwa
- Alikodi moadhamu - Hemedi bin Salimu
Ilimtoka fahamu - Kidogo akaghumiwa
- Akatamka Hemedi - Sina tena jitihadi
Najuta miye kukodi - Bora ningelipumuwa
- Inanipata taabu - Na mashaka na adhabu
Mali yangu inaghibu - Na nyengine nadaiwa
- Tamaa ilinishika - Nisiweze ifunika
Yananipata mashaka - Na mali inapoteya
- Hii ni bakhti yangu - Kunipiga ulimwengu
Naapa mapesa yangu - Kodi nitaikimbiya
- Jonza Khamisi Hemedi - Mali ya watu hakodi
Na alivyo mkaidi - Yake hataki itowa
- Washitiri wakifika - Yeye huwa awacheka
Nyuma akizunguuka - Hayupo keshakimbiya
- Hayupo haonekani - Wala hakai nyumbani
Hadi saa za jioni - Karibu juwa kutuwa
- Utamuona yuwaja - Mwendo wa kujikongoja
Na hayo si mara moja - Hiyo ni yake tabiya
- Wageni hawaondoki - Na kukodisha hataki
Na wala hasemezeki - Huna la kumwambiya
- Mwisho hufanya ubishi - Akasema sikodishi
Mwenyewe hazinitoshi - Naomba kusamehewa
- Ingawa bado ni changa - Lakini banda najenga
Na hivi natangatanga - Watu wa kunichumiya
- Nimeshakusnya pesa - Zi tayari hivi sasa
Na watu sitawakosa - Wa kuja niokoteya
- Sasa niwape mahali - Mwende mukakodi mali
Karibu wala si mbali - Na jina tawatajiya
- Ni bora niwaeleze - Mwende mukabembeleze
Mufike musikilize - Salehe awangojeya
- Shekhe Salehe Saidi - Iwapo muna lukudi
Mukifika mutakodi - Haja yenu itakuwa
- Ana shamba la fakhari - Ni kubwa tena ni zuri
Naye si mtu jeuri - Bashasha azitambuwa
- Salehe ni maarufu - Na shamba lake nadhifu
Ni zuri wala si chafu - Kila mwaka alimiya
- Washitiri wakafika - Salehe hajaondoka
Nao wakafurahika - Kwa kule kumkutiya
- Wakafurahika sana - Kwa Salehe kumuona
Nao wakaambizana - Bora kumuhadithiya
- Wakasema tunakuja - Tunakusudiya haja
Tukodishe shamba moja - Ndilo tulilokujiya
- Na kama iko ya pili - Ikiwa haiko mbali
Juu yetu si thakili - Pamoja kuzichukuwa
- Salehe akakubali - Akawapa shamba mbili
Kaona ni afadhali - Kama kuwazuiliya
- Yakamaliza maneno - Wakaeka maagano
Watowe elfu tano - Zibaki tisaa miya
- Mikono wakapeyana - Shamba wakakodishana
Tena wakaoneshana - Pahala pa kutumiya
- Maneno yalipokwisha - Mabanda wakajengesha
Kuchuma wakaanzisha - Ikamiminika mvuwa
- Kwa hakika watu hao - Ilighibu mali yao
Wasipate hata nguo - Ikawa kudirikiwa
- Hawakupata tijara - Bali wepata hasara
Kwa mvuwa kuwakwangura - Msiba ukawangiya
- Ukawangiya msiba - Kula hawapati shiba
Wenda wakipiga toba - Pesa zao kupoteya
- Mvuwa iliposhtadi - Ikawa kubwa shadidi
Mchana ukasawidi - Mvuwa ilivyoeneya
- Maji yakamiminika - Na maradi kuwalika
Zote zikaharibika - Zile walizochumiwa
- Kilindi na Kuungeni - Huko ilikuwa shani
Khasara Matwaiwani - Nao ikawashukiya
- Watu wa mitaa hiyo - Walikiyhiri kiliyo
Kwa mali waliyonayo - Na ilvyowachachiya
- Shekhe Issa Twaiwani - Alikuwa taabani
Kutwa yupo barazani - Kimya kanajinamiya
- Echuma akazipata - Akavijaza vikuta
Mvuwa iliponyonyota - Kuchuma akazuwiya
