|
|
KISA CHA MIRAJI
- Nanza kunudhumu kwa isimu ya karima
Mola Mtukufu wa milele mwenye dawama
Zimewaenea watu wote zake neema
Sala na salamu kwa mtume zende daima.
- Na jamaa zake na sahaba tuwasalie
Tupate ya kheri miongoni mwao tungie
Siku ya kiama wasimame watuombee
Tupate Nusura, Siku nzito ya jahanama.
- Haya yanatosha sendi mno kwa dibaji
Kwani nina mambo kuyataja nahitaji
Ni hadithi njema ya usiku wa Miraji
Ya Mtume wetu kupandishwa katika sama
- Ilipowadia Mola wetu kadhihirisha
Cheo cha Mtume Jibirilu alimshusha
Akaja nyumbani kwa Mtume akamwamsha
“Ondoka silale,Mola wako akwita hima”.
- Alipoamka Jibirilu alipasua
Kifua cha Tumwa taka zote akaondoa
Kisha kikajazwa kila mema kile kifua
Akaja Buraqi mbele yao akasimama.
- Jibirilu Kasema“ mola wako akusalimu
Tumekuja kwita twende nawe kwake Karimu
“Upande Buraki kwa heshima na taadhimu”
Buraki ni nyama ametoka katika sama.
- Wakenda kwa mbio wakafika kwenye Madina
Jibirilu kamba “shuka hapa mwombe Rabana
“Sali kwa vizuri rakaati mbili za Sunna
“Kisha umsifu Mola wako kwa sifa njema”.
- Wakashika njia wakafika Jabali Turi
Jibirilu kasema“Sali hapa upate kheri
Hapa ni mahali Maulana Mola Qahari
Amemsemeza Nabi Musa maneno mema”.
- Wakafululiza wakafika Beti Lahamu
alipozaliwa Nabi Isa wa Mariyamu
Jibirulu kasema“Sali hapa penye Makamu
Muombe Rabuka hapa pia mahali pema”.
- Na katika kwenda wakaona jinni njiani
na kijinga chake amwunguze Nabi Amini
Jibrilu kasema Soma Dua omba manani
Nabi akaomba , Mola wake akakizima
- Baada ya hayo mambo mengi wakayaona
Wakaona watu wakipanda mara huvuna
Jibirilu kasema“Watu hao mujahidina
Wendao jihadi wajaziwa mema daima.
- Baada kidogo ilinuka harufu nzuri
Jibirilu kamba “ ni harufu ya mwenye kheri
Msusi wa nywele akisuka watu vizuri
Binti Firauni akisuka kwake daima”.
- Alipomchana na shanuo kumwanguka
Msusi kasema “Fiarauni amepotoka
Binti Firauni aliinuka kaghadhibika
“Takwenda mwambia utakiona chako kiyama”.
- Khabari zikenda Firauni akasikia
Akawakusanya ,mke ,mume,na wana pia
Ndani ya mafuta yenye moto akawatia
Ni kaburi lao lifukalo harufu njema.
- Na katika kwenda waliona watu wazima
Zinapondaponda vichwa vyao nyundo za chuma
Jibirilu kamba “Wasosali sala daima
Ndio jaza yao wajaziwa kesho kiyama”.
- Kisha wakanenda wakaona wasio wema
Wanalishwa moto , mishubiri na michongoma
Wapigishwa nyinda utasema wana wa kima
Jibirilu kamba “Wasotoa zaka,nasema”.
- Baada ya hapa wakaona walao nyama
Wanalazimishwa kula mbovu waache njema
Jibirilu kamba “ni wazinzi wasiokoma
“Wake na mume wazinio dom-daima”.
- Kisha wakaemda wakaona mto wa damu
Mna watu ndani wogelea wakila sumu
Jibirilu kamba “watu hao wala haramu
Mali yao yote kwa haramu wameyachuma”.
- Na katika kwenda waliona watu wabaya
wakikatwa ndimi kwa mikasi zinarejeya
Ndio hali yao wakikatwa ndimi humeya
Jibirilu kamba “wazuwao wanaposema”.
- Kisha wakanenda wakaona watu njiani
waparura nyuso kwa makucha wataabani
jibirilu kamba “wasemao watu penbeni
watafufuliwa nyuso zao hazina nyama.
- Na katika kwenda walikuta mitume pia
akawamkia kwa salamu wakitia
kasha akafika nyumba kubwa akaingia
Bet Mukadasi nyumba njema yenye heshima.
- Walipowasili msikiti wenye baraka
Waliona nuru pande mbili kimemutuka
Nuru ya ya kaburi la daudi alotukuka
Na ya pili nuru ya kaburi la Mariyamu.
- Wakaingia ndani wakasali rakaateni
kaona mitume imejaa msikitini
Hapo Jibirilu kainuka akaadhini
Akakimu sala ,hawajui yupi Imama.
- Jibirilu kamba “Waambiwa utakadamu
Na mitume iwe nyuma yako ,wewe imamu
Ukubwa ni wako na heshima na taadhimu
Kesho utakuwa muombezi wa wote uma”.
- Baada ya kusali kila mtu alishukuru
Neema za Mungu Mola wake Mola Ghafuru
Na kila mmoja nema yake akadhukuru
Neema za Tumwa zikazidi zao neema .
- Kisha ikashuka Miiraji-ngazi thamini
Imepabwa fedha na dhahabu na marijani
Akapanda Tumwa Muhammadi hata mbinguni
Wakapiga hodi waingie katiak sama ..
- Wakamba “ni nani mwenye nuru yenee sama’
Jibirilu kamba “ Muombezi wa wote umma
Akafunguliwa kwa haraka na hima hima
Wakampokea kwa heshima na taadhima .
