.

Welcome to Zanzinet Swahili Poems

Where Swahili matters!

UTENZI WA KISA CHA NABII YUSUF (A.S.)

 

Related links

UTENZI WA KISA CHA NABII YUSUF (A.S.)

Date: 5 September , 2003

  1. Bisimilahi Kahari, Ya Rabi Mola Jabari, Mmoja uso akhiri, Wala mwanzo kuanzia
  2. Naanza kwa lako jina, Mola wetu Subuhana, Mtukufu wetu Bwana, Wa pili asotokea
  3. Twamsalia kaumu, Sote ndugu Isilamu, Mtume Bani Hashimu, Sayyidil Arabia
  4. Sote Rabi Ya Rahimu, Twamsalia Hashimu, Na tunu nyingi salamu, Twamtakia Nabia
  5. Nina kisa maarufu, Cha tumwa wake Latifu, Mtume mwema Yusufu, Wao Isirailia
  6. Mtume wake Wahabu, Yusufu tumwa Habibu, Baba yake Yaakubu, Jinale tawatajia
  7. Mzazi wake wa pili, Jinale ni kama hili, Aitwa bibi Rahili, Mtukufu wa muruwa
  8. Yusufu ndie Rasuli, Aloletwa na Jalali, Kwa bani Isiraili, Kaumu isosikia
  9. Nduguze kuwahisabu, Kwa majina ni taabu, Samahani masahibu, Idadi tawatajia
  10. Ana kumi wa awali, Kwa baba na mama mbali, Na mdogo ni Rakili, Kwa baba na mama pia
  11. Walikuwa majabari, Wasiogopa shari, Shujaa walo hodari, Dhiki ikiwafikia
  12. Alipokwisha kuzawa, Na ndugu wakachukiwa, Wamuhasidi na ngowa, Maradhi yalokomaa
  13. Sababu yeye kwa kweli, Alikua na jamali, Uzuri wake rasuli, Akipendeza Nabia
  14. Ni mrembo mtulivu, Mwenye busara mwerevu, Na mwilini hana kovu, Uzuri umezidia
  15. Yusufu alipokaza, Kwa wazazi kupendeza, Ndugu yakawachukiza, Mabaya kukusudia
  16. Ndugu walifanya wivu, Na kila la uwerevu, Wamtendee uovu, Kumwangamiza dunia
  17. Siku moja ya utoto, Amelala hako mato, Yusufu kaota ndoto, Ajabu nawaambia
  18. Ndoto hiyo ya kioja, Jua na mwezi pamoja, Na nyota kumi na moja, Vyote kumsujudia
  19. Muda alipogutuka, Hapo alipoamka, Alikimbia haraka, Kwa baba kumwelezea
  20. Baba kwake ujuzi, Akaifahamu wazi, Ndoto ya jua na mwezi, Na nyota kumi na moya
  21. Na baba asinyamaze, Ndipo amsisitize, Mwanangu siwaeleze, Nduguzo nakuusia
  22. Mwanangu stahamili, Siwaambie asili, Yusufu usikubali, Siri ya ndoto zuwia
  23. Mungu atakukhitari, Akufunze tahariri, Ya ndoto na ya khabari, Waja wasizozijua
  24. Hapo ndipo auladi, Hao kumi mahasidi, Ikashtadi hasadi, Wakawa na jicho baya
  25. Hasadi ya jicho ovu, Kwa kumuonea wivu, Ili wamtenze nguvu, Yusufu mmwema nabia
  26. Ndio waliokutana, Wote ashara vijana, Wasijizuie tena, Moyoni kuvumilia
  27. Faragha walionana, Wote kushauriana, Mwisho wakasikizana, Maovu kuazimia
  28. Wakatoka taratibu, Vijana hao kidhabu, Wakenda kwa Yaakubu, Baba yao kumwambia
  29. Wakafika pasi khofu, Maneno kumuarifu, Kwa kumtaka Yusufu, Ruhusa kumuombea
  30. Wamtaka ndugu yao, Yusufu mdogo wao, Ili asafiri nao, Huko wanakokwendea
  31. Hila waliyoisema, Kwa wao mtu mzima, Ni Yusufu kuandama, Kwenda kucheza pamoya
  32. Hapo baba kashangaa, Na kwanza akakataa, Akajua ni hadaa, Wana walomwelezea
  33. Maana alitambua, Hila yao kuijua, Yusufu wamchukua, Lakini hatarejea
  34. Mola aliyoandika, Ni uongo kufutika, Ni lazima kutendeka, Kwani yote yamwelea
  35. Na baba kwa takilifu, Ya wanawe wapotofu, Moyo ukafanya khofu, Lakini kavumilia
  36. Ikawa hapana budi, Baba yao kuburudi, Akamtoa fuadi, Yusufu kuwaachia
  37. Vijana wakaondoka, Na mji wakautoka, Pamoja na muhibbuka, Yusufu tumwa Jalia
  38. Wakawa wasafarini, Wapotelea porini, Na huku wamachungani, Walisha katika njia
  39. Wakawasili makini, Kando ya mji njiani, Kwenye mji Dausani, Mji walioingia
  40. Kufikia kisimani, Mmoja wa ikhiwani, Ambae ni wa mwanzoni, Umri alozidia
  41. Akalitoa shauri, Kuwapa ndugu khabari, Akasema jambo zuri, Yusufu kumtendea
  42. Mimi katu sikubali, Tulivyowaza awali, Ni lazima liwe hili, Jengine sitoridhia
  43. Yusufu tusimuweni, Sote na tumshikeni, Tumtupe kisimani, Haya kwake ni kifaya
  44. Ikawa budi hawana, Asili kutoshindana, Mkubwa aloyasema, Wadogo wakatikiya
  45. Hapo tena kwa upesi, Wakamvua libasi, Ambayo ndio khalisi, Yusufu alovalia
  46. Na kisha wakamshika, Wakamtupa haraka, Kwenye kisima cha nyoka, Kirefu chenye udhia
  47. Kwa uwezo wa Rabuka, Hata si robo dakika, Jibrili akashuka, Ajabu ilotokea
  48. Kufumba na kufumbua, Jibrili keshatua, Yusufu kumuokoa, Kabla hajaumia
  49. Jibrili kamnyaka, Kabla chini kufika, Taratibu kamuweka, Mahali pema nabiya
  50. Baada ya kutendeka, Kisa hiki kufanyika, Nduguze wakatoroka, Wakanza kukimbia
  51. Wenda wakifurahika, Waongea wakicheka, Wakajua kwa hakika, Yusufu keshajifia
  52. Kumbe wamehadaika, Na bure kuadhirika, Na Yusufu hana shaka, Bukheri kajikalia
  53. Hata kwa muda saghiri, Wakazuka wasafiri, Wenda mji wa Misiri, Wa katika yao njia
