|
|
Madaraka Yana Mwisho !
Date: 06 January, 2007
- Kwa jina lake manane, Mola mwenye upendo,
Asokua na khiyana, sifa zake ni mrundo,
Mwana Adam ni dhaifu, usijifanye komando,
Madaraka yana mwisho, usiwe mwenye kiburi.
- Salmin ulitamba, kwamba wewe ni kombando,
Sasa muda umekwisha, umebaki ni kondoo,
Umekuwa kama kuku, aloshikwa na mdondo,
Madaraka yana mwisho, usiwe mwenye kiburi.
- Zanzibar kama yako, ulishika kwa kishindo,
Wenzio unawatesa, gerezani kwa marundo,
Watu tulikirahika, kwa maneno ya uvundo,
Madaraka yana mwisho, usiwe mwenye kiburi.
- Pemba walikukataa, mavi ukanya mrundo,
Maji ukayachafua, watu wakenda kando,
Ukajifanya kifaru, hakuna tena upendo,
Madaraka yana mwisho, usiwe mwenye kiburi.
- Ukajifanya kafiri, Mungu kumuweka kando,
Sasa leo kiko wapi, umechezeshwa msondo,
Na bado kesho Akhera, utakipata kipondo,
Madaraka yana mwisho, usiwe mwenye kiburi.
- Madhila uliyofanya, wewe ukaona bado,
Muda wataka ongeza, utufanyie kishindo,
CCM namba moja, wakakupiga kwa nyundo,
Madaraka yana mwisho, usiwe mwenye kiburi.
- Ndugu zako wawatesa, kuwapiga kwa upondo,
Sheria ukaipinda, kama nguo ya upindo,
Wenzio wakakupamba, kwamba wewe ni komando,
Madaraka yana mwisho, usiwe mwenye kiburi.
- Sasa ujirekebishe unavyokwenda si mwendo,
Mimi ninae kuonya, ninaitwa Mwela Bondo,
Sikama nakusimanga, ninaondoa mfundo,
Madaraka yana mwisho, usiwe mwenye kiburi.
Limeletwa na Abdalla Sani
Mtungaji : Mwela Bondo (Kipupwe), Makumbusho, Dar es Salaam
|