- Karafuu zikaoza - Nyumbani akazijaza
Hata juu ya baraza - Yeye akianikiya
- Nyingi zikaharibika - Nyingi zikapukutika
Hizo zilizokauka - Nyeusi kama makaa
- Shekhe Issa akakonda - Asijuwe la kutenda
Na wala hana pa kwenda - Fikira zikamwishiya
- Akasema shekhe Issa - Karafuu nishakosa
Na ndani sina mapesa - Ya kulipa vibaruwa
- Mambo yananishangaza - Sijuwi la kufanyiza
Sina budi tamuuza - N'gombe wangu wa maziwa
- Tamuuza n'gombe wangu - Nifiche aibu yangu
Kwani ndiyo kilimwengu - Nakhofu kuadhiriwa
- Japo tapata khasara - Kuuza n'gombe ni bora
Naikimbiya idhara - Iliyonielekeya
- Basi Chemi kwa Kikasa - Huko mvuwa yepangusa
Watu wote wakakosa - Waliyoyakusudiya
- Wote waliokuwako - Viliwafika vituko
Ikawa ni sikitiko - Kwa yaliyowazukiya
- Nabahani Muhamedi - Kwa Kikasa akakodi
Elfu kumi lukudi - Pamoja alizotowa
- Na hata akishachuma - Elfu yamtazama
Mbali mambo ya gharama - Shilingi tisaa miya
- Hizo ni vile akenda - Na magarini kupanda
Na za kujengesha banda - Pahali pa kutumiya
- Akaja na watu wake - Waume na wanawake
Akaanza kazi yake - Muda umeshawadiya
- Akahamiya akesha - Shamba la kufurahisha
Kuchuma akaanzisha - Bila ya kukawiliya
- Echuma muda wa wiki - Haraka hapumziki
Lakini hazikauki - Ni mbaya hali ya hewa
- Ikanya mvuwa kikweli - Ikaharibika mali
Uso ukatabadali - Mweusi ukafifiya
- Zote ziliharibika - Moja haikukauka
Na za juu zaanguka - Za chini zakokolewa
- Ikawa khasara yake - Pesa za watu na zake
Na nyengine apeleke - Hana pa kuzizumbuwa
- Ikamjiya nadhari - Ende aliko tajiri
Ili ampe khabari - Kwa yale yalotokeya
- Hapo hakutaakhari - Akenda hana nadhari
Kamueleza khabari - Na huku ajinamiya
- Akenda hadi Pujini - Hali yake tabani
Hajuwi aseme nini - Fikra zinamwishiya
- Pujini akawasili - Kwa Salimu bin Ali
Akashtakiya hali - Mengi akaelezeya
- Yote akamueleza - Hata moja hakusaza
Tajiri kananyamaza - Kama asiyesikiya
- Tajiri akatamka - Hayo najuwa hakika
Lakini sijatosheka - Na wala sijaridhiya
- Shamba nilikukodisha - Fedha ukasalimisha
Zile zilizobakisha - Nazi nzihitajiya
- Mengine miye sitaki - Na wala sisemezeki
Labda shamba la Piki - Ukinipa tachukuwa
- Tachukuwa kwa thamani - Au tashika rahani
Ukinilipa mwakani - Shamba takurudishiya
- Muhamedi ndugu yangu - Ni hayo maneno yangu
Nazitaka pesa zangu - Uwe hali ya kujuwa
- Muhamedi kakalimu - Sikiza sheke Salimu
Kukulipa ni lazimu - Usidhani nakataa
- Lakini kwa hivi sasa - Similikimhata pesa
Kwa sababu nimekosa - Yamini nakuapiya
- Shekhe Salimu naapa - Sikatai kukulipa
Kama napata kukopa - Deni nigelichukuwa
- Nikachukuwa kwengine - Hakupa tusigombane
Na sasa tusikizane - Maliyo takuleteya
- Takupa kitu rahani - Ukishike kwa thamani
Hata tufike mwakani - Panapo majaaliwa
- Mwakani takuja nazo - Pamoja zote pesazo
Kwangu mimi pesa hizo - Siwezi kuzuwiliya
- Tajiri hakuyarudi - Maneno ya Muhamedi
Sababu hapana budi - Kwa hivyo akaridhiya
