.

Welcome to Zanzinet Swahili Poems

Where Swahili matters!

Ukweli!

 

 

 

 

 

 

Related links

Ukweli !

Date:  06 January, 2007

  1. Ukweli kitu adimu, katika hii dunia,
    Ukweli japo muhimu, watu wanauchukia,
    Ukweli watia hamu, kutaka kuusemea,
    Ukweli waleta hofu, sababu unaumiza.

  2. Ukweli taona kiza, ukitaka kuusema,
    Ukweli utaumiza, utabebeshwa na dhima,
    Ukweli utakimbiza, mamboyo yende mrama,
    Ukweli taleta kifo, sababu unaumiza.

  3. Ukweli unaachisha, kazizenye manufaa,
    Ukweli unahamisha, uende usikojua,
    Ukweli unafupisha, maisha yaliyotua,
    Ukweli unaadui, sababu unaumiza.

  4. Ukweli waleta chuki, jamaa takuhaini,
    Ukweli tapata dhiki, uishipo duniani,
    Ukweli ingawa haki, waja hawauthamini,
    Ukweli una machungu, sababu unaumiza.

  5. Ukweli ukishiriki, mpweke utabakia,
    Ukweli una mikiki, wenzako takukimbia,
    Ukweli hata rafiki, khiyana takufanyia,
    Ukweli warusharoho, sababu unaumiza.

  6. Ukweli utapuuzwa, uonwe usiefaa,
    Ukweli utaburuzwa, khofu itakufikia,
    Ukweli utakatizwa, furaha ulozoea,
    Ukweli taadhibiwa, sababu unaumiza.

  7. Ukweli ukiushika, watachukia nduguzo,
    Ukweli watakuweka, mnyonge bila liwazo,
    Ukweli watakucheka, kwa dharau na mabezo,
    Ukweli utateseka, sababu unaumiza.

  8. Ukweli mesisitizwa, na Allah Mola Jalia,
    Ukweli umehimizwa, waja watu wajibia,
    Ukweli umetukuzwa, kila mtu kuuvaa,
    Ukweli ulete haki, ijapo unaumiza.

  9. Ukweli usidanganye, haki ikatokomea,
    Ukweli haki ufanye, japo wengine talia,
    Ukweli uutawanye, watu wapate zoea,
    Ukweli ulete tija, ijapo unaumiza.

  10. Ukweli ukizoea, raha yake ya pekee,
    Ukweli utazindua, wanyonge wasinyongee,
    Ukweli tasimamia, haki kote isambae,
    Ukweli sio dhuluma, ingawa unaumiza.

  11. Ukweli na tuuvae, tuishi kwa usalama,
    Ukweli tukumbatie, tuziepuke naqama,
    Ukweli tuujengee, hima udumu daima,
    Ukweli ulete nema, ingawa unaumiza.

  12. Ukweli kitamalaki, neema zitajazana,
    Ukweli tandoa dhiki, ufisadi na fitina,
    Ukweli utadiriki, kusimamia amana,
    Ukweli taleta kheri, ijapo unaumiza.

  13. Ukweli pia amani, tajaa na kufurika,
    Ukweli si kisirani, uhasidi tatoweka,
    Ukweli si uhaini, bali haki kuiweka,
    Ukweli iwe ibada, ingawa unaumiza.

Limeletwa na Abdalla Sani

Mtungaji : Mwanoti A. Abdullah (Pemba)

  About Us | Zanzinet Home | Contact Us | ©2004 Zanzinet