  54. Ulikua msafara, Ulotimia imara, Wafanyaji biashara, Wasafiri wa ngamia
  55. Hapo bila ya kungoja, Maji ndio yao haja, Wakamtuma mmoja, Maji kwenda watekea
  56. Ndoo ikashika papo, Yusufu hapo alipo, Akashika papo hapo, Kamba ilomlekea
  57. Kamba alipoipata, Akawa yuwaivuta, Na aliyeikamata, Uoga ukamwingia
  58. Uoga na taharuki, Kwa kamba yake kusaki, Ndoo haitaharuki, Yusufu ameigwia
  59. Katizama kutafiti, Kujua kilo tiati, Mara ikaja sauti, Kisimani kutokea
  60. Kwa nguvu zake Kahari, Ndipo tena wasafiri, Hapo pasi kusubiri, Kutafuta kila ndia
  61. Ikawa ni pata shika, Waume kushughulika, Kamba zimekusanyika, Kisimani zangojea
  62. Yusufu kwenye kisima, Akatolewa mzima, Ameokoka salama, Kama hakutumbukia
  63. Basi hapo mtukufu, Mtume mwema Yusufu, Akawa yukwenye safu, Na wasafiri pamoya
  64. Wakawa wasafarini, Na Yusufu yukundini, Hadi Misiri mjini, Wendako kuwasilia
  65. Nduguze bila kungoja, Wote kumi kwa umoja, Kutimia yao haja, Walianza kurejea
  66. Wenda bila wasiwasi, Ndiani wakihadisi, Pamoja nayo kamisi, Walomvua nabiya
  67. Na mipango walofanya, Ya hila na kudanganya, Ili kwamba kuwaponya, Baba wanapomwambia
  68. Walingia kwenye kazi, Ya kumkamata mbuzi, Kumchinja kwa ukuzi, Ovu lao kufidia
  69. Wakaipaka libasi, Yusufu yake kamisi, Kwa hiyo damu najisi, Ya mbuzi walomuua
  70. Nyumbani wakawasili, Na baba kumkabili, Na la kwanza ni ajali, Ilowakumba na njia
  71. Wakazidi kutongoa, Na kamisi kuitoa, Ilokua na madoa, Ya damu iloingia
  72. Uongo walouzuwa, Walosema ndugu hawa, Yusufu ameuawa, Kwa mbwa kumrukia
  73. Baba kusikia yale, Ya wanawe muda ule, Na huzuni pale pale, Alianza na kulia
  74. Baba alisema kua, Kwa mwanangu yalokua, Si mbwa alomuua, Wallahi nawaapia
  75. Ni uongo uso shaka, Wa kanzu kutoraruka, Hata tundu kutoboka, Na mwenyewe akalia
  76. Yusufu kumdhulumu, Nawaachia Rahimu, Ndie mwenye kuhukumu, Yote Mola yamwelea
  77. Sasa Yusufu Misiri, Kafika na wasafiri, Maliki akaghairi, Na Yusufu kubakia
  78. Kampeleka makani, Mtume wa Rahamani, Ambapo ni mnadani, Ili kwamba kunadiwa
  79. Na kwa bahati nzuri, Akatokea waziri, Kadawaa kwa uzuri, Aliopewa nabiya
  80. Kamnunua Yusufu, Kwa bei ilo pungufu, Kama mtumwa dhaifu, Asiye na manufaa
  81. Waziri akamtwaa, Yusufu nae kukaa, Kama mwana wa kuzaa, Mahaba yalomwingia
  82. Baadae atamke, Kumwambia mke wake, Zulekha mwana mshike, Mola katujaalia
  83. Waziri bila ya khofu, Akaishi na Yusufu, Asimpe taklifu, Kwa kila lenye udhia
  84. Waziri akamsifu, Kwa wake uaminifu, Akimpa maalufu, Mali kuyasimamia
  85. Sasa hapa tufahamu, Umri aliotimu, Ndiyo apewa ilimu, Na hikima zote pia
  86. Ili kufunzwa khabari, Ya ndoto kuzibashiri, Na akawa ni hodari, Kujua mambo ya ruya
  87. Hata kwa muda fulani, Hapo Zulekha nyumbani, Ndipo yuwaanza zani, Maovu kuazimia
  88. Kila siku yamoyoni, Iwapo mili ya ndani, Yusufu kumtamani, Kumuwazia mabaya
  89. Zulekha yalikithiri, Mapenzi kumuathiri, Na hapo akamghuri, Ibilisi kumwingia
  90. Kukicha azidi huba, Vitendo vya ukahaba, Ili yake matilaba, Yapate kumnyokea
  91. Tangu akipenda siri, Na mwisho asisubiri, Mambo yakawa dhahiri, Kwa huba kumtokea
  92. Na siku hiyo yakini, Waziri hako nyumbani, Mumewe yusafarini, Ndipo aanza udhia
  93. Na ndiyo siku hakika, Zulekha kufedheheka, Na yake kutotendeka, Aliyoyaazimia
  94. . Wakati ulipofika, Hiyo siku aloweka, Zulekha akatamka, Na Yusufu kusikia
  95. Alimwita faraghani, Zulekha kwake chumbani, Amueleze kanuni, Hilo alokusudia
  96. Yusufu akamwitika, Zulekha bibi labeka, Kwa upesi akatoka, Alikoitwa kungia
  97. Hata akifika ndani, Akasubiri makini, Asikize jambo gani, Bibi alilomwitia
  98. Ndipo basi atamke, Huyu baa mwanamke, Amwambie haja yake, Yusufu kumwelezea
  99. Akatamka machafu, Zulekha bila kukhofu, Yusufu kumuarifu, Na nguvu kumtilia
  100. Kasema kwa yake dhati, Zulekha muhasharati, Kila njia kutafiti, Amghilibu rasua
  101. Akazidi ubazazi, Akanena ya upuzi, Kumpa Yusufu wazi, Lake alohitajia
  102. Moyo wako burudika, Niridhi ninalotaka, Na huna la kukufika, Lolote lenye udhia
  103. Yusufu hapo rasuli, Kupata hino kauli, Ilimdhuru akili, Na moyo kushitukia
  104. Moyo ukabadilika, Yusufu kukasirika, Akaanza kumwepuka, Kabisa kutoridhia
  105. Kasema Yusufu katu, Jambo hilo sithubutu, Sitendi yaso na utu, Ya kumuudhi Jalia
  106. Basi ndipo hapo hapo, Zulekha pake alipo, Katambua yaliyopo, Yake kutomnyokea
  107. Akainuka haraka, Ili kutaka mshika, Na Yusufu kaepuka, Zulekha kumkimbia