- Shekhe Ali bin Juma - Kitongani alihama
Ulimpata mughuma - Ole akenda hamiya
- Na alipofika huko - Ni vivyo jua haliko
Likazidi sikitiko - Asijuwe pa kwendeya
- Akamwambiya nduguye - Ewe Khamisi siliye
Si weye wala si miye - Khasara inaeneya
- Haya yaliyotufika - Hutokeya kila mwaka
Wengine husikitika - Na wengi huvumiliya
- Mwaka huu yako kwetu - Lakini si peke yetu
Ni pamoja na wenzetu - Yaliyotufikiliya
- Sasa tustahamili - Tumfike mwenye mali
Tukamliliye hali - Tuombe kupunguziwa
- Tena twende kwa haraka - Isiwe kuakhirika
Pengine ataondoka - Si mtu wa kutuliya
- Shekhe Ali na Khamisi - Wakenda mbiyo upesi
Huku wana wasi wasi - Khofu inawazidiya
- Wakamfika tajiri - Pasi na kutaakhari
Yote wakamkhubiri - Waliyoyakusudiya
- Shekhe Ali katamka - Bwana kwako tumefika
Neno tunalolitaka - Ni vizuri kukwambiya
- Tumekuja na mawili - Moja wapo ukubali
Na ingawa ni thakili - Lakini ndiyo duniya
- La kwanza tusamehewe - La pili tupunguziwe
Na gharadhi tuondowe - Uwe watuhurumiya
- Utuonee huruma - Hatuwezi kusimama
Mwiba uliotukwama - Hatuwezi kuutowa
- Inatupata khasara - Yaoneke kwa jahara
Tena inatukwangura - Na hila zinatwishiya
- Ni hayo tukwambiyayo - Nawe sema upendayo
Wasemaje manenoyo - Jawabu twahitajiya
- Tajiri naye kajibu - Shekhe Ali ni muhibu
Maneno yenu twaibu - Yote nimeyasikiya
- Lakini nawaeleza - Mengi mulozungumza
Ama yananishangaza - Tena yananikuliya
- Kwa hayo muliyosema - Kwa uzani hiyapima
Kwangu hayakuinama - Uzito unapunguwa
- Niliwakodisha mali - Rahisi wala si ghali
Kusamehe sikubali - Siwezi wapunguziya
- Kuwasamehe siwezi - Pesa moja sipunguzi
Na tena kwa siku hizi - Fedha nazihitajiya
- Mulivyokubali kodi - Mali yangu hairudi
Ikiwa hapana budi - Nawapa shilingi miya
- Zitabaki alfeni - Hizo tuandike deni
Muje mulipe mwakani - Rabi akitujaliya
- Maneno yangu ni hayo - Wala sina mengineyo
Fedha ndiyo nitakayo - Nipate kuzitumiya
- Kwa hivyo wakaondoka - Na machozi yawatoka
Nyuso zinasawijika - Majoinzi yanawangiya
- Kitongani wakahama - Na deni yawatazama
Wakajutiya kukoma - Kwa deni kuwakuliya
- Ama Abedi Rajabu - Ilimfika taabu
Ikawa ndiyo sababu - Mali yake kupoteya
- Alikuwa akichuma - Mtaa wa Giriyama
Kila kizitizama - Chungu zimemjaliya
- Ikamfika hilaki - Ambayo haisemeki
Kupewa jema hataki - Kazi yake achukiwa
- Akija Mtu Haliwa - Huagiziya kahawa
Hapokei akipewa - Jinsi alivyoghumiwa
- Sheke Abedi Rajabu - Mambo yalimuadhibu
Akangiwa ni ghadhabu - Zote akazifukiya
- Na nyuma viko vikuta - Huku mvuwa yanyonyota
Kuzichima akajuta - Kwa zilivyomuozeya
- Zote zikaharibika - Majamvi yamun'gunyuka
Na mvuwa yapukutika - Bado haijanyamaa
- Akipiga makelele - Apita huku na kule
Uwanjani tope tele - Hana pa kuanikiya
- Kambi yake mlimani - Ina vikuta wanjani
Karafuu za bondeni - Zote zinakokolewa
- Yakmjiya mahana - Hapati kutulizana
Si usiku si mchana - Kutwa kiguu na njiya
