NJAA NA SHIBA (Suali)!
Date: 27 August, 2006
Yafuatayo ni mashairi mawili yenye jina NJAA NA SHIBA. La kwanza ni suala na la pili ni majibu yake. Suala limeulizwa na kijana Muhammed Suleiman ambae hapo alipotunga shairi hili mwaka 1982 alikuwa ndio kwanza anajifundisha kutunga na munaweza kuzigundua kasoro kidogo za utungaji. Alimpelekea Sk. Khamis bin Nassor Al-Nabhani, Mola amrehemu, ambae amemjibu kama munavyoona.
Njaa na shiba ilivyokusudiwa unaachiwa msomaji ufafanuwe.
- Nimengiya kwenye pango - Kubwa tena ni katile
Kwa yangu yote mipango - Nashindwa kutoka mule
Wewe ni mwenye mipango - Naomba uniokole
Hii njaa naye shiba - Aliye bingwa ni nani
- Nimezongwa mote mote - Nashindwa kufika mule
Kwa kakara zangu zote - Nashindwa kutoka mule
Nabaki kutema mate - Kama nyoka kipilile
Hii njaa naye shiba - Aliye bingwa ni nani
- Nimekuja huko kwako - Wewe unisaidile
Niokowe ami yako - Nitoke pangoni mule
Ufanye akili zako - Kwani zako ni za kale
Hii njaa naye shiba - Aliye bingwa ni nani
- Shiba ikiwa tumboni - Njaa haikai mule
Si mchana si jioni - Kabisa haipotele
Yazunguuka uwani - Kidogo yafika pale
Hii njaa naye shiba - Aliye bingwa ni nani
- Shiba ikiwa tumboni - Ikitazama kwa mbele
Kiona njaa njiani - Yaja kwenye tumbo lile
Haikai asilani - Yatoka bila sumile
Hii njaa naye shiba - Aliye bingwa ni nani
- Mambo haya ni magumu - Nawauliza wa kale
Nyinyi ni mulo khitimu - Akili yenu imbele
Nami bado ni hirimu - Akili ni ya chechele
Hii njaa naye shiba - Aliye bingwa ni nani
- Hapa ndio kituoni - Kabisa siendi mbele
Jibu liweke nyumbani - Nikija nilikutile
Mimi naja karibuni - Tamaa usikatile
Hii njaa naye shiba - Aliye bingwa ni nani
Mtungaji : Muhammed Suleiman
NJAA NA SHIBA (Jawabu)!
- Nakuja nakaa sungo - Niseme unisikile
Nikuonyeshe mlango - Penye wazi upitile
Utoke huna kinyongo - Ufurahike milele
Njaa ni bingwa wa ndwele - Na shiba ina huzuni
- Nikupayo yakamate - Na tena uyatumile
Ya watu usifuate - Nakwambia kwa kelele
Ashibae ni kiwete - Mwenda wazimu mpole
Njaa ni bingwa wa ndwele - Na shiba ina huzuni
- Kitini kaa kitako - Ulo nalo unambile
Useme maradhi yako - Madawa nikusagile
Nikutibu wende zako - Wende ukanitambule
Njaa ni bingwa wa ndwele - Na shiba ina huzuni
- Shiba ina kisirani - Uvivu ndiyo umbole
Shiba ikiwa tumboni - Njaa hupiga kelele
Huwaita majirani - Wafike wampokele
Njaa ni bingwa wa ndwele - Na shiba ina huzuni
- Katu shiba huioni - Kwa hayo usitongole
Hayaingii kichwani - Kwa hayo usinambile
Njaa ikija mjini - Huzinga nyumba ingile
Njaa ni bingwa wa ndwele - Na shiba ina huzuni
- Hayo ni mambo adhimu - Sikiliza nikwambile
Nikwambie ufahamu - Ukae ukumbukile
Yamo ndani ya dhulamu - Wala usiyafichule
Njaa ni bingwa wa ndwele - Na shiba ina huzuni
- Tamati sendi usoni - Bora sasa nipumule
Nami nipo uwanjani - Ukija nikupokele
Nikujibu kwa undani - Uchukuwe utumile
Njaa ni bingwa wa ndwele - Na shiba ina huzuni
Mtungaji : Sh. Khamis bin Nassor Al-Nabhany Mola amrehemu