  108. Zulekha kwa zake kasi, Asimshike khalisi, Ila kugwia qamisi, Muda alimtapiya
  109. Alimshika kwa nyuma, Akaivuta kwa hima, Libasi ikamwandama, Qamisi kuipasua
  110. Ikawa kuchoropoka, Yusufu akaokoka, Na vazi limepasuka, Wakati ajitetea
  111. Zulekha uchungu wake, Kwa Yusufu amwepike, Kapasua nguo zake, Na makucha kujitia
  112. Maana ya hiki kisa, Nguo zake kuzitesa, Ilikua ni siasa, Yusufu kumchongea
  113. Kusudio ni kunena, Arudipo wake bwana, Kumtilia fitina, Yusufu kumzulia
  114. Ghafula mara waziri, Karudi kwenye safari, Akingia yake dari, Mlangoni kufikia
  115. Ndipo kuwahi matata, Mwenyewe akayakuta, Kwa kushuhudia vita, Vya mkewe na nabiya
  116. Moyowe ulishituka, Kwa mambo kubadilika, Si kama alivyotaka, Mbele ya kusafiria
  117. Moyo mengi ukahisi, Khofu ndani ya nafusi, Akazidi wasi wasi, Kuona yalivyokua
  118. Waziri kumtangaza, Zulekha kumueleza, Hebu bibi nieleza, Ni vipi umechukiwa
  119. Niambia tafadhali, Ijapokuwa qalili, Niondowe mushikili, Zulekha bibi nambiya
  120. Na Zulekha kajibu, Kwa nyingi zake ghadhabu. Kumpa mume jawabu, Kisa kilomfikia
  121. Bwana unavyoniona, Wala sina la kunena, Ni mambi ajabu sana , Mtu akiyasikya
  122. Akaanza kwa mpango, Zulekha wake uongo, Kumtakia kifungo, Yusufu pasi na njia
  123. Alimwambia mumewe, Yalonikumba ujuwe, Yote dhamana ni wewe, Bwana ulonitakia
  124. Nimetendewa vituko, Mume wangu nawe huko, Na Yusufu mtu wako, Huyo uloniletea
  125. Ni jambo la kipumbavu, La kunishika kwa nguvu, Anifanye tendo ovu, Nami nikakatalia
  126. Tena akanisumbuwa, Ni lazima lake kuwa, Nguo zangu kupasuwa, Kutaka nigeukia
  127. Na mara bila ajizi, Kijana kasema wazi, Mbele yao kubarizi, Na wote wakasikia
  128. Kwa nguvu zake Karima, Mola mwingi wa rehema, Mwana mchanga kasema, Bila khofu kumwingia
  129. Alinena hivi sasa, Sote tufanye siasa, Tutamjua mkosa, Ni yupi alokosea
  130. Tuliyopo hapa sisi, Tupeleleze tukisi, Tuitazame qamisi, Kwa ilivyonyanyuliwa
  131. Upande ulopasuka, Nguo hio kunyanyuka, Tutamjua hakika, Vita alotangulia
  132. Na qamisi ndio ile, Nyanyuko likwa mbele, Hapo hapana kelele, Yusufu amekosea
  133. Au tukiitazama, Imepasuka kwa nyuma, Zulekha ana lawama, Na ndie mwenye khatia
  134. Kijana alipokoma, Mwana mchanga kusema, Ikawa ni rai njema, Ushahidi alotoa
  135. Hata walipochungua, Qamisi kuangaliwa, Nyuma imepasuliwa, Wote kuishuhudia
  136. Basi kwa hichi kiwango, Tushaujua mpango, Zulekha ndie muongo, Yusufu kumzulia
  137. Mwishowe kimtangaza, Wanawake kueleza, Zulekha ni miujiza, Kwa yeye kutenda haya
  138. Kwani hawajaamini, Banati hao yakini, Kujua yuhali gani, Uzuri wake nabiya
  139. Khalafu wakatamka, Banati wakamtaka, Ili Yusufu kufika, Wapate mshuhudia
  140. Hapo Zulekha mwenyewe, Akasikia mwishowe, Kwa kumsema wenziwe, Khabari kumtokea
  141. Ndipo ghera kumshika, Kwake akawaalika, Na vyakula akaweka, Wote wakahudhuria
  142. Akapitisha sharuti, Mbele yao mabanati, Wakayakubali dhati, Zulekha alowambia
  143. Yusufu alipopita, Banati wakamkuta, Kwa visu wakajikata, Bila ya kufahamia
  144. Wote kodo macho mbele, Ajabu ya maumbile, Wakakatika vidole, Kwa urembo wa nabiya
  145. Ni hapo kujulikana, Hapo walipomuona, Kuwa ni mzuri sana, Yusufu wameridhia
  146. Mwanena lawama kwangu, Kwa hasira na uchungu, Jitizameni wenzangu, Nanyi yalowafikia
  147. Nanyi mumeadhirika, Kushinda yalonifika, Na vidole kukatika, Bila ya kuzingatia
  148. Wakazidi kina mama, Waeleza kua kama, Zulekha hana lawama, Yusufu katimilia
  149. Basi mwisho akapuza, Kwa hasira kumkaza, Zulekha luwaeleza, Wenziwe kuwaambia
  150. Yakuwa asipoweza, Yusufu kunisikiza, Nyumba yake ni gereza, Lazima ataingia
  151. Namweleza ya muanga, Yangu anapoyapinga, Hakika nitamfunga, Kiapo namuapia
  152. Kisha tena awambiye, Hao mabibi wenziye, Na nyinyi semeni naye, Huenda akasikia
  153. Zulekha kumpa nguvu, Kwa alosema maovu, Wakafanya uerevu, Tumwa kumkazania
  154. Ndipo wakamuarifu, Kwa nguvu na takilifu, Wakamwmbia Yusufu, Ya bibi yako ridhia
  155. Ikawa asitamke, Yusufu asiyashike, Maneno ya wanawake, Hayo waliyomwambia
  156. Kwa hayo aloambiwa, Akaona hana dawa, Ila ya kuomba dua, Kwa Mola wake Jalia
  157. Na Yusufu dua yake, Ni machafu yamwepuke, Kalingana Mola wake, Hapo akaombolea
  158. Ya Rabi Mola ujuwe, Yashanishinda mwenyewe, Uiwezae ni Wewe, Shida yangu yakwelea
  159. Nihifadhi Bwana Mola, Kwani sina tena hila, Kwangu kheri kwenda jela, Kuliko huno udhia
  160. Mungu aliyakubali, Maombi yake rasuli, Kwa mujibu wa kauli, Ya dua yake nabiya
  161. Akamkinga Jalali, Na wa Zulekha muhali, Rabi akatakabali, Na gerezani kungia