- Wale wamchumiyao - Wataka rudi makwao
Wazitaka pesa zao - Hawana cha kutumiya
- Kwa lazima azitowe - Wala asiwasumbuwe
Zote awape wenyewe - Moja isije punguwa
- Pakaingiya mzozo - Abedi pesa hanazo
Ikawa ni matatizo - Ikaanguka ghasiya
- Ikawa ni kugombana - Hapana kusikizana
Karibu na kupigana - Abedi na vibaruwa
- Basi mambo ya Tasini - Kwa Abdul Rahamani
Naye epata huzuni - Kubwa isiyo mithaa
- Abdul Rahamani Khalidi - Mvuwa ilimhusudi
Zote alizozikodi - Jamii zilipoteya
- Zilimpoteya zote - Hata moja asipate
Kutumwa mtu amwite - Basi huyo akimbiya
- Ama Sefu Muhamedi - Kwake mambo yalizidi
Kwenda huku akirudi - Tasini hawezi kaa
- Na huko Mkanyageni - Nako ilikuwa shani
Abdalla Khalfani - Mughma unamngiya
- Ulimpata mughuma - Asijuwe la kusema
Zile alizozichuma - Zilimharibikiya
- Zote ziliharibika - Machozi yakamtoka
Kwa kazi ya kuanika - Hapati za kuanuwa
- Basi Omari Bakari - Cheyameni mashuhuri
Mvuwa ilimkithiri - Na mengi yakatokeya
- Hakika Mkanyageni - Ilikuwa kisirani
Hususa kwa cheyameni - Mambo yalimkuliya
- Akijikeketa meno - Akaeka mkutano
Akenda hana maneno - Hawezi kukhutubiya
- Akamwambiya katibu - Nisemalo likutubu
Maneno hiyaharibu - Nirudisha hipoteya
- Kwa sababu moyo wangu - Si hadhiri ndugu yangu
Nafikiri ulimwengu - Ulivyonielemeya
- Sikodi tena maisha - Na zangu tazikodisha
Ucheyameni watosha - Hayo nijiaguliya
- Mambo ya Mkanyageni - Ya Omari cheyameni
Na Abdulla Khalfani - Nishawazungumziya
- Kangani tusisahau - Zilioza karafuu
Zilizo chini na juu - Jamii zilipoteya
- Shekhe Salehe Hemedi - Ni jusuri wa kukodi
Khasara ilimzidi - Shamba aliyochukuwa
- Yalimpata matata - Akawa yeye ajuta
Alikosa hakupata - Makusudi hayakuwa
- Ama Rashidi Saidi - Kwa khasara alizidi
Ikawa hapana budi - Maliye kuchukuliwa
- Alishikwa akabinywa - Asemayo akakanywa
Maliye akanyan'ganywa - Yote hakubakishiwa
- N'gombe dume na mtamba - Jamaa waliwakumba
Bakhti yake ni nyumba - Ndiyo aliyoachiwa
- Mvuwa yekuwa Chokocho - Pasiwe kipatikacho
Ridhwani afichacho - Si kazi kufichuliwa
- Kwa hakika Ridhwani - Alikuwa taabani
Kwa shamba la Mchangani - Ndilo lililomuuwa
- Ridhwani akasema - Unanipata mughuma
Hata moja sikuchuma - Nami huku nadaiwa
- Mapesa nidaiwayo - Ni mengi wala sinayo
Mwaka huu ni kiliyo - Kilichonifikiliya
- Naye ndugu Juma Kombo - Ekodi shamba kwa Yambo
Yakamfika majambo - Asiyoyategemeya
- Shamba ekodi kwa pupa - Na pesa ni za kukopa
Asipate cha kulipa - Kodi ilimchachiya
- Juma Kombo kimuona - Alivyongiya mahana
Ukimwita hukuguna - Tena hukunyamaziya
- Japo mwite haitiki - Wala hana urafiki
Kusema yeye hataki - Mara hukuhamakiya
- Juma Kombo tumjuwe - Chokocho ndiye mjiwe
Ridhwani jiraniye - Pamoja wanapokaa
- Asubuhi huitana - Mikono wakapeyana
Ikawa ni kulizana - Kina wakiomboleya
- Upande wa Makombeni - Na Mkoano mjini
Mimi huko nu mgeni - Nilikwenda kutembeya
- Lakini niliuliza - Watu wakanieleza
