.

Welcome to Zanzinet Swahili Poems

Where Swahili matters!

UTENZI WA KISA CHA NABII AYYUB (A.S.)

 

Related links

UTENZI WA KISA CHA NABII AYYUB (A.S.)

Date: 7 September, 2003

  1. Bismillahi Qadimu, Arrahmani Rahimu, Mwenye enzi ya kudumu, Muumba ndiwe Jalia

  2. Uloumba ulimwengu, Arshi juu ya mbingu, Ukapanga na mafungu, Waja kuwamiminia

  3. Aridhi ukatandika, Ziumbe ukawaweka, Hukuwa na mshirika, Ni kazi yako Moliwa

  4. Ukanyesha na mvua, Ukalitowa na jua, Miti nayo ikamea, Ikanawiri dunia

  5. Hakuna mtenda kazi, Ila ni wewe muyuzi, Mwenye mkubwa uyuzi, Ndiwe wa kutegemewa

  6. Ukaumba majabali, Makubwa yaso mithali, Ndani yake muna mali, Na aridhi kuziwiya

  7. Ukakusnaya milima, Ya mitanga ilokwima, Meupe ukiiona, Na raha kuyangalia

  8. Yote ni kazi ya Mola, Asokula asolala, Na kwake huna muhula, Popote utarejea

  9. Katengeza kwa udongo, Na tope zenye mavundo, Mwanadamu lake umbo, Quruani yatwambia

  10. Ukayaweka mauti, Kwetu sisi ni sharuti, Huja pasi na wakati, Siku zikisikilia

  11. Tahadhari mwanadamu, Yataka ujifahamu, Siku zikishakutimu, Budi huna nakwambia

  12. Ewe mja usojali, Kumbuka huna mahali, Mauti hayako mbali, Popote hukungilia

  13. . Ghafula hukukabili, Mauti hayako mbali, Na jina likabadili, Wendo wakakulilia