  162. Ikawa si muda tena, Zulekha kungoja sana, Ndipo aanze fitina, Uongo kuuchochea
  163. Maana alipojuwa, Atakalo halikuwa, Tena ameadhiriwa, Khabari zimeenea
  164. Akamwambia waziri, Mume wake kasisiri, Bwana nnayo khabari, Tafadhali nisikiya
  165. Nakuomba kwa hisani, Yusufu mtie ndani, Mpeleke gerezani, Kwani amenikosea
  166. Mji wote ni sherehe, Yusufu kunifedhehe, Katu usimsamehe, Idhara imeenea
  167. Na kwa hapo ndipo mume, Asijibu asiseme, Ya mkewe aandame, Bila ya kufikiria
  168. Waziri akawa radhi, Ili bibi amridhi, Mkewe asimuudhi, Ijapo ni jambo baya
  169. Kamtia kifungoni, Yusufu korokoroni, Hali hako makosani, Badili kumuonea
  170. Yusufu akenda ndani, Na wawili ithinani, Walokua khatiani, Kwa yao walokosea
  171. Walifanya ukhalifu, Mfalume kaarifu, Wafungwe wawe madufu, Na adabu kuwatia
  172. Kwa kutokea ubishi, Kwa ndoto za ushawishi, Waloota watumishi, Jela walikofungiwa
  173. Na wakenda kwa Yusufu, Kwa shaka na takilifu, Kwani ashawaarifu, Kua ndoto zamwelea
  174. Saiki ndie wa kwanza, Aliyejitanguliza, Ndoto yake kueleza, Yusufu kuisikia
  175. Akasema jana kua, Nimeota kuchukua, Sinia iliyokua, Na vinywaji vimetiwa
  176. Na mwendo wangu wa shime, Njiani nisisimame, Nenda kwake mfalume, Vinywaji kumwandalia
  177. Yusufu akamjibu, Kama ilivyo wajibu, Kumpa njema jawabu, Ndoto kumfasiria
  178. Saiki akajibiwa, Ndoto ikaaguliwa, Kifungoni kutolewa, Tumwa kumbashiria
  179. Akanena langu shika, Wala usifanye shaka, Wewe jela utatoka, Kazi yako kurejea
  180. Mara hapo akaruka, Mpishi akatamka, Ili hakika kutaka, Kumjaribu nabiya
  181. Asifikiri ninini, Yakamwingia kichwani, Akaanza ubishani, Kujifanya yamwelea
  182. Na hapo bila kusita, Ndoto yake kufuata, Kusema aliyoota, Yote yalomfikia
  183. Yusufu kabwaga shingo, Kuusikiza uongo, Upangwavyo kwa mpango, Bila ya kuona haya
  184. Ewe nabii wa Mungu, Yusufu mkubwa wangu, Nimeota ndoto yangu, Nimejitweka sinia
  185. . Nimejitweka kichwani, Na mikate imo ndani, Naipeleka nyumbani, Kwa mkuu wa raiya
  186. Nilipokuwa njiani, Kaja ndege wa angani, Kaudona siniyani, Mkate kauchukua
  187. Mkate akaudona, Kabaki nimedangana, Ndipo Yusufu kanena, Ndoto kumfumbulia
  188. Fasiri ya ndoto yako, Haina salama kwako, Utakatwa kichwa chako, Lazima utauwawa
  189. Mpishi akaduwaa, Akawa ataataa, Ikawa hana tamaa, Kwa alivyobashiriwa
  190. Akamwambia mwalimu, Yusufu bwana fahamu, Hayo nilotakalamu, Ni dhihaka nakwambia
  191. Yusufu ndipo kusema, Ujuwe huna salama, Utauliwa lazima, Kama nilokwelezea
  192. Siku nyingi zisitimu, Kwa rehema za Karimu, Mungu akamrehemu, Saiki kafunguliwa
  193. Mwenziwe yule laimu, Aliyengiwa na hamu, Ikatolewa hukumu, Akenda akauwawa
  194. Na siku ya kuachana, Na Yusufu kuagana, Hapo Yusufu kanena, Saiki kumwashiria
  195. Akamba leo watoka, Kwako nnalolitaka, Siwache kunikumbuka, Yakumbuke mazoweya
  196. Ewe wangu muhisani, Sinisahau mwendani, Na kunitaja nyumbani, Kwake mfalume pia
  197. Saiki kenda kuanza, Kazi yake kufanyiza, Shetani kamsauza, Kutekeleza wasia
  198. Ikatukia azizi, Maliki kwenye malazi, Alipitiwa na njozi, Mno kaigutulia
  199. Muda alipogutuka, Malazini kuamka, Akangiwa na wahaka, Wasiwasi kumwingia
  200. Akawataka maliki, Watumiao falaki, Watizame kisa hiki, Cha ndoto ilomjia
  201. Kawaita makuhani, Wakuu wanavyuoni, Wote walio mjini, Kuja kumbashiria
  202. Nimewaita wajuzi, Muifanye yangu kazi, Ya ndoto munipe wazi, Jawabu ilo na njia
  203. Bidii munvyoweza, Munipe ya muangaza, Kwani yamenishangaza, Sasa nawatamkia
  204. Nimeota waungwana, Usingizini kuona, N'gombe walodhofu sana, Saba katika ruwiya
  205. Huwala walionona, N'gombe sabaa mabwana, Kisha nikaota tena, Baada ya mambo haya
  206. Nikayaota mashuke, Yaso kitu ndani yake, Na mengine yalo pweke, Sabaa yaliyojaa
  207. Ikabidi makuhani, Kutazama vitabuni, Kuiona hawaoni, Akili zimewashia
  208. Kushindwa kwa watu hao, Maliki kazidi mwao, Akawa hana makao, Wasiwasi kuzidia
  209. Saiki akagutuka, Ghafula kamkumbuka, Yusufu akatamka, Maliki kumwelezea
  210. Saiki katakalamu, Kumwambia muadhamu, Mimi bwana nafahamu, Wakati nilipokuwa
  211. Nimefungwa gerezani, Nilimkuta mwendani, Mfadhila na hisani, Ajuaye mambo haya
  212. Na Yusufu kakariri, Bila ya kuyafikiri, Ndoto akaibashiri, Alivyombashiria
  213. Ni miaka ya neema, Sabaa ya wakulima, Watavuna vuno jema, Chakula cha kuzidia
  214. Ikisha miaka hiyo, Yenye shibe iso choyo, Itakuja mengineyo, Saba ya watu kulia
  215. Kilio kiso nyamaa, Kwa kungiliwa na njaa, Iwe ni kuu balaa, Chakula kuwashilia
