|
|
Naliya!
- L-akhi nakuja kwako, Kukupa niliyo nayo
Ni mbali nitokeyako, Nakuja kwa haja hiyo
Nakuja kwa sikitiko, Na tena nna kiliyo
Naliya ndani ya moyo, Kwa kuninyima harusi
- Naliya nasikitika, Kuninyima harusiyo
Naliya nahuzunika, Sijuwi niyasemayo
Naliya nikikumbuka, Kunikhasimu kakeyo
Naliya ndani ya moyo, Kwa kuninyima harusi
- Naililiya suhuba, Nzuri tuliyonayo
Naliya hipiga toba, Hiyakumbuka mamboyo
Naliya hii dharuba, Ni kubwa unipigayo
Naliya ndani ya moyo, Kwa kuninyima harusi
- Naliya sikukudhani, Waweza kufanya hayo
Naliya nimebaini, Kuwa ndiyo tabiayo
Naliya nna huzuni, Nawe fanya upendayo
Naliya ndani ya moyo, Kwa kuninyima harusi
- Naliya nikifikiri, Ni mengi niyawazayo
Naliya sina nadhari, Kwa hayo nikumbukayo
Naliya nikisubiri, Nayangojeya yajayo
Naliya ndani ya moyo, Kwa kuninyima harusi
- Naliya hiomboleza, Katu furaha sinayo
Naliya sitanyamaza, Roho yangu yenda mbiyo
Naliya chaniumiza, Kidonda cha dundumiyo
Naliya ndani ya moyo, Kwa kuninyima harusi
- Naliya natiya tama, Shairi niitungayo
Naliya siwezi sema, Nnafikiya upeyo
Naliya yananikwama, Mabaya unifanyayo
Naliya ndani ya moyo, Kwa kuninyima harusi
(Kidonda cha dundumiyo = Kidonda cha kooni)
DUNDUMIYO = koo = koromeo
Khamis Nassor Al-Nabhany
|