  14. Nakuomba ndugu yangu, Tafadhali nisikia, Roho si ya ulimwengu, Hakuna cha kubakia

  15. Wawapi wanazuoni, Matajiri masikini, Na wenye nguvu wendani, Kama hawakuzaliwa

  16. Wako wapi wenye nguvu, Akili na uwerevu, Hawakuwa watukivu, Leo wameshika ndia

  17. Mamako alihajali, Mimba yako kahimili, Uzito kama jabali, Hakushindwa katukuwa

  18. Kwa kite kaitukuwa, Henenda akijishuwa, Na mangi akiongowa, Kwa kazi yake Karima

  19. Ukazawa mwanadama, Huna mbele wala nyuma, Kakuyeya wako mama, Kwa uwezo wa Karima

  20. Ulimwengu si makazi, Kwa kila alomuyuzi, Ni mapito ya wemuzi, Ya kwenenda mui mwema

  21. Baada haya kunena, Nina kiswa waungwana, Cha Ayubu tumwa mwema, Nimependa kukitowa

  22. Nimependa kufasiri, Niwape zake khabari, Nimeona ni uzuri, Mupate kumuelewa

  23. Babake alitajiri, Alina mali kathiri, Alihai kadhukuri, Mali nda mwane nabiya

  24. Alipokufa babake, Kayashika mali yake, Ayyubu ndie pweke, Mali kaikusanyia

  25. Alitajiri ajabu, Wa majumba na dhahabu, Na wana wenye adabu, Mola memruzukia,

  26. Alikuwa na hekima, Za fahamu ya ilima, Na akili zilo tama, Yote kampa Jalia

  27. Alikuwa mahabubu, Kwa watu na maswahibu, Akipendeza Ayubu, Kwa watu ni maridhia

  28. Uli na nguvu muili, Na sura zake jamali, Na biashara amali, Ndio alokifanyia

  29. Kamuoa mwana mwema, Rahama binti Fartima, Babu yake nitasema, Ndie Yusufu nabiya

  30. Ayyubu alioa, Wake watatu sikia, Wawili wakakimbia, Rahama akabakia

  31. Riwaya ilopokewa, Watoto walozaliwa, Ni kumi kuongezewa, na wanane kutimia

  32. Kawaeya wake zake, Pamoja na wana wake, Hawakumuata pweke, Kwa raha na mazowea

  33. Mkubwa mtoto wake, Kawalika ndugu zake, Harimala jina lake, Kwake akawatukua

  34. Kawapikia chakula, Ndugu yao Harimala, Haukupita muhula, Balaa zikawangia

  35. Balaa zikawafika, Kwa msiba ulotuka, Ya ukuta kuanguka, Wanawe wakajifia

  36. Mali yakataharika, Mno akafilisika, Yali yakipuputuka, Kila siku kupungua

  37. Ali na mengi majumba, bustani na mashamba, Na wanyama wa kutunga, Wote hawakubakia

  38. Maradhi yalimshika, Siku nyingi na miaka, Hakuwa akipunguka. Ila kuzidi nabiya

  39. Maradhi ya kiajabu, Yalompata Ayubu, Hakusaza matibabu, Na wanaojua dawa

  40. Mabombwe yalikitoka, Na ngozi ikatanika, Mkewe akashutuka, Kamba unani nabiya

  41. Muili hukushanuka, Na mabombwe hukutoka, Nawe umebadilika, Na wazidi kwendelea

  42. Hata naona ajabu, Yalonipata muhibu, Ni kazi yake Wahabu, Ilahi yamueleya

  43. Kamba wewe hufahama, Yalonipata Rahama, Mitihani ya Karima, Nami taisubiria

  44. Maradhi ya miujiza, Ya ngozi yake kuoza, Wadudu wakitapuza, Muilini kwa nabiya

  45. Hakuona la sahali, Ugonjwa kauhimili, Mkubwa ulo thaqili, Mola aloqadiria

  46. Rahama kamuhimili, Kenda nae huko mbali, Nti yenye majabali, Kibanda kamjengea

  47. Kenda nae taratibu, Kamueka kwa adabu, Hakusikia dharubu, Za mikukuto ya ndia

  48. Kali chakula hakuna, Wala maji ya kunwa, Ndaa ilipowabana, Rahama hakungojea

  49. Kateremka mjini, Rahama katumaini, Tapata mwema mwendani, Riziki kumpatia

  50. Watu walipomuona, Kwa umoya wakanena, Ndoo kwetu wata bwana, Shere wakimtezea

  51. Rahama hakukubali, Waloyasema rijali, Kaomba Mola Jalali, Amlinde na mabaya

  52. Ayyubu akamwita, Kamba wewe huniata, Ni gani wenda tafuta, Nambiya nipate juwa

  53. Kamba wewe mume wangu, Nakuapia kwa Mungu, Sitakutupa bwanangu, Wala sibadili nia

  54. Kanena na moyo wake, Ni wapi mimi nifike, Kakumbuka mwanamke, Upesi akamwendea

  55. Mlango akaubisha, Akataka kukopesha, Nikipata tarejesha, Kanena wangu nabiya

  56. Mwanamke kwa umbeja, Kishipa kikampija, Akanena kwani ngoja, Lilokueta nambiya

  57. Hukuya nyumbani kwangu, Ila kunipa matungu, Akuone mume wangu, Apate kukuridhia

  58. Rahama akamjibu, Mwanamke kwa ghadhabu, Nina wangu Ayyubu, Nilopewa na Jaliya

  59. Mimi sitokukiridhi, Kwani mimi meniudhi, Una kitu chenye hadhi, Ukitaka niatia

  60. Ali na nyele safira, Rahama zalikin'gara, Mwanamke kwa hasira, Makasi kamuetea

  61. Kazikata nyee zake, Akampa mwanamke, Kabeba mikate yake, Mumewe kampekea

  62. Rahama akadhahabu, Akafika kwa Ayubu, Mumewe kataghadhabu, Maneno kimwelezea

  63. Mumewe likamkera, Kutoa nyee safira, Zilikua nyee bora, Ni ndefu zikin'garia

  64. Akamwapia Jalali, Mbee za wake rasuli, Si haramu ni halali, Chakula nilokwetea

  65. Mla wewe mume wangu, Nimeuza nyee zangu, Nimekwapia kwa Mungu, Maovu kukutendea

  66. Kanena tahakikisha, Na hadi taipitisha, Mboko mia takutwesha, Ninapopata afiya

  67. Kiwa na afiya yangu, Tachunguza mke wangu, Ili nilipe matungu, Na kufuata sharia

  68. Rahama akamjibu, Kwa sitaha na adabu, Kwamba uovu Ayubu, Siwezi kukufanyia

  69. Rahama ayatamke, Amwambie mume wake, Amuombe Mola wake, Mateso kumwondolea

  70. Kamwambia mke wangu, Naona haya kwa Mungu, Mestarehe na wanangu, Ashara wa thamania

  71. Tasubiri Mola wangu, Na balaa za matungu, Maadamu moyo wangu, Na ulimi mebakia

  72. Na ulimi nibakishe, Ilahi nikukumbuke, Dudu usimuoneshe, Ulimini kuningia

  73. Walitoka kwa muili, Wadudu wote wawili, Tiati wamekabili, Ayyubu changaliya

  74. Wa kwanza katumbukia, Mtoni akaingia, Mai yakamtukua, Ayyubu kionea

  75. Wa pili kapanda bara, Kwenye jangwa la sahara, Akawa mnyama bora, Asali yake ni dawa

  76. Hapohapo Jibrili, Kwa Ayubu kawasili, Yali mikono miwili, Kudhumani metukua

  77. Metukua kudhumani, Metoka nayo peponi, Amepewa na Manani, Ayyubu kumwetea

  78. Ayubu katakauli, Kamwambia Jibirili, Menikumbuka Jalali, Kunipa yangu afiya

  79. Jibirili kamjibu, Menipa Mola Wahabu, Dawa yako kukutibu, Matunda ya jannatia

  80. Akamwambia simama, Ayyubu tumwa mwema, Kwa amri ya Karima, Inshalla utatulia

  81. Mimi nimetumwa kwako, Nipoze ugonjwa wako, Piga tini guu lako, La upande wa kulia

  82. Yakatoka maji moto, Meupe yalo mazito, Akapowa tumwa wetu, Maradhi yakapungua

  83. Kamwambia Jibirili, Upige nao wa pili, Wa kushoto sikuvuli, Maji yakaitokea

  84. Mabaridi ya kutosha, Jibrili kamnwesha, Mola akamrejesha, Kama zamani nabiya

  85. Maradhi yake kapona, Tumwa akawa mzima, Akarudi kama zama, Kwa uwezo wa Jaliya

  86. Ayyubu akanawiri, Kan'gara kama qamari, Ukarudi utajiri, Wake na watoto pia

  87. Riwa nyengine hunena, Alibaki na Rahima, Kazaa wangine wana, Na mali yakarejea

  88. Haya yaliyomsibu, Kumpata Ayyubu, Mitihani ya Wahabu, Nae kaisubiria

  89. Mola anatufundisha, Kutaka kutuonesha, Maana ukiondeshwa, Sibabaike sikia

  90. Uyatie akilini, Usubiri kwa Manani, Ndake Mola mitihani, Quruani yatwambia

Mtungaji: Muhammad Abdulla Shatry wa Lamu.

Umeletwa na Saleh Barkey

 

  About Us | Zanzinet Home | Contact Us | ©2004 Zanzinet