  216. Kupata hayo Saiki, Mambo yakamuafiki, Akamwambia rafiki, Yusufu tuonye njia
  217. Yusufu yake kalima, Kampa jawabu njema, Nawalime wakulima, Mavuno yakiwadia
  218. Mupatafute mahala, Muvitie kwenye ghala, Shida ikija ghafula, Mupate cha kutumia
  219. Basi hapo ikabidi, Bwana Saiki karudi, Na kamili ushahidi, Wa kwenda kuwaridhia
  220. Hata akifika ndani, Kwa mfalume nyumbani, Akaeleza makini, Yote yaliyotukia
  221. Alimpa tafsiri, Ya ndoto yake dhahiri, Mambo yatakayojiri, Ambayo yatatokea
  222. Papo kastaajabu, Mfalume kwa jawabu, Mno kaona ajabu, Kwa ujuzi wa nabiya
  223. Na pale pale kwa hamu, Maliki katakalamu, Saiki kumlazimu, Upesi jela rejea
  224. Mwite Yusufu haraka, Umwambie ukifika, Mfalume akutaka, Haraka akungojea
  225. Kufika kwenye kizimba, Asingoje akamwamba, Yusufu bwana aomba, Wende kwake akwambia
  226. Kukangiya walakini, Kuwa haiwezekani, La kutoka gerezani, Yusufu kakatalia
  227. Akasema kumjuza, Saiki kumueleza, Mimi katika gereza, Sitaondoka sikia
  228. Salamu zangu zifishe, Mfalume mjulishe, Mpaka athubutishe, Yakua sikukosea
  229. Na kisha kwa hiki kisa, Awajuze watu khasa, Yakuwa sina makosa, Zulekha ndie mbaya
  230. Awaite vilevile, Banati wa siku ile, Walojikata vidole, Na Zulekha wote pia
  231. Ni kua apeleleze, Maliki awaulize, Wanawake wamweleze, Ni yupi alokosea
  232. Saiki akaushika, Ujumbe kaupeleka, Yote aliyotamka, Yusufu kumwaridhia
  233. Alipokwisha ambiwa, Maliki kuelezewa, Maneno yakamtuwa, Pingamizi kutotia
  234. Ndipo hapo apeleke, Mfalume mtu wake, Wakaitwe wanawake, Na wote wakafika
  235. Banati wakiwasili, Maliki kawakabili, Kisha akawasaili, Mfalume kuwambia
  236. Musiogope muhali, Baina hawa wawili, Mwenye makosa kwa kweli, Mwaweza kunitajia
  237. Ni Zulekha na Yusufu, Mkosa muniarifu, Yupi alo mpotofu, Huyo alo na hatia
  238. Wanawake wakasema, Kwa upole na heshima, Bwana mwenye na lawama, Zulekha ndie mbaya
  239. Na Zulekha baadae, Akiulizwa na yeye, Asili asikatae, Akajibu ya sharia
  240. Yakua wangu ulimi, Leo uongo sisemi, Mwenye makosa ni mimi, Hakika nakubalia
  241. Mfalume ufahamu, Yusufu simlaumu, Bali niemedhulumu, Na tena kumzulia
  242. Zulekha akalingana, Ya Ilahi Subhana, Nakubali mimi Bwana, Yakua nimekosea
  243. Na makosa kua kwangu, Nakuomba Bwana Mungu, Nisamehe dhambi zangu, Ya Rabbi Mola Jalia
  244. Yote maneno ya watu, Yusufu imethubutu, Si mkosa huyu mtu, Hakika imetokea
  245. Imethubutu Yusufu, Kua mtu mtukufu, Sababu hana machafu, Maovu kujizuiya
  246. Zulekha alitamka, Kua alighilibika, Ndie aliemtaka, Sasa amekubalia
  247. Tushafahamu Yusufu, Kwamba hana ukhalifu, Zulekha ndie mchafu, Kosa lilomwelemea
  248. Alipopata ukweli, Maliki kwa jambo hili, Ikawa yastahili, Yusufu kwenda tolewa
  249. Ndipo Saiki atoka, Kwa furaha na kucheka, Kwa Yusufu akifika, Akawa atmwambia
  250. Itunze yako nafusi, Usiwe na wasiwasi, Zulekha ndie mkosi, Makosa ameridhia
  251. Wameitwa watu tele, Kaulizwa mambo yale, Akajibu yale yale, Kama yalivyotokea
  252. Yusufu iliyobaki, Sasa twende kwa Maliki, Usiwe mwenye hamaki, Kufikiri mambo haya
  253. Yusufu akaitika, Gerezani akatoka, Kwa Maliki akafika, Vizuri akapokewa
  254. Maliki akasimama, Mtukufu wa heshima, Akampa taadhima, Sitaha kumfanyia
  255. Maliki kamkubali, Kuwa ni mtu wa kweli, Tena ni mwenye akili, Yusufu kajaaliwa
  256. Yusufu akataraji, Awe waziri wa mji, Awe ni mtazamaji, Neema ikitokea
  257. Mfalme karidhia, Na kumsafia nia, Akamba nakuachia, Fanya litakalofaa
  258. Yusufu asighairi, Wala asitaakhiri, Akashika uwaziri, Cheo hicho kupokea
  259. Ndipo yaanza neema, Chakula mji mzima, Furaha kwa wakulima, Hadi waliobakia
  260. Wala vyema wakishiba, Na vyengine kwa akiba, Muda wa miaka saba, Njaa kuwaepukia
  261. . Kwa furaha wakakaa, Muda wa myaka sabaa, Hapo ikangia njaa, Raha kuwapungukia
  262. Lakini wao hakika, Japo njaa imefika, Waliishi pasi shaka, Wakila bila udhia
  263. Ila ilizidi dhiki, Kwa miji iliyobaki, Kwa majirani rafiki, Njaa ikawafikia
  264. Ndipo ilipomsibu, Njaa kuu Yaakubu, Kumfikia taabu, Ya wanawe wote pia
  265. Yaakubu hapo basi, Akazidi wasiwasi, Wakati alipohisi, Chakula kimeishia
  266. Na baba yeye mwenyewe, Akawajuza wanawe, Kuwaambia wajuwe, Njaa ile ilongia
  267. Ili kwamba wasafiri, Wende mji wa Misiri, Na wana wakakhiari, Baba kumkubalia
  268. Wakenda wana ashara, Ila wa hidaashara, Hakua na msafara, Nyumbani akabakia
  269. Aliebaki nyumbani, Kutokua safarini, Ni huyu Binyamini, Ndie aliesalia
