Poets Profile
Khamis Bin Nassor Al Nabhany
Sh. Khamis Bin Nassor Bin Khamis Al Nabhany alizaliwa tarehe 18 mfungo 8
mwaka 1338H (Februari 9, 1920) katika kijiji cha Piki wilaya ya Wete mkoa wa kaskazini Pemba.
Ni mtoto peke yake kwa baba na mama kwani wazazi wake waliachana muda
mfupi tu baada ya kuzaliwa. Udogoni kwake alilelewa na mama yake ambae alizaa
watoto wanane na mume wake wa pili na baba yake aliowa mke mwengine na
kuzaa watoto tisa.
Sh. Khamis alisoma Qur-an mpaka kukhitimu chuoni kwa maalim Mtwana bin Marzouk hapo hapo Piki. Hakusoma skuli na mpaka leo hii maandishi yake
alitumia herufi za kiarabu.
Sh. Khamis alianza kutunga mnamo mwaka 1940.
Wakati wa udogo wake, alipenda sana kukaa na ami zake hasa wakati wa jioni kwa
mazungumzo. Miongoni mwao wako ambao wakitunga mashairi jambo ambalo lilimfanya aingie katika utungaji". Siku moja katika
baraza kama hiyo alikuwepo bwana mmoja jina lake Abdulla bin Muhammed ambae alikua
siku hiyo hana furaha kwa khiana aliyofanyiwa na kwa sababu hiyo
alikasirika sana na akatunga shairi ambalo Sh. Khamis alikumbuka beti mbili tu zifuatazo:-
Dhila iliyonifika, kwako wewe l-azizi
Kwa kila nikikumbuka, hunizidisha machozi
Maini yaunguzika, na kusubiri siwezi
Nnarudi na machozi, naliya sinyamaziki
Naliya sinyamaziki, hayakatiki machozi
Mabaya wayashiriki, ukinitenda huwazi
Usidhani siudhiki, ni kathara ya mapenz
Nnarudi na machozi, naliya sinyamaziki
Shairi hili lilimvutia sana Sh. Khamis bin Nassor na ndio
khasa sababu ya yeye kuanza kutunga.
Sh. Khamis alifariki dunia tarehe 2/3/2003 na ameacha kizuka na watoto wanne wote wa kike. Hakubahatika kupata watoto wa kiume kwani mwanawe wa kwanza ambae alikuwa mwanamume alifariki
alipokua mchanga. Wakati wa uhai wake, Sh. Khamis alikuwa fundi wa charahani na pia anajishughulisha na kilimo kama
vile migomba, mihogo na mpunga.
Nimalizie maelezo haya mafupi kwa kunukuu maneno yake mwenyewe kama ifuatavyo:
"Mashairi kwangu si
sehemu ya kazi bali ni moja ya starehe. Hutunga kutokana na matukio na visa mbali
mbali ambavyo tunaviona au wakati tunaokwenda nao".
Ingawa Sh. Khamis ametutoka hapa duniani, sadaka yake ya mashairi itawafaa wengi wanaopenda kusoma tungo za Kiswahili. Mwenyeenzi Mungu ampe malazi mema peponi, Amin.
Ali bin Said Al
Jahdhamy (Kamange)
Mahmoud Ahmad Mahmoud
Maelezo binafsi ya Ustadhi Mahmoud Ahmad Mahmoud:
Mahmoud Ahmed Abdulkadir (MAU) nilizaliwa Amu pwani ya Kenya mwaka 1950 nilisoma madrassa Annajah, sikwenda shule za kawaida.
Ni mwalimu wa madrassa, vile vile nahutubu Ijumaa. Nafundisha somo la dini ya Kiislamu katika shule kadhaa za msingi pia naendesha darasa la watu wazima msikitini. Naelewa vyema
lugha ya kiswahili na pia kiarabu vizuri na kiengereza kwa kadiri Fulani.
Kadhalika naandika mashairir na natumia lahaja ya kiamu. Naandika katika maudhui tofauti tofauti zaidi mambo ya kijamii na vile vile siasa.
Kwa mara ya kwanza nalijitokeza kusoma shairi nililoandika juu ya uhuru wa Kenya baada ya miaka kumi 12/12/1973. kuanzia hapo nilipata umashuhuri nakutangaa kuwa ni mshairi. Mwaka
1974 niliandika “WASIA WA MABANATI” Utendi wenye baiti 140 ambao ulikua ukielezea mikasa iliyompata msichana aliefanya urafiki na mvulana ambae alimtia mimba na baadae akamruka. 1975 – 1979
niliandia tendi tisa kwa jina la kimondo ambazo zilitumika kufanya kampeni wakati wa uchaguzi wa wabunge hapa Lamu. Mimi nilimsaidia Mzamil Omar Mzamil mpinzani wake alikuwa ni Madhubuti na
baada ya hapo niliendelea kuandika mashairi lakini mafupi mafupi na sana huwa ni ya watu binafsi kuhusu mambo yao wenyewe k.m harusi, matanga, safari na kadhalika.
Mwaka wa 2000 niliandika tendi mbili, mmoja kwa jina la UZUNDUZI na wa pili MWANGAZA kujaribu kuwahimiza watu wazundukane na watambue haki zao na kuzitetea. Pia niliandika utendi mrefu
wa baiti 700 juu ya haki za uraia vile vile niliandika tendi juu ya Ukimwi, Mihadharati na haki za watoto.
2004 niliandika tendi mbili kwa anwani ya ramani ya maisha ya ndoa, mmoja wa mume na wa pili wa mke. Pia nimeandika mashairi mafupi kadha moja ni kuhusu Ahmad Yassin na lingine kuhusu
Faluja, IRAQ. Nina nia ya kuandika utendi juu ya haki za wazazi. Babangu pia alikuwa ni mshairir vile vile mamangu. Mtoto wangu wa kwanza ana kipawa cha ushairi lakini haandiki sana. Mimi
nimeoa nina watoto 11, mkubwa na miaka 29 na mdogo ana miaka 8. wasichana ni 7 na wavulana ni wane. Napata mkate wangu wa kila siku kwa uwokaji mikate “BAKERY” kazi ambayo nilirithi kutoka
kwa mlezi wangu Ammi yangu, Bwana Abdulghafur Abdulkadir.
Napendelea sana kusoma vitabu mbali mbali zaidi kwa kiarabu. Napenda kuogelea baharini na kusafiri. Kusoma ndio pumbao langu kubwa!! Mwaka jana 2004 nilitunukiwa tuzo ya “THE HEAD OF
STATE’S COMMENDATION (HSC- CIVILAN DIVISION).