|
|
Ondoa!
Date: 7 September, 2007
- Ondoa toa sitaki, kuasi Mwenyezi Mungu,
Ya nguruwe mishikaki, na mikuku ya kizungu,
Minofu iso ya haki, sionji ulimi wangu,
Ondoa mlo batili, vya haramu sifuturu.
- Huwezi kunizuzuwa, nipate kizunguzungu,
Nyepesi nikachagua, hukumu za mwenye mbingu,
Katu sintopagawa, kuzigawanya mafungu,
Ondoa mlo batili, vya haramu sifuturu.
- Sitanii kweli kweli, japo nipigwe virungu,
Chumo lisilo halali, sizugiki walimwengu,
Iwekwe na kachumbali, sirambi enyi wenzangu,
Ondoa mlo batili, vya haramu sifuturu.
- Nimekhiyari kufunga, lengo niwe mcha Mungu,
Sili ulovikaanga, vinono vya chako chungu,
Bora nifuturu chunga, hata kama ya uchungu,
Ondoa mlo batili, vya haramu sifuturu.
- Kabla hata kufunga, sikufanya vunja jungu,
Leo sitegwi kijinga, kheri yazuke majungu,
Mukisema najivunga, maji yanatosha kwangu,
Ondoa mlo batili, vya haramu sifuturu.
- Hata kama nitakufa, kinywa kimefungwa pingu,
Bado nitapata shufa, chini na kwenye mawingu,
Na kutesa maghorofa, makasisi si vidungu,
Ondoa mlo batili, vya haramu sifuturu.
- Nangoja siku ya Idi, sana nimtaje Mungu,
Uso ukimuhimidi, chini liwe paji langu,
Kwenye busati jadidi, radhi awe Mola wangu,
Ondoa mlo batili, vya haramu sifuturu.
Al- Habibi Al Mardad,
Dar es Salaam.
|