  270. Mwana huyu mtukufu, Na tena nawaarifu, Ni mdogo wa Yusufu, Kwa baba na mama pia
  271. Basi kumi walobaki, Wakenda na yao dhiki, Kuitafuta riziki, Misiri wakafikia
  272. Wakawasili vijana, Hata walipopambana, Yusufu akawaona, Kwake walipoingia
  273. Walipofika ikawa, Yusufu kuwatambuwa, Na wao kutomjuwa, Yakuwa ni ndugu moya
  274. Yusufu akafuliza, Na wao kuzungumza, Na hali kuwauliza, Na wao kumwelezea
  275. Yusufu yakamtosha, Nduguze walompasha, Nae akayakinisha, Ni nduguze wote pia
  276. Khalafu mwisho akaze, Yusufu awaeleze, Awaambie nduguze, Hao walomjilia
  277. Katamka akanena, Enyi ashara vijana, Munaporejea tena, Hapa mukifikilia
  278. Ndugu yenu muje nae, Aandamane na nyie, Ili hapa afikie, Nipate mshuhudia
  279. Hilo hakika nawapa, Nisipomuona hapa, Na chakula sitawapa, Munachokihitajia
  280. Wala musinifikie, Kwangu musikaribie, Huko huko mubakie, Sitaki washuhudia
  281. Ikangia tafauti, La kusema hawapati, Ikawa kwao sharuti, Ndugu hao kuregea
  282. Wakapakiliwa tweka, Za chakula walotaka, Ili wapate ondoka, Makwao kurejelea
  283. Walipowasili kwao, Kufikia ndugu hao, Wakampa baba yao, Khabari ilotukia
  284. Walipofungua tweka, Nyoyo ziliwapasuka, Kwa furaha kuwafika, Ya mali kuregezewa
  285. Hata chakula kikisha, Ndiyo siku ikatisha, Wana kujitayarisha, Safari kuandalia
  286. Baba wakamshauri, Ili wao kwa uzuri, Kwa huyo mwana saghiri, Ili wende nae pia
  287. Na watoto wakasema, Kumpa baba kalima, Baba hakyna hekima, Tutakayokufanyia
  288. Utupe Binyamini, Awe nasi safarini, Usiwaze asilani, Salama atarejea
  289. Na baba yakamtanza, Halijui la kufanza, Akakumbuka la kwanza, La Yusufu kupotea
  290. Baba alifanya khofu, Akidhania machafu, Yalomkumba Yusufu, Na huyu atatendewa
  291. Khalafu akakariri, Kuwapa wana khabari, Akasema mwafikiri, Kua nitakubalia
  292. Na wana yao kauli, Kumtoa mushikili, Wakasema ilo kweli, Baba yao kumwambia
  293. Hakika amtakae, Ili sisi twende nae, Ni waziri asemae, Ndiyo alotwelezea
  294. Kwa nyingi taabu, Akanena Yaakubu, Wanawe akawajibu, Kwa hilo sitaridhia
  295. Hendi hadi ushahidi, Munipe kweli ahadi, Yake Ilahi Wadudi, Yakuwa atarejea
  296. Na ijapo ni ajali, Jambo lisokua hili, Siwalaumu asili, Apendalo Mungu huwa
  297. Na wana wote walipo, Ikawa kula kiapo, Wakasema papo hapo, Kwa Mungu kushahidia
  298. Wallahi twenda na yeye, Khofu isikuingiye, Baba tutakuja nae, Mwanayo atarejea
  299. Baba kwa hino ahadi, Ya ashara auladi, Moyowe uliburudi, Imani ikamwingia
  300. Basi baba akaridhi, Moyo wake kuwa radhi, Mwanawe kuwakabidhi, Wanawe walosalia
  301. Ndipo baba amtake, Binyamini afike, Na alipokuja kwake, Mara kamkumbatia
  302. Yaakubu akanena, Na mwanawe kuagana, Kwaheri ya kuonana, Na kheri nakutakia
  303. Safiri Binyamini, Kwa salama salmini, Na urudi mara thani, Kwa umri na afiya
  304. Hapo muda ukajiri, Hapana tena shauri, Vijana wakasafiri, Hidaashara pamoya
  305. Wakenda mara ya pili, Vijana kama awali, Kwa Yusufu kuwasili, Misiri wakafikia
  306. Kuwasili ikhiwani, Yusufu kwake nyumbani, Kwapanga ithineni, Wawili chumba kimoya
  307. Yusufu yake akili, Kwatenga mbalimbali, Ndugu wawili wawili, Mdogo akasalia
  308. Ndipo basi masikini, Kabaki pweke mwendani, Yaani Binyamini, Hapo kaanza kulia
  309. Mambo yakamtatiza, Yusufu kumshangaza, Kisha akamuuliza, Mdogowe kumwambia
  310. Nieleze kwa makini, Likulizalo ni nini, Walizwa na jambo gani, Nambia nipate juwa
  311. Binyamini kasema, Kwa sauti ya huruma, Kumpa yake kalima, Yusufu kumwadithia
  312. Lau yuhai Yusufu, Leo mimi pasi khofu, Singepata takilifu, Kwa haya kunifikia
  313. Yusufu nae kajibu, Wasemaje mahabubu, Leo ni wako sahibu, Binyamini sikia
  314. Yusufu na ndugu yake, Wakangia chumba pweke, Na Yusufu atamke, Siri hapo kuitoa
  315. Kampa la burudiko, Biyamini tamko, Mimi ndie ndugu yako, Yusufu alopotea
  316. Na muda ulipofika, Ndugu chakula kutaka, Ili wapate ondoka, Kwa haraka kurejea
  317. Wote wakamiminiwa, Magunia kujaziwa, Bila ya kulia ngowa, Na Binyamini pia
  318. Lakini gunia lake, La Yusufu ndugu yake, Yaani mdogo wake, Huyo aliyeletewa
  319. Humo mwake guniani, Kwa huyo Binyamini, Kaificha pishi ndani, Yusufu kumtilia
  320. Ndipo ndugu wakafisha, Safari kutayarisha, Mizigo kuipandisha, Kuwabebesha ngamia
  321. Na mara kwa muda huo, Kuepuka ndugu hao, Katika safari yao, Wanjiani warejea
  322. Askari nae basi, Akakimbia upesi, Akawakuta khalisi, Bado wangali na njia
  323. Muda alipowapata, Asikari, kuwakuta, Kwa kelele kawaita, Mkono kuwapungia
  324. Askari kanena, Kuwajulisha vijana, Nasema kwenu mabwana, Jambo nilowaitia