Karafuu zinaoza - Zahinda kuondolewa
- Ziliharibika kweli - Kwa mvuwa kuwa thakili
Uwanjani kama vuli - Ukipita wachopeya
- Ama dalali Kichungi - Epoteza mali nyingi
Kataa sasa haringi - Maringo yanamwishiya
- Yalimwishiya maringo - Akaingiya kinyongo
Akawa hana mpango - Wala hana pa kwemndeya
- Akenda akinadisha - Wengi aliwakodisha
Mavuno yalipokwisha - Fedha hakurudishiwa
- Ikamfika hilaki - Nyumbani hakukaliki
Probeti hakwendeki - Akhofu kulaumiwa
- Sababu mali si yake - Epewa yeye ashike
Akusanye apeleke - Probeti angojewa
- Hayo ndiyo matatizo - Kishungi pesa hanazo
Yakamwishiya mawazo - Hana pa kuzizumbuwa
- Lakini efanya rai - Ya kupita akidai
Akawa kwake hakai - Kutwa kiguu na njiya
- Wengine walimlipa - Wengine hawakuumpa
Akabakiya kurapa - Roho haikutuliya
- Na mwisho alitamka - Mwaka huu kwa hakika
Khasara inanifika - Nisiyoitazamiya
- Hii ni bakhti yangu - Kunipiga ulimwengu
Nnamshukuru Mungu - Ndiyo hali ya duniya
- Kishungi esema hayo - Wala furaha hanayo
Akanyamaza kiliyo - Lakini akiuguwa
- Na kila mwenye shambaye - Hajitambuwi haliye
Hapotei asemaye - Kuwa nataka semewa
- Za chini hazikauki - Za juu hazichumiki
Mvuwa hainyamaziki - Mali yazidi poteya
- Waliyo na mali yao - Walikosa hata nguo
Khasara ya mwaka huo - Ndivyo nilivyokwambiya
- Khasara kubwa ajabu - Wengi iliyo wasibu
Mali haina hisabu - Nyingi iliyopoyteya
- Kuna wapikao uji - Khasara zao sitaji
Lakini binti Haji - Huyo aliteketeya
- Akiupika mseto - Na uji juu ya moto
Jioni hapana pato - Uji hewenunuliwa
- Na asokuwa na kazi - Akichoma maandazi
Kukaa bure hawezi - Si mtu wa kutuliya
- Kukicha alfajiri - Kila chakula tayari
Angojeya washtiri - Bado hawajatokeya
- Hapana mtu ajaye - Wala amuulizaye
Bi Haji na khasaraye - Hana wa kumpokeya
- Bi Haji hapumziki - Huwakaanga samaki
Atembeza hawatoki - Hayupo wa kununuwa
- Mbugwani Bi Mafunda - Biashara yemshinda
Asijuwe la kutenda - Fikra zikamwishiya
- Bibi Asha na Salima - Maneno waliyosema
Sasa ni bora kuhama - Hapana la kukaliya
- Tuwaarifu wenzetu - Tuhame turudi kwetu
Hapa hatupati kitu - Biashara yapoteya
- Salima akatamka - Yapendeza kuondoka
Mwaka huu kwa hakika - Tumeshaharibikiwa
- Sasa ni bora tuhame - Twende kwetu tukalime
Asemaye na aseme - Kusema ndiyo duniya
- Hakika mabibi hao - Ni kubwa khasara yao
Lukudi ya kwenda kwao - Ikawa kudirikiwa
- Ni hayo yaliyopita - Hapana aliyopata
Na wengine wakajuta - Majuto yasiyofaa
- Nami ndiyo haandika - Bukuni nikayaweka
Yasijesahaulika - Iwe yakikumbukiwa
- Mwisho wangu wa utenzi - Kwenda usoni siwezi
Zatosha baiti hizi - Kiasi cha kuongeya
- Utenzi natiya tamma - Kuandika nasimama
Nijuwayo nishasema - Mengine sikuyajuwa
- Sasa nawambiya jina - Ingawa najulikana
Uzuri kuambiyana - Ili mukanitambuwa
- Khamisi jina ni langu - Ni jina la baba yangu
Nasoro ni baba yangu - Piki nilipozaliwa
Sk. Khamis bin Nassor Al Nabhani [
1962].
Limeletwa na Saleh Barkey