|
|
Mja!
- Mja hutashiba kula, Waona ladha daima
Mja wakonga na ila, Hujui bora khatima
Mja hiyo ni ghafala, Na kukutaza si vyema
Ulipofika simama, Urudi kwa Mola wako
- Urudi kwa Mola wako, Ghafuru ndio Rahima
Dhiki na taabu yako, La'ala ndio salama
Nuwiya kwa dhati yako, Toba isiyo na dhima
Ulipofika simama, Urudi kwa Mola wako
- Mja usihadaike, Sikiya yangu kalima
Bilisi asikushike, Ukasahau Kiyama
Fahamu safawa yake, Siku hiyo ni hasama
Ulipofika simama, Urudi kwa Mola wako
- Mja fikiri mauti, Sikuhadae uzima
KYAM waliofaiti, Mashujaa hapo zama
Wasikiya huwakuti, Na hio ndio salama
Ulipofika simama, Urudi kwa Mola wako
- Mja khofu siku hiyo, 'L-hashiri wannadama
Ni siku ya makamiyo, Kufufuliwa 'aama
Ni wewe na amaliyo, Hiyo siku ya zahama
Ulipofika simama, Urudi kwa Mola wako
- Mja ladha ya duniya, Haitakwisha daima
Mja ufikiri njiya, Sirata 'l-mustaqima
Njiya inayo baliya, Ndani yake jahannama
Ulipofika simama, Urudi kwa Mola wako
- Ewe mja tafakari, Inuka ukiinama
Wenda ndani ya kaburi, Hapana baba na mama
Mja khofu munkari, Na fimbo zake za chuma
Ulipofika simama, Urudi kwa Mola wako
- Mja mkhofu Jalali, Kwa siku ya mahakama
Siku ya Rabi kujali, Wa yuhyi 'l-idhama
Siku hiyo ya kitali, Rabi asiyo huruma
Ulipofika simama, Urudi kwa Mola wako
- Mja natia tamati, Yangu nasaha nakoma
Mja duniya sukuti, Quruani kunasoma
Haihati haihati, Mauti kwako lazima
Ulipofika simama, Urudi kwa Mola wako
Khamis Nassor Al-Nabhany
|