.

Welcome to Zanzinet Swahili Poems

Where Swahili matters!

Tahadhari Na Ukimwi!

 

 

 

 

 

 

Related links

Tahadhari Na Ukimwi!

Date: 17 June, 2006

  1. Nataka towa nasaha
    Ya dhati si ya mzaha
    Kuhusu kuu jaraha
    Dunia liloingiya
  2. Jaraha ni la ukimwi
    Janga lake halikomi
    Limekuwa kama zimwi
    Hula mmoya mmoya
  3. Ukimwi dawa hauna
    Tena ni khatari sana
    Kwa wazee na zijana
    Wake na waume piya
  4. Ukimwi ukikushika
    Yuwa zako zimefika
    Ni mno utateseka
    Wewe na wangine piya
  5. Ukimwi hukukondesha
    Damu ukakukausha
    Sura zikawa hutisha
    Jamaa wakukimbiya
  6. Basi ndugu jihadhari
    Ukimwi una khatari
    Kuu mno lake shari
    Ni nyingi zake balaya
  7. Jitunge kila wakati
    Epuka uhasharati
    Sifanye hata katiti
    Mtegoni utangiya
  8. Hiyo ndiyo yake kinga
    aha zote kuzifunga
    Kubali kuwa mjinga
    Salama kuipatiya
  9. Uzinifu si werevu
    Bali ni maangamivu
    Na mangineyo maovu
    Ni chambo hukuvutiya
  10. Muangaliye samaki
    Kinena chambo sitaki
    Asilani humshiki
    Salama atasaliya
  11. Na wewe mwana Adamu
    Mungu mekupa fahamu
    Huwaje ukanywa sumu
    Na hali waangaliya
  12. Fikiri yako maisha
    Kwa nini wayafupisha
    Wanao kuwabakisha
    Yatima bila hatiya
  13. Wewe kwa kutaka raha
    Wengi wawapa karaha
    Haya mambo si mzaha
    Yataka kufikiriya
  14. Wenda kujitumbukiza
    Kwenye janga lenye giza
    Wenzio kuangamiza
    Kwa rahaya mara moya
  15. Wajitiya mayutoni
    Wewe mwenyewe mwendani
    Huu ni ujinga gani
    Kifo kujitafutiya
  16. KIfo si chako wepweke
    Utamuuwa na mke
    Watoto waungulike
    Lipi walilokoseya
  17. Tuate uhasharati
    Na kwa hishima tuketi
    Ukimwi hautupati
    Illa tukiuzengeya
  18. Na zaidi wasichana
    Kadhalika wavulana
    Hawa ndiwo wengi sana
    Kwa ukimwi kupoteya
  19. Wasichana barobaro
    Jiziwiyeni mparo
    Hapo utakwenda ziro
    Ukimwi kutosaliya
  20. Jiepusheni kabisa
    Na za upuzi anasa
    Hizo ndizo huwatosa
    Mtegoni mukangiya
  21. Ukishapija mtindi
    Lolote halikushindi
    Hata koo kwenye landi
    Mwenyewe utaitiya
  22. Wewe ndiye muamuzi
    Na wangine hawawezi
    Ukiamua upuzi
    Mwenyewe utaumiya
  23. Nasaha naikariri
    Tahadhari tahadhari
    Ukimwi kuu khatari
    Inatishia duniya
  24. Kauli yetu tammati
    Ni nasaha kwa umati
    Hayana dawa mauti
    Ukimwi ni moya ndiya

Mahmoud A. Abdulkadir (MAU) - Lamu, Kenya

  About Us | Zanzinet Home | Contact Us | ©2004-2006 Zanzinet