  325. Nimeambiwa nifike, Na Maliki niwashike, Imeibwa pishi yake, Ya chakula kupimia
  326. Na vijana wakafika, Kwa khofu kutetemeka, Khalafu wakatamka, Askari kumwambia
  327. Twaapa kwa Mwenye enzi, Twakupa ilyo wazi, Sisi bwana sio wezi, Pishi tulowaibia
  328. Yusufu kasisitiza, Mwishowe kuwauliza, Ni nini yake majaza, Pishi aliyeitwaa
  329. Walipoulizwa hayo, Wakamjibu kwa payo, Jaza yake mtu huyo, Adhabu kumfikiya
  330. Ikatazamwa vizuri, Kwa ndugu hao kabiri, Na ikawa asikari, Pishi hakuivumbuwa
  331. Basi kawa imara, Askari kuchakura, Hadi vijana ashara, Kwenye yao magunia
  332. Askari kakazana, Hata wa kumi kijana, Na pia hakuiona, Pishi kuishuhudia
  333. Kuja kutizama nadani, Kwa huyo Binyamini, Humo mwake guniani, Pishi hio ikagwiwa
  334. Kufika wakatongowa, Uongo wakauzuwa, Kwama huyu hana dawa, Si mwanzo kufanya haya
  335. Na huyo ndugu wa mbele, Alimwivi vile vile, Hata tembe ya mchele, Akiona huitwaa
  336. Yusufu katabasamu, Moyoni katakalamu, Ni uovu ulotimu, Machoni kunizulia
  337. Bwana ufanye imani, Twakuomba kwa hisani, Muwache Binyamini, Tafadhali twakwambia
  338. Twaomba kwako Maliki, Na sote kutuafiki, Mmoja wetu kubaki, Badili kumfidia
  339. Yusufu yake kauli, La ndugu asikubali, Kushika mtu badali, Hilo hakukubalia
  340. Hapo akazidi chuki, Ndugu mkubwa hataki, Kanena mimi sitoki, Misri nitabakia
  341. Kuwasili kwa mzazi, Na mema maamkuzi, Kisha lao simulizi, Baba kumuhadithia
  342. Siri hawakuiziba, Wakampa wazi baba, Baba mwanao kaiba, Nasi kumshuhudia
  343. Na baba yake kauli, Kajibu hili si kweli, Hilo ni yenu nakili, Ni hila mwaniletea
  344. Kwa yote haya madhara, Inshalla niko imara, Mungu tanipa subira, Njema ya kuvumilia
  345. Kisa hiki kumfika, Ndipo alipokumbuka, Yale ya kwanza mashaka, Ya Yusufu kupotea
  346. Akanena kwa uchungu, Rudini enyi wanangu, Kwenye aridhi ya Mungu, Musiogope udhia
  347. Nendeni pasi nakhofu, Musijali takilifu, Mumtafute Yusufu, Na Binyamini pamoya
  348. Wakafika kwa heshima, Kwake Yusufu salama, Na wote wakainama, Hishima kumfanyia
  349. Khalafu kisha waanze, Wakatamka nduguze, Yusufu wamueleze, Wanalolihitajia
  350. Ewe mwingi wa fadhila, Tuna haja ya chakula, Sisi na yetu aila, Tusije kufa na njaa
  351. Nasi hatuna thamani, Wala kitu mkononi, Ila ni bidhaa duni, Isiyo na manufaa
  352. Yusufu kasikitika, Wazazi kawakumbuka, Machozi yakamtoka, Hawezi kuvumilia
  353. Sasa ndio wapambana, Yusufu na hao wana, Maswali kujibizana, Siri Yusufu atoa
  354. Yote mambo ya zamani, Ya kutupwa kisimani, Ndipo hapo yabaini, Yusufu alotendewa
  355. Yusufu awaambie, Ni nani wapili yeye, Alofarikana nae, Baba alompotea
  356. Ndugu wakamuarifu, Wakasema bila khofu, Jina lake ni Yusufu, Mwana aloangamia
  357. Na ndugu wakatongowa, Yusufu akajibiwa, Mwana huyo kauawa, Na mbwa mwitu kuliwa
  358. Yusufu akatamka, Kweli mbwa kamshika, Au nyinyi kwa hakika, Kisa mumemtendea
  359. Yusufu kasema tena, Na ndugu kujibishana, Hamukufanya khiana, Kisimani kumtia
  360. Na papo wakajibiwa, Na Yusufu kuambiwa, Jee aliemuuwa, Ni nyinyi wenu mmoya
  361. Ndugu nao kwa upesi, Wakanena kua sisi, Tutauwaje nafusi, Bila kisa kutokea
  362. Basi Yusufu kakaza, Kuzidi kuwaeleza, Yote waloyafanyiza, Mpaka kuishilia
  363. Na hiyo si dhambi katu, Kwa huyo mbwa wa mwitu, Hiyo ni dhambi ya watu, Yenu mulokusudia
  364. Ajabu yao ni kua, Vipi Yusufu kujua, Ni kama aliekua, Yuko na wao pamoya
  365. Baadae ndipo tena, Mmoja wao vijana, Alama akaiona, Yusufu kamtambua
  366. Na hapo kwa nyingi khofu, Kanena kwa takilifu, Wewe kwani ni Yusufu, Bwana hebu niambia
  367. Yusufu nae haraka, Na mara akatamka, Mimi ndie pasi shaka, Yusufu alopotea
  368. Ndie Yusufu wenzangu, Mimi mtume wa Mungu, Na huyu ni ndugu yangu, Aliyeniandamia
  369. Akazidi kukariri, Kuwapa ndugu khabari, Hakika ukisubiri, Mja kwa kila udhia
  370. Nao ndugu wakaanza, Yusufu wakamweleza, Mola amekutukuza, Kwa dhiki kuvumilia
  371. Kwa hili Yusufu kuwa, Mungu akujaze sawa, Kwa uliyoyachukuwa, Mambo tulokufanyia
  372. Yusufu nae kasema, Kuwajibu ndugu vyema, Leo hakuna lawama, Kwenu nyinyi ndugu pia
  373. Na mola wetu Karimu, Tawasamehe Rahimu, Ndie mwenye kurehemu, Viumbe wake Jalia
  374. Kisha nae atamke, Yusufu kwa ndugu zake, Qamisi muipeleke, Nawatuma nyote pia
  375. Twaeni yangu libasi, Tena haraka upesi, Mufikapo na qamisi, Kwa baba mukiingia
  376. Musimpe mkononi, Nitakavyo ikhiwani, Mumbwagie usoni, Macho yatamrudia
  377. Na khalafu baadae, Murudi pamoja nae, Nyote kwangu mugurie, Pasi mtu kubakia
