|
|
Tujitahidi na Sunna
- Wazee na as-habu, Akh-wa na ukhtina
Nimeandika kitabu, Kiasi kukumbushana
Kidogo nimekutubu, Si ila kuambizana
Tujitahidi na sunna, Tukamilishe faradhi
- Faradhi iwe kamili, Tujitahidi na sunna
Tufunge tena tusali, Kwa usiku na mchana
Na tukimiliki mali, Twende Maka na Madina
Tujitahidi na sunna, Tukamilisha faradhi
- Aidha zaka tutowe, Kwa amri ya Rabbana,
Walokhusika wapewe, Bila ya kupendeleana
Kwa kipimo wagawiwe, Pasi kudhulumiana
Tujitahidi na sunna, Tukamilishe faradhi
- Tukae tukikumbuka, Kua uhai hapana
Wengi waliotutoka, Wala hawarudi tena
Jambo jema la kushika, Ni kumtii Rabbana
Tujitahidi na sunna, Tukamilishe faradhi
- Tunyanyueni mikono, Tukisikia adhana
Tusali na sala tano, Na dua kuombeana
Tuombe masikizano, Jamii muuminina
Tujitahidi na sunna, Tukamilishe faradhi
- Tujitahidi na dini, Ndio jambo la maana
Na sadaka tutoweni, Ina ubaya khiyana
Tumlaani shetani, Laanahul mal-una
Tujitahidi na sunna, Tukamilishe faradhi
- Tuitambuwe dunia, Kua si kubwa ni duna
Hii dunia ni njia, Twapita si maskana
Dunia yatuzomea, Na huku yatutafuna
Tujitahidi na sunna, Tukamilishe faradhi
- Pana safari lazima, Kubwa mfano haina
Sote inatuandama, Aasi na msalihina
Habakii mtu nyuma, Babu na baba na mwana
Tujitahidi na sunna, Tukamilishe faradhi
- Soteni lazima kwenda, Mbele yake Subhana
Kila tuliyoyatenda, Wenyewe tutayaona
Mwenye lake talipanda, Sayyia au hasana
Tujitahidi na sunna, Tukamilishe faradhi
- Dhalimu na madhulumu, Walo wakikopeshana
Wakae wakifahamu, Siku ya kwenda kutana
Wanaekewa zakumu, Chakula cha kulishana
Tujitahidi na sunna, Tukamilishe faradhi
- Wako wapi watukufu, Walokuwa na majina
Ambao ni maarufu, Na sote tukiwaona
La mwisho ni udhaifu, Hali zao hairana
Tujitahidi na sunna, Tukamilishe faradhi
- Waliokuwa na raha, Wanangiwa na mahana
Wote wapiga siyaha, Kina wakiambiana
Hayupo mwenye furaha, Jamii wanadangana
Tujitahidi na sunna, Tukamilishe faradhi
- Tuwatazame wazuri, Walio wakijivuna
Maringo na ujeuri, Fedhuli na kujiona
Unakwisha uhodari, La kulifanya hawana
Tujitahidi na sunna, Tukamilishe faradhi
- Wako wapi maridadi, Wa vikoi na fulana
Kwenda huku wakirudi, Na kujiona wapana
Sasa hawajisafidi, Unawapata mdhana
Tujitahidi na sunna, Tukamilishe faradhi
- Iwapi ile suhuba, Watu kutemebleana
Kila wendapo washiba, Karamu kupikiana
Jamii wapiga toba, Na wote ni mahuzuna
Tujitahidi na sunna, Tukamilishe faradhi
- Tuwatazame walevi, Waliowakilevyana
Na ukali kama uvi, Na watu kuwatukana
Unawishia ujuvi, Khatima wachukiana
Tujitahidi na sunna, Tukamilishe faradhi
- Ndugu zangu nawambia, Kama kunabihishana
Ni kali mno dunia, Yauma tena yabana
Atakaeichezea, Ajuwe watapambana
Tujitahidi na sunna, Tukamilishe faradhi
- Kuna adhabu akhera, Ya namna kwa namna
Toba ya Rabbi sitara, Allahu mustaana
Tuombeni maghfira, Kwa Rabbil-aalamina
Tujitahidi na sunna, Tukamilishe faradhi
- Niliyowahadithiya, Ni ya kweli si ya dhanna
Kwa maneno yangu haya, Ni kama kuzinduana
Na iwapo ni mabaya, Nawaomba samahana
Tujitahidi na sunna, Tukamilishe faradhi
- Tammati sina la kwamba, Ni bora tatulizana
Lakini radhi naomba, Kwa wazee na vijana
Musije mukanigomba, Ikawa kununiana
Tujitahidi na sunna, Tukamilishe faradhi
Khamis Nassor Al-Nabhany
|