- Tumwa kamuwona baba yetu Tumw Adamu
Akamwamkia maamkio ya kiislmu
Kamba : Marhaba ,mepokea yako salamu
“Ndiwe mwenye ,mbele na mitume yote i-nyuma”.
- Kisha wakakwea wakafika wingu wa pili
Kabisha mlango wakaingia kama awali
Kmwona Isa na Yahya wote wawili
Sura zao moja kama ndugu baba na mama .
- Na wingu wa tatu wakaingia kwa taadhima
Nabii yusufu wakamwona na sura njema
Akanza salamu Tumwa wetu, ndiyo hishima
Akakaribishwa akawekwa mahala pema.
- Kisha wakafika wingu wane wakamwona
Nabii Idrisa na watano Nabii Haruna
Uwingu wa sita Nabii Musa bini-Mrana
Wingu wa saba Burahimu mwenye adhama .
- Kisha wakakwea wakaona hapo walipo
Beti Maamuri imekaa chini ya pepo
Wakangia ndani wakaona mahali hapo
Safu sabiini za malaika –viumbe vyema.
- Kisha akataka kuonyeshwa moto mkali
kaona vituko na adhabu ilo kamili
Moto unawake kuni zake in majabali
Na watu wabaya waasio Mola daima .
- Kisha wakafika kwenye pepo nzuri sana
Wakaona mambo hapanaye aliyeona
Wala myawaza kwa moyoni kamwe hakuna
Wala msikia mambo hayo akayasema .
- Baada ya hapa akapewa aliopewa
Mambo matukufu mfanowe hutaujuwa
Kapewa na sala khamsini akachukuwa
Yeye na umati wake wote wapate mema .
- Alipomwendea Nabi Musa alimwambia
“Sala khamsini kila siku zina udhia
Bora urejee Mola wako kwa kuombea
Awapunguzie Mola wetu ana rehema” .
- Tumwa karejea kumwomba Mola Karima
Anawaomba takhfifu wapate uma
Akapunguziwa na Molawe mwenye rehema
Zikawa ni tano- natusali basi kwa hima .
- Kisha wakashuka na usiku wakawasili
Beti Muqadasi nyumba njema tangu asili
Ikawa Buraki kasimama kama awali
Tumwa kampanda kwa isimu yake karima.
- Katika kwenenda wakaona wengi ngamia
Watokao Shamu mali mengi wamepakia
Walipomuona Burakiye walikimbia
Moja kavunjika goti lake kwa kwenda hima .
- Kisha wakanenda wakafika Makka na kiza
Hakujacha vyema akakaa Tumwa kiwaza
Kujuwa yakini Makureshi watamcheza
Shere kubwa mno wamwone mwongo daima .
- Katika kuwaza aliona tumwa Rasuli
Mbele yake asi maluuni Abu Jahali
Akamwuliza kwa dhihaka na kwa kejeli
“Ewe Muhammadi ! nakuona uso kunama .
- “Una jambo gani kubwa mno la kughairi
Ukabadili uso wako usinawiri
Hunambii nami nikajua yako khabari
Siyo hali yako tujuwayo kwako daima”
- Akamba “Naam takwambia yangu khabari
Usiku wa leo nalikwenda mbali safari
Beti Mukadasi nikafika nyumba ya kheri
Kisha nikapanda baadae katika sama”.
- Akawakusanya maluuni Abu Jahali
Makureshi waje wawe naye wakinakili
Alipoweleza kwa utungo wasikubali
Pakawa vicheko na dhihaka na kumzoma .
- Kureshi wakamba “tusifiye Beti Kudusi
Kama umekwenda hutashindwa tukidadisi
Ama mbingu saba usemazo hatuziisi
Kwani katukwenda hatujui zake alama” .
- Moyo wake Tumwa ukaingia nyingi shughuli
Mambo ya usiku asiweze kuyafasili
Mola kaamuru Jibrilu kuinakili
Beti Mukadasi mbele ya yake kuitazama .
- Akawasifia sifa zake wakazikiri
Kapima kwa nyayo na dhiraa hata shubiri
Na Abubakari akisema “Ewe Bashiri
Ndizo sifa zake umesibu zote alama”.
- Wale Makureshi wakanena “Ewe Amini
Ndizo sifa zake umekwisha kuzibaini
Tuna watu wetu safarini Bani Fulani
Twambie na siku ya yao kukoma” .
- Kamba “Watu wenu karibuni watatokeya
Ijumatano ndiyo siku yao yakuya”
Ilipowadia siku hiyo walingojea
Wakatoka nje majiani wakasimama .
- Wakawatokea watu wao wote idadi
Jua halijachwa ikatimu yake miadi
Wakamba “Ni kweli alosema hatuyarudi
Lakini mchawi , anafanya haya daima .
- “Ingawa ni kweli sifa zote alofasili
Ila ni mchawi kama haya kwake kalili
Kwani anapenda dini yetu kuibatili
Hatumfuwati tukaacha wetu sanamu” .
- Basi nimekwisha Miiraji kuinudhumu
Kwa Himdi yake Maulana Mola Karimu
Sala na Salamu na Baraka na Taadhimu
Zimwendee Tumwa na Ali na Sote uma .
- Rabi turehemu kwa rehema yako Azizi
Turehemu sote wasomao na wasikizi
Sote turehemu kwa Baraka ya Muombezi
Siku ya Kiama utokowe na Jahanama .
Mtungaji: Kadhi Sheikh Abdulla Saleh Farsi
Mosomaji: Sheikh Abdallah A. Bakathir
November 1963
Mfungo Tisa ,1383 .
Umeletwa: Ahmed Rashid
|