  378. Muje na wote jamaa, Na wala kutokataa, Tuje pamoja kukaa, Hapa kwangu kuguria
  379. Walipotoka nyumbani, Kwa Yusufu ikhiwani, Wakali bado ndiani, Muda wakisafiria
  380. Yaakubu mtukufu, Akasikia harufu, Ya qamisi ya Yusufu, Puani kumuingia
  381. Ilokwenda kwa upepo, Muda huo hapo hapo, Kwa Yaakubu alipo, Harufu kumfikia
  382. Yaakubu kabashiri, Kwa walokua hadhiri, Akawapasha khabari, Akasema kuwambiya
  383. Naisikia harufu, Ya mwanangu maarufu, Al-waladi Yusufu, Fuadi alopotea
  384. . Jamaa wakamjibu, Kumweleza Yaakubu, Yuko wapi aloghibu, Alokufa kurejea
  385. Mara kwa chache dakika, Saa kutomalizika, Hapo wana wakafika, Kwa shangwe wakatokea
  386. Na mbele ya kujilisi, Ili wapate marisi, Waliibwaga qamisi,Usoni kumtupia
  387. Akarejea kuona, Kama zama za ujana, Na kisha ndipo kanena, Yaakubu kutongowa
  388. Kujuza wale mabwana, Mbele ya kuja vijana, Kwa harufu kushindana, Wakati wakiongea
  389. Yaakubu katongowa, Mambo nnayoelewa, Najuwa musoyajuwa, Mimi sikuwaambia
  390. Kwa kufupisha maneno, Mambo yakawa manono, Furaha iso mfano, Kwa baba na wana pia
  391. Na hapo baba na wana, Wote kukumbatiana, Dhambi kusameheana, Wana waloyakosea
  392. Ikawa baba kuhama, Wana pamoja na mama, Wakawasili salama, Kwa Yusufu kuguria
  393. Kawakaribisha vyema, Aila ilomwandama, Kwa adabu na heshima, Yusufu kuwapokea
  394. Furaha ikawa kuu, Wana hadi wajukuu, Si shangwe mambo makuu, Furaha kuwazidia
  395. Kisha ndipo kawaweka, Wazazi wake katika, Kiti chenye mamlaka, Heshima kuwafanyia
  396. Na mara baba na mama, Na wana wakaandama, Kwa furaha kuinama, Wakasujudu pamoya
  397. Walipokwisha pumuka, Kwa furaha na kucheka, Wakashukuru Rabuka, Kumhimidi Jalia
  398. Na muda huo haraka, Yusufu papo kafika, Ndoto yake kakumbuka,Ya zama zilopitia
  399. Akamweleza mzazi, Babake kumpa wazi, Huno ndio uwaguzi, Wa ndoto nilokwambia
  400. Alizidi akinena, Wa ndoto niloiona, Katika wangu ujana, Leo yatufunukia
  401. Siku leo imefisha, Ya Mola kutonyesha, Haki amehakikisha, Ilahi Pweke Mmoya
  402. Tena Ilahi Karima, Kanitendea na wema, Kuniokoa salama, Jela kunifungulia
  403. Na nyinyi akawaleta, Niliko kunifuata, Mukaja mukanikuta, Kwa salama na afiya
  404. Kwa uwezo wa Rabbana, Kawaleta nyinyi tena, Tukaja tukaonana, Kujumuika pamoya
  405. Na mwisho wake khalafu, Mtume mwema Yusufu, Kamshukuru Latifu, Huku akiombolea
  406. Ewe Bwana Mtukufu, Uliyenipa sharafu, Ufalme uso khofu, Bwana Ulotimilia
  407. Ukanipa na uweza, Ndoto za kimiujiza, Uwaguzi kunifunza, Tafsiri kuzijua
  408. Ewe Mwenye enzi Mungu, Ya Ilahi Mola wangu, Uloumba ulimwengu, Na ardhi zote pia
  409. Ya ilahi niongowa, Nipite hali ya kuwa, Kila haki kuijuwa, Na kwako kunyenyekea
  410. Njia njema nionyeshe, Na wema nilahikishe, Yaani nikutanishe, Na wetu wema Jalia
  411. Na hapo akamaliza, Yusufu aloeleza, Pasi moja kulisaza, Shukurani kutumia
  412. Kwa hivyo wote wendani, Wakakutana yakini, Kama zama za zamani, Siku zilizopitia
  413. Kufikia kwa Yusufu, Aila ilo tukufu, Wakaishi bila khofu, Kusahau yote pia
  414. Kwa furaha wakadumu, Kwenye makao timamu, Nyoyo zikatabasamu, Hadi kuaga dunia
  415. Kwa kufupisha niseme, Yusufu kawa mtume, Kapata na ufalume, Mola kumjaalia
  416. Basi hapa waungwana, Yatosha niloyanena, Ya zaidi tena sina, Samahani ila haya
  417. Sasa ndio nasimama, Kisa chetu kimekoma, Na dua kwake Karima, Naanza kuombolea
  418. Ni wewe Mola Mmoja, Muumba wa sote waja, Itimize yetu haja, Ilahi watusikia
  419. Twakuomba Ya Manani, Isilamu ikhiwani, Tuongoze kwenye dini, Imani kutuzidia
  420. Tupe nguvu za nafusi, Tumshinde Ibilisi, Asiipate nafasi, Njia mbovu kututia
  421. Twakuomba Ya Wadudi, Machafu yawe baidi, Na waovu mahasidi, Yao kutowanyokea
  422. Ya Ilahi Ya Karimu, Tupe akili timamu, Ya dini na ya ilimu, Tushike bila udhiya
  423. Tulinde tuwe wekevu, Tuyaepuke maovu, Na nyoyo ziwe na nguvu, Machafu kuyakimbia
  424. Tuepushie na dhara, Kwa dini tuwe imara, Twaiomba na sitara, Ya akhera na dunia
  425. Dua ifike ulipo, Na kabuli ije papo, Utupe na njema pepo, Hiyo ulotwandalia
  426. Amina Rabi amina, Amina Mola amina, Utukabalie Bwana, Kwa baraka za nabiya
  427. Na hapa ninamsifu, Mola wetu Mtukufu, Mkubwa Mtakatifu, Taala Rabi Jaliya
  428. Na mtume Muhammadi, Mjumbe wake Wadudi, Kila siku turadidi, Swala na salamu pia
  429. Bwana Saidi Karama, Mungu takwegesha pema, Akupe na nyingi hima, Malenga usiye doa

Mtungaji : Said Karama - Lamu
Mletaji: Saleh Barkey

 

  About Us | Zanzinet Home | Contact Us | ©